Sunday, May 31, 2015

RC MASENZA AITAKA JAMII KUWEKEZA KWENYE MICHEZO



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Jamii imetakiwa kuwekeza katika michezo kwa wanafunzi ili kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa ajira kwa vijana.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza katika hotuba yake iliyosomwa na Mkuu wa Wilaya ya Kilolo, Selemani Mzee wakati wa ufunguzi wa mashindano ya UMISSETA ngazi ya Kanda ya nyanda za juu kusini yanayofanyika katika Manispaa ya Iringa.

“Wakati taifa kwa sasa likikabiliwa na changamoto ya ukosefu wa ajira kwa vijana, ni vema tukaelekeza nguvu katika kuimarisha sekta ya michezo hapa nchini. Ni imani yangu kuwa endapo michezo itaimarishwa, vijana wengi watapata ajira kuanzia kwenye vilabu vya michezo, vyama vya michezo, mawakala wa wachezi na timu za taifa” alisema Masenza. Vijana wenye weledi wa michezo watakaochukuliwa na timu zilizopo ndani na nje ya nchi na kulipwa vizuri watakuwa na uwezo wa kuwekeza hapa nchini na kuweza kutoa ajira kwa vijana wengine ambao sio wanamichezo. Amesema kuwa wote ni mashahidi kuwa watu wanaoongoza kulipwa fedha nyingi ni wachezaji wenye uweledi.

Amesema kuwa mataifa ya Scandinavia yameweza kupunguza gharama za matibabu katika hospitali mbalimbali kwa wananchi wake kutokana na kuwekeza katika sekta ya michezo. Kutokana na hali hiyo ametaka jamii kushirikiana zaidi katika kukuza sekta ya michezo nchini. “Kwa kufanya hivyo tutaweza kuimarisha afya za wananchi wa mikoa yetu na taifa kwa ujumla na fedha nyingi tunazoelekeza katika sekta ya afya zitawekezwa katika miradi mingine ya maendeleo. Napenda nitoe wito kwa wananchi wa Kanda ya nyanda za juu kusini na taifa kwa ujumla tujenge tabia ya kuipenda michezo ili tuweze kuimarisha afya zetu” alisisitiza Mazenza.

Akiwasilisha taarifa ya UMISSETA Kanya, Mwenyekiti wa UMISSETA Kanda ya nyanda za juu kusini, Mwalimu Asheli Komba amesema kuwa mashindano hayo yanakabiliwa na changamoto za uhaba wa vifaa vya kichezo na viwanja vya michezo. Nyingine ni uhaba wa wataalam wa michezo na baadhi ya shule binafsi kutochangia michezo na kuona shule hizo si sehemu ya mashindano. Changamoto nyingine ameitaja kuwa ni ufinyu wa bajeti zinazotengwa serikalini kwa ajili ya uendeshaji wa shughuli za michezo.
Mwalimu Komba amependekeza halmashauri ziendelee kutenga fedha kadri fursa inavyopatikana ili kuendeleza wataalam wa michezo waliopo katika halmashauri hizo. Aidha, ameshauri kuwa mikoa na halmashauri ziendelee kuhamasisha wadau wa ndani na nje ya mikoa ili waweze kuchangia shughuli za michezo. 

Mashindani ya UMISSETA kitaifa yatafanyika mkoani Mwanza kuanzia tarehe 8-20 Juni, 2015 na Kanda ya nyanda za juu kusini itawakilishwa na wanamichezo mahili 136 wakati michezo itakayoshindaniwa ni mpira wa miguu, kikapu, wavu, riadha, netiboli, meza na bao. Michezo mingine ni tamthilia na ngoma. Kaulimbiu ya mashindano hayo mwaka huu ni michezo ni amani, upendo na mshikamano tujitokeze kuchagua viongozi bora.
=30=

No comments:

Post a Comment