Thursday, February 21, 2013


WAZIRI KAGASHEKI AANZA KUTATUA KERO ZA VIBALI VYA UVUNAJI KATIKA SHAMBA LA MITI SAO HILL


Waziri Kagasheki
Waziri wa Maliasili na Utalii Mheshimiwa Khamis Suedi Kagasheki amewaruhusu watu 292 ambao vibali vyao vilisitishwa mwezi Januari mwaka huu, kutokana na utata uliojitokeza, kuendelea na uvunaji katika Shamba la Sao Hill. Waziri Kagasheki ametoa ruhusa hiyo baada ya kujiridhisha kuwa watu hao walipata vibali hivyo kwa kufuata taratibu za uvunaji.

Mheshimiwa Kagasheki wakati alipotembelea Wilaya ya Mufindi Mkoani Iringa tarehe 25 na 26 Januari 2013 ili kusikiliza kero zilizopo Wilayani humo kuhusiana na Shamba la miti la Sao Hill, aliahidi kufanyia kazi baadhi ya masuala yaliyojitokeza.

Kuhusu suala la vibali 292 vilivyotolewa katika msimu wa mwaka 2012/13 na kusitishwa wakati wa ziara yake, Waziri Kagasheki amelifanyia kazi na kubaini kuwa matatizo na changamoto zilizojitokeza zilitokana na utendaji katika kipindi cha mpito, hususan mabadiliko ya utaratibu wa utoaji vibali vya uvunaji.

Hivyo, wadau hao 292 ambao hawana vibali rasmi vilivyochapishwa kutokana na kutumika utaratibu wa zamani, wameruhusiwa kukamilisha taratibu na kupewa vibali rasmi vya uvunaji.

Ruhusa hii inawahusu wavunaji wote waliofuata taratibu zote za usajili, ikiwa ni pamoja na kupata usajili na kulipia maduhuli na tozo mbalimbali za Serikali ambavyo ndivyo vigezo muhimu vya kumfanya mvunaji kufanya shughuli zake zinazohusiana na masuala yote ya uvunaji.

Wizara ya Maliasili na utalii inaendelea kufanyia kazi kero zote zilizojitokeza wakati wa ziara hiyo Waziri na taarifa itaendelea kutolewa kuhusu utekelezaji wake.

George Matiko
MSEMAJI
WIZARA YA MALIASILI NA UTALII
Tarehe 21 Februari, 2013