Sunday, May 31, 2015

JIMBO JIPYA LA UCHAGUZI LA MJI WA MAFINGA KUBORESHA HUDUMA KWA WANANCHI



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Kuanzishwa kwa Jimbo la uchaguzi la Mji wa Mafinga litatoa uwakilishi wa watu na kusaidia upatikanaji wa rasilimali na huduma kwa wananchi.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Menejimenti ya Serikali za Mitaa katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Wilfred Myuyu alipokuwa akiwasilisha mapendekezo ya kugawa Majimbo ya Uchaguzi wilaya ya Mufindi katika kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Iringa kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Siasa ni Kilimo katika Manispaa ya Iringa.

Myuyu amesema kuwa mapendekezo ya kugawa Majimbo ya Uchaguzi wilaya ya Mufindi yatatoa nafasi kubwa ya uwakilishi wa watu katika maeneo. Amesema kuwa mapendekezo hayo yatasaidia upatikanaji wa rasilimali na kurahisisha utendaji na utoaji wa huduma kwa wananchi. 

Amesema kufuatia kugawanywa kwa Halmashauri ya wilaya ya Mufindi na kuzaliwa kwa Halmashauri ya Mji wa Mafinga, pendekezo la kuongeza Jimbo moja la Uchaguzi ambali ni Jimbo la Mji wa Mafinga. Amesema kuwa Halmashauri ya Mji wa Mafinga ambayo itakuwa na Jimbo la Mji wa Mafinga ina kilometa za mraba 953. Halmashauri ya wilaya ya Mufindi itabaki na Majimbo ya Mufindi Kaskazini na Mufindi Kusini ikiwa na kimometa za mraba 6,170. 

Akiongelea mipaka ya kiutawala, Myuyu amesema “Jimbo la Mji wa Mafinga litakuwa na Kata tisa, Jimbo la Mufindi Kaskazini Kata 11 na Mufindi Kusini Kata 14. Eneo kubwa la Jimbo la Mji wa Mafinga ni tambarare wakati Majimbo ya Mufindi Kaskazini na Kusini yana maeneo ya milima, tambarare na sehemu za mabonde. kwa mujibu wa makisio ya ongezeko la watu hadi Oktoba, 2015 kwa mujibu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu ni watu 77,364 kwa Mji wa Mafinga, 159,991 kwa Mufindi Kusini na 105,757 kwa Jimbo la Mufindi Kaskazini”.

Myuyu amesema “kama maombi yetu yatakubalika itaepusha mwakilishi mmoja kutumikia Halmashauri mbili tofauti kwa sababu Halmashauri mpya ya Mji wa Mafinga imetokana na Majimbo yote mawili ya Mufindi Kaskazini na Kusini. Kwa sabau hiyo Majimbo mawili ya Mufindi Kaskazini na Kusini yatabaki Halmashauri ya wilaya ya Mufindi wakati Jimbo la Mji wa Mafinga litakuwa Halmahauri ya Mji wa Mafinga”.

Kamati ya ushari ya mkoa wa Iringa imeridhia kwa kauli moja uanzishwaji wa Jimbo la uchaguzi la Mji wa Mafinga.
=30=

No comments:

Post a Comment