Monday, September 3, 2012

WAUGUZI WAMETAKIWA KUTUMIA MAFUNZO KUBORESHA UTOAJI HUDUMA



Wauguzi Mkoani Iringa wametakiwa kutumia mafunzo waliyopata ya kuwajengea uwezo katika kutoa huduma nzuri kwa kuzingatia miiko na maadili ya kazi zao ili mwananchi aweze kunufaika na huduma zao.

Kauli hiyo imetolewa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Robert Salim alipokuwa akifunga mafunzo ya siku mbili ya kuwajengea uwezo katika utoaji huduma Wauguzi kutoka katika taasisi za serikali na binafsi Mkoani hapa.

Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa wa Iringa, Dr. Robert Salim akifunga mafunzo ya Wauguzi


Dkt. Salim amesema “tumieni mafunzo mliyoyapata katika kuboresha huduma za afya katika mkoa wetu wa Iringa”. Amewaasa wauguzi hao kuwa wanao wajibu wa kufanya kazi kwa bidii na kujituma kwa kufuata miiko na maadili ya taaluma zao katika kuihudumia jamii. Amesema lengo la ushirika baina ya serikali na sekta binafsi ni kuhakikisha mwananchi anapata huduma bora kwa upande mmoja na mtoa huduma kuendelea kutoa huduma katika mazingira salama. Amesema kuwa mafunzo hayo pia yamelenga maeneo yenye changamoto hatarishi kama kuzuia maambukizi ya maradhi baina ya mtoa huduma na mpokea huduma, maadili kwa wauguzi na jinsi ya kupambana na kuzuia magongwa ya kuambukiza.

Aidha, Mganga Mkuu wa Mkoa amewataka waganga wakuu wa Wilaya kuanza kufikiria kuingiza katika bajeti na mipango ya maendeleo ya Halmashauri programu za mafunzo ya kuwajengea uwezo wauguzi ili kuyafanya mafunzo hayo yawe endelevu hata baada ya mradi huo kukamilika mwishoni mwa mwaka 2013.

Akielezea matarajio baada ya mafunzo hayo, Mratibu wa mafunzo, Veronica James amesema kuwa matarajio yake ni wauguzi kutoa huduma kitaalamu na kitaaluma zaidi, na uwezo wa kufikisha huduma bora kwa wananchi. Amesema lengo la mafunzo hayo kutolewa kwa wauguzi katika mkoa wa Iringa pia ni kupunguza na hatimae kuondoa kabisa dhana ya huduma zisizo za kuridhisha kwa baadhi ya wauguzi Mkoani Iringa.

James ambae pia ni Meneja wa Hospitali ya Agakhan- Iringa amesema kuwa ili huduma ziweze kuwa bora zaidi dhana ya ushindani lazima ijengeke niongoni mwa wauguzi katika kutoa huduma bora. Amesema kuwa pamoja na kwamba baadhi ya mambo wauguzi wameyasoka wakiwa vyuoni lakini ipo haja ya kuendelea kuwakumbusha ili kuwaamsha zaidi katika kukabiliana na changamoto na utoaji huduma za kila siku.

Meneja wa Agakhan Hospitali Veronica James akifafanua jambo kwa waandishi wa Habari hawapo pichani

Akielezea mafanikio ya mradi huo, Daidu Beyai, Mratibu wa Mradi huo amesema kuwa lengo mahususi la mradi huo ni kuwajengea uwezo wauguzi ili waweze kutoa huduma bora za afya katika Mkoa wa Iringa kwa kuwaongezea ulimu na ujuzi. Ameyataja mafanikio makubwa katika kipindi cha miaka mitatu kuwa ni kuwapatia mafunzo wauguzi 510 katika Mkoa wa Iringa. Amesema katika kufuatilia utekelezaji na ufanisi wa mafunzo hayo kwa wauguzi, tathmini imekuwa ikifanyika kabla ya mafunzo na baada ya mafunzo ili kuona kama mafunzo hayo yanatoa matokeo chanya. Amesema kwa mujibu wa tathmini hiyo wauguzi waliopatiwa mafunzo hayo wameendelea kufanya vizuri katika utekelezaji wa majukumu yao pamoja na kuongeza elimu na ujuzi.   

Akielezea umuhimu wa mafunzo hayo, Eligia Lwela, Muunguzi katika hospitali ya Wilaya ya Mufini, amesema kuwa mafunzo hayo yamemsaidia kuboresha utoaji wake huduma na kuleta ufanisi mkubwa wa kazi yake. Aidha, ameomba mafunzo hayo yawe endelevu ili yaweze kuwafikia wauguzi wote katika Mkoa wa Iringa.

Mafunzo ya kuwajengea uwezo wauguzi katika Mkoa wa Iringa yamefadhiliwa na Shirika la misaada la Marekani kupitia mradi wa Intra Health na kusimamiwa na Hospitali ya Agakhan Iringa.

No comments:

Post a Comment