Monday, September 3, 2012

RCC SIMAMIENI MIRADI YA MAENDELEO



Wajumbe wa Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Iringa wametakiwa kusimamia vizuri miradi na fedha za Serikali ili kudhibiti matumizi mabaya na hoja zinazoweza kujitokeza kutokana na kutokusimamia vizuri fedha na miradi hiyo.

Rai hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma, wakati akifungua kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Siasa ni Kilimo katika Wilaya ya Iringa.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (katikati) akiendesha kikao cha RCC


Dkt. Christine amesema kuwa katika agenda zitakazojadiliwa ni utekelezaji wa Taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali. “Ninalowasihi ndugu wajumbe, kwa mwaka huu, kuanzia sasa ni kusimamia miradi na fedha ambazo Halmashauri hupewa na Serikali, ili kudhibiti ubadhilifu wa fedha na hoja zinazoweza kujitokeza” asilisitiza Dkt. Christine. Aidha, aliwashauri kutokuanzisha miradi mipya wakati miradi ya zamani haijakamilika na kuwataka kumaliza miradi viporo kwanza ndipo waanzishe miradi mipya.

Mwenyekiti huyo ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Iringa, aliwashauri wajumbe wa kikao hicho kuwashauri wakulima wanaoishi katika maeneo yenye upungufu wa mvua, kulima mazao yanayovumilia ukame. Amesema “nichukue fursa hii kuwaomba kufikisha ujumbe kwa wakulima wanaoishi maeneo yenye upungufu wa mvua, kuwa ni vizuri wakulima walime mazao ya mtama na alizeti ambayo yanavumilia ukame”.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa alitumia kikao hicho kuwataka wajumbe kusimamia suala la utunzaji wa mazingira ambayo kwa sasa yanaharibiwa kwa kasi kubwa na shughuli za binadamu.   
Wakati huo huo, Sekretarieti ya Mkoa wa Iringa imefanikiwa kukusanya zaidi ya shilingi 950,000,000 kwa mwaka wa fedha 2011/ 2012.

Akiwasilisha taarifa ya Utekelezaji wa Mpango na bajeti kwa kipindi cha Julai-Juni, 2011/ 2012, Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Mipango na Uratibu, Nuhu Mwasumilwe amesema kuwa kwa mwaka wa fedha 2011/2012, Sekretarieti ya Mkoa wa Iringa ilikadiriwa kukusanya jumla ya shilingi 903,000. Amesema hadi kufikia mwezi Juni, 2012 jumla ya shilingi 950,895,762 zimekusanywa kwa mchanganuo ufuatao, marejesho ya mishahara ni shilingi 949,591,700, kodi ya pango la nyumba ni shilingi 636,238 na ada ya ufuatiliaji shilingi 19,000.

Mwasumilwe amesema kwa upande wa Serikali za Mitaa, katika kipindi cha mwaka 2011/ 2012, Halmashauri za Wilaya, Miji na Manispaa zilitarajiwa kukusanya jumla ya shilingi 8,342,138,599 kutoka katika vyanzo vyake vya mapato vya ndani. Amesema hadi kufikia mwezi Juni, 2012 jumla ya shilingi 7,358,634,981 zimekusanywa ambazo ni sawa na asilimia 88.2 ya lengo.

VIJIJI VIFUTWE MANISPAA YA IRINGA



Halmashauri ya Manispaa ya Iringa imekuwa ikishindwa kutekeleza baadhi ya mikakati ya mipango ya mji na mipango mingine ya maendeleo kutokana na uwepo wa vijiji saba, jambo linaloleta mkanganyiko wa kiutendaji ndani ya Manispaa.

Akiwasilisha mapendekezo ya kufuta vijiji katika Manispaa ya Iringa katika kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Iringa, Mkurugenzi wa Manispaa ya Iringa, Theresia Mahongo ameitaja sababu kuu ya Halmashauri kutaka kufutwa kwa vijiji hivyo kuwa ni Halmashauri ya Manispaa kupanua mipaka yake kama inavyoelekezwa kwenye fungu la 12 la ‘The Local Government (Urban Authorities) Act, 1982. Amesema kifungu cha 12 kijifungu (1) kinasema kwamba Waziri mwenye dhamana anaweza kutangaza kwenye Gazeti la Serikali kufuta kijiji ama kijiji cha ujamaa kilichoingia kwenye mipaka ya eneo la Mji. 

Akielezea hali halisi, Theresia amesema kuwa Manispaa yake imekuwa ikipata matatizo ya kiutendaji katika maeneo ya vijiji husika na kusababisha baadhi ya mikakati ya mipango ya mji na mipango mingine kutokukamilika. Ameyataja baadhi ya matatizo hayo kuwa ni kufanana kwa baadhi ya kazi za Halmashauri ya Manispaa na Halmashauri ya kijiji jambo linalosababisha kupingana katika suala la kiutendaji na utoaji wa maamuzi. Vilevile, amesema mvutano katika kutekeleza mipango thabiti na madhubuti ya Halmashauri ya Manispaa katika eneo lake la kiutawala na kusababisha baadhi ya mipango kutokutekelezwa katika maeneo ya kiutawala ya kijiji.

Matatizo mengine Mkurugenzi wa Manispaa ya Iringa ameyataja kuwa ni suala la Ardhi ambalo limekuwa ni kikwazo kikubwa katika Mpango wa Mji na vijiji, kwa kuzingatia Sheria zinazolinda vijiji, vijiji vimepewa ruhusa ya kuuza, kuzuia na kuendeleza Ardhi ya kijiji bila ya kuingiliwa na mamlaka yoyote. Ameongeza kuwa Sheria ya Ardhi ya vijiji Na. 5 ya mwaka 1999 kifungu cha 8(1) kinaeleza kuwa Halmashauri ya kijiji kwa kuzingatia masharti ya Sheria hii itawajibika kusimamia Ardhi yote ya kijiji. Amesema kwa tafsiri ya kifungu hicho, Halmashauri ya Manispaa ambayo ndiyo inayoshughulika na Mpango wa Mji, haitakuwa na mamlaka kuingia na kutekeleza Mpango wowote wa Mji katika eneo la kijiji.

Theresia ameyataja manufaa yatakayopatikana baada ya kufutwa vijiji kuwa ni pamoja na Mipango ya Matumizi bora ya Ardhi inayojumuisha huduma muhimu na za msingi kwa jamii inayozingatia Sheria, pamoja na kuongezeka kwa thamani ya Ardhi kutokana na maeneo kupimwa na kupata hati milki. Ongezeko la hali ya kiuchumi na kipato kwa jamii kutokana na kutumia hati katika kuomba mikopo katika asasi za kifedha. Manufaa mengine ameyataja kuwa ni kupungua na kuisha kabisa kwa migogoro na migongano ya Ardhi isiyokuwa ya lazima kutokana na kuzingatia Sheria na Mipango iliyowekwa.

Akitoa hoja, Mkurugenzi wa Manispaa ya Iringa amesema ili kukabiliana na changamoto za kiutawala na kiutendaji, ni muafaka hatua madhubuti zichukuliwe kufuta vijiji vyote ndani ya eneo la Halmashauri ya Manispaa ili kurahisisha utendaji na utekelezaji wa mipango endelevu katika maeneo yanayomilikiwa na vijiji kwa sasa.
Ikumbukwe kuwa Halmashauri ya Manispaa ya Iringa inavyo vijiji saba vilivyosajiliwa kisheria, ambavyo ni Igumbilo, Kigonzile, mgongo, Nduli, Itamba, Mkoga na Kitwiru.

SENSA YA WATU NA MAKAZI



Wananchi Mkoani Iringa wametakiwa kuhakikisha kuwa wanahesabiwa ndani ya siku saba za zoezi la kuhesabu watu ili kuiwezesha Serikali kupata takwimu sahihi na kupanga mipango shirikishi ya maendeleo.

Kauli hiyo ameitoa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma, katika mahijiano ya moja kwa moja na Redio Furaha ya mjini Iringa kupitia kipindi maarufu cha Nyota ya Asubuhi.

Dkt. Christine amesema “msisubiri mpaka siku saba zifike, ukiona imefika siku ya tano yaani tarehe 30.08.2012 hujahesabiwa toa taarifa kwa kiongozi wa Serikali katika eneo lako”. Amesema kuwa wale wanaokaa mijini watoe taarifa zao kwa wenyeviti wao wa mitaa na wale wanaokaa vijijini wahakikishe wanatoa taarifa zao kwa wenyeviti wa vijiji.

Akifafanua kuhusu changamoto ya lugha katika kufanikisha zoezi hilo, Mkuu wa Mkoa amezishukuru juhudi ya hayati baba wa Taifa, Mwl. Julius Nyerere za kuwaunganisha watanzania wote kwa lugha ya kiswahili. Amesema kuwa kwa wale wachache itakaotokea hawafahamu lugha hiyo ni vema wakawaandaa watu wanaowaamini na kuwa wakalimani wao ili kufanikisha zoezi hilo.

Wakati huohuo, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, amewatoa hofu wananchi wote wanaotaka kulihusisha zoezi la Sensa ya Watu na Makazi na dhana ya u-freemarson kuwa zoezi hili hali uhusiano wowote na dhana hiyo na kuwataka wananchi kuwapuuza wale wote wanaotumia dhana hiyo kwa ajili ya kutaka kukwamisha zoezi hilo. 

Akijibu swali juu ya imani ya Serikali katika kuhakikisha kila mwananchi anahesabiwa ndani ya kipindi cha siku saba na upungufu wa makarani wa Sensa, Mratibu Msaidizi wa Sensa Mkoa wa Iringa, Conrad Millinga amesema kuwa Serikali haina wasiwasi juu ya zoezi hilo kukamilika ndani ya muda uliopangwa. Amesema kuwa katika Sensa ya Majaribio iliyofanyika tarehe 02 Oktoba, 2011, ilikamilika ndani ya siku saba na ilifanyika katika maeneo 44 ya kuhesabu watu katika mikoa tisa, mikoa saba ya Tanzania Bara na mikoa miwili ya Zanzibar. Amesema kuwa makarani wapo wa kutosha na katika maeneo yaliyo na idadi kubwa ya kaya wameongezwa makarani wa ziada ili kuhakikisha kuwa zoezi hilo linakamilika katika muda uliopangwa na kwa ufanisi mkubwa. 

WAUGUZI WAMETAKIWA KUTUMIA MAFUNZO KUBORESHA UTOAJI HUDUMA



Wauguzi Mkoani Iringa wametakiwa kutumia mafunzo waliyopata ya kuwajengea uwezo katika kutoa huduma nzuri kwa kuzingatia miiko na maadili ya kazi zao ili mwananchi aweze kunufaika na huduma zao.

Kauli hiyo imetolewa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Robert Salim alipokuwa akifunga mafunzo ya siku mbili ya kuwajengea uwezo katika utoaji huduma Wauguzi kutoka katika taasisi za serikali na binafsi Mkoani hapa.

Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa wa Iringa, Dr. Robert Salim akifunga mafunzo ya Wauguzi


Dkt. Salim amesema “tumieni mafunzo mliyoyapata katika kuboresha huduma za afya katika mkoa wetu wa Iringa”. Amewaasa wauguzi hao kuwa wanao wajibu wa kufanya kazi kwa bidii na kujituma kwa kufuata miiko na maadili ya taaluma zao katika kuihudumia jamii. Amesema lengo la ushirika baina ya serikali na sekta binafsi ni kuhakikisha mwananchi anapata huduma bora kwa upande mmoja na mtoa huduma kuendelea kutoa huduma katika mazingira salama. Amesema kuwa mafunzo hayo pia yamelenga maeneo yenye changamoto hatarishi kama kuzuia maambukizi ya maradhi baina ya mtoa huduma na mpokea huduma, maadili kwa wauguzi na jinsi ya kupambana na kuzuia magongwa ya kuambukiza.

Aidha, Mganga Mkuu wa Mkoa amewataka waganga wakuu wa Wilaya kuanza kufikiria kuingiza katika bajeti na mipango ya maendeleo ya Halmashauri programu za mafunzo ya kuwajengea uwezo wauguzi ili kuyafanya mafunzo hayo yawe endelevu hata baada ya mradi huo kukamilika mwishoni mwa mwaka 2013.

Akielezea matarajio baada ya mafunzo hayo, Mratibu wa mafunzo, Veronica James amesema kuwa matarajio yake ni wauguzi kutoa huduma kitaalamu na kitaaluma zaidi, na uwezo wa kufikisha huduma bora kwa wananchi. Amesema lengo la mafunzo hayo kutolewa kwa wauguzi katika mkoa wa Iringa pia ni kupunguza na hatimae kuondoa kabisa dhana ya huduma zisizo za kuridhisha kwa baadhi ya wauguzi Mkoani Iringa.

James ambae pia ni Meneja wa Hospitali ya Agakhan- Iringa amesema kuwa ili huduma ziweze kuwa bora zaidi dhana ya ushindani lazima ijengeke niongoni mwa wauguzi katika kutoa huduma bora. Amesema kuwa pamoja na kwamba baadhi ya mambo wauguzi wameyasoka wakiwa vyuoni lakini ipo haja ya kuendelea kuwakumbusha ili kuwaamsha zaidi katika kukabiliana na changamoto na utoaji huduma za kila siku.

Meneja wa Agakhan Hospitali Veronica James akifafanua jambo kwa waandishi wa Habari hawapo pichani

Akielezea mafanikio ya mradi huo, Daidu Beyai, Mratibu wa Mradi huo amesema kuwa lengo mahususi la mradi huo ni kuwajengea uwezo wauguzi ili waweze kutoa huduma bora za afya katika Mkoa wa Iringa kwa kuwaongezea ulimu na ujuzi. Ameyataja mafanikio makubwa katika kipindi cha miaka mitatu kuwa ni kuwapatia mafunzo wauguzi 510 katika Mkoa wa Iringa. Amesema katika kufuatilia utekelezaji na ufanisi wa mafunzo hayo kwa wauguzi, tathmini imekuwa ikifanyika kabla ya mafunzo na baada ya mafunzo ili kuona kama mafunzo hayo yanatoa matokeo chanya. Amesema kwa mujibu wa tathmini hiyo wauguzi waliopatiwa mafunzo hayo wameendelea kufanya vizuri katika utekelezaji wa majukumu yao pamoja na kuongeza elimu na ujuzi.   

Akielezea umuhimu wa mafunzo hayo, Eligia Lwela, Muunguzi katika hospitali ya Wilaya ya Mufini, amesema kuwa mafunzo hayo yamemsaidia kuboresha utoaji wake huduma na kuleta ufanisi mkubwa wa kazi yake. Aidha, ameomba mafunzo hayo yawe endelevu ili yaweze kuwafikia wauguzi wote katika Mkoa wa Iringa.

Mafunzo ya kuwajengea uwezo wauguzi katika Mkoa wa Iringa yamefadhiliwa na Shirika la misaada la Marekani kupitia mradi wa Intra Health na kusimamiwa na Hospitali ya Agakhan Iringa.