Sunday, May 31, 2015

RCC IRINGA YABARIKI JIMBO LA UCHAGUZI KILOLO KUGAWANYWA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa

Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Iringa imeridhia kwa kauli moja mapendekezo ya kugawa Jimbo la uchaguzi la Kilolo lililopo katika wilaya ya Kilolo kwa lengo la kuboresha utoaji wa huduma bora kwa wananchi.

Katika kikao maalum cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Iringa kilichofanyika katika ukumbi wa Siasa ni Kilimo mjini Iringa kimepitisha kwa kauli moja mapendekelezo ya kugawa Jimbo la uchaguzi la Kilolo na kuanzishwa kwa Jimbo jipya la Ilula.

Akiwasilisha mapendekezo ya kugawa Jimbo la uchaguzi la Kilolo, Kaimu Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Mipango na Uratibu katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Conrad Millinga amesema “wilaya ya Kilolo ipo katika mchakato wa kuanzisha Halmashauri mpya ya wilaya ya Ilula, kwa sababu hiyo tunawasilisha mapendekezo ya kuligawa Jimbo la uchaguzi la Kilolo kuwa Majimbo mawili ya uchaguzi yaani Jimbo la uchaguzi la Kilolo na Jimbo la uchaguzi la Ilula”. 

Amesema kuwa mapendekezo haya yamepitishwa na vikao vya kisheria katika ngazi ya Halmashauri na wilaya na kuvitaja vikao vya Kamati ya Fedha, Mipango na Utawala, Baraza la Madiwani na Kamati ya Ushauri ya Wilaya. Amesema kuwa vikao vyote vimeridhia uanzishwaji wa Jimbo la uchaguzi la Ilula ili kuwezesha kila Halmashauri kuwa na Jimbo lake la uchaguzi na kuepuka Jimbo moja kuwa ndani ya Halmashauri mbili. Sababu nyingine ameitaja kuwa ni kusaidia upatikanaji wa rasilimali na kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Akiongelea hali ya Majimbo yanayopendekezwa kugawanywa, Millinga amesema kwa mujibu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu makadirio ya idadi ya watu katika wilaya ya Kilolo ifikapo Oktoba, 2015 ni watu 235,556. Amesema Majimbo yanayopendekezwa yanakadiriwa kuwa na idadi ya watu kama ifuatavyo; Jimbo la Kilolo watu 115,164 na Ilula watu 120,392. Aidha, ukubwa wa Jimbo la kilolo ni Km za mraba 2,642.5 na Jimbo la Ilula ni Km za mraba 5,232.1. 

Mipaka ya kiutawala, Millinga amesema kuwa Jimbo la Kilolo litakuwa na Kata 12 wakati Ilula Kata 14. 

Afisa Habari ya Wilaya ya Kilolo, Filemon Namwinga amesema kuwa mapendekezo ya kugawa Halmashauri ya wilaya ya Kilolo na Jimbo la uchaguzi la Kilolo yanafanyika katika muda muafaka. Amepongeza vyombo vya maamuzi kufikia hatua hiyo na kusema huo ni uamuzi wa kimkakati unaolenga kuwafikishia wananchi huduma bora. Amesema kuwa sababu za kijiografia na ukubwa wa maeneo ni changamoto kuwa katika kufikisha huduma stahiki kwa wananchi. “Kwa mfano changamoto ya kijiografia kama ukanda wa juu wenye msimu mrefu wa masika na msimu mfupi sana wa kiangazi tofauti na ukanda wa chini wenye msimu mrefu wa kiangazi na masika muda mfupi sana.
=30=

No comments:

Post a Comment