Sunday, May 31, 2015

MASENZA AVITAKA VYAMA VYA SIASA KUDUMISHA AMANI



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Vyama vya siasa mkoani Iringa vimetakiwa kudumisha amani na utulivu katika kipindi hiki kuelekea uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipokuwa akifunga kikao maalum cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Iringa kilichofanyika katika ukumbi wa Siasa ni Kilimo.

Masenza amesema “Iringa hatuhitaji vurugu kwa wananchi wetu. Vyama vya siasa waambieni wafuasi wenu kuwa Iringa hatuhitaji vurugu kwa namna yoyote katika kipindi chote kuelekea uchaguzi mkuu na katika uchaguzi mkuu wenyewe. Kamati ya Ulinzi na Usalama ipo makini muda wote na itashughulika na wote watakaojipanga kufanya vurugu”. Amewataka kuingia katika uchaguzi mkuu wakiwa wamoja na kudumisha mshikamano uliopo. 

Mkuu wa Mkoa amewataka kuendelea kushirikiana na kutengeneza timu itakayowezesha kufanikisha majukumu ya kiutekelezaji. Amepongeza juhudi na usimamizi wa Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu katika mchakato wa kuanzisha na kusimamia ugawanaji wa watumishi na mali baina ya Halmashauri ya wilaya ya Mufindi na Halmashauri ya Mji wa Mafinga. “Napongeza kazi nzuri iliyofanywa na Katibu Tawala Mkoa kutokana na uzoefu wake. Yapo maeneo ambayo mgawanyo ulifanyika vibaya kwa kupeleka watu wasiokubalika eneo moja na kufanya utendaji wa kazi kuwa mgumu” alisema Masenza.

Awali akijibu hoja juu ya ushirikishwaji wananchi kwa lengo la kuondoa migongano baina ya wananchi na serikali katika uanzishwaji wa Halmashauri ya wilaya ya Kilolo iliyotolewa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Iringa, Stephen Mhapa, Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu amesema kuwa mgawanyo uliofanyika ni shirikishi na umezingatia hali na mahitaji ya kijiografia hasa maeneo ambayo wananchi walikuwa wanapata changamoto zaidi. Amesema kuwa ramani inaendelea kuandaliwa inayoonesha uhalisia wa maeneo yaliyogawanywa. Akijibu hoja ya changamoto ya mawasiliano, amesema kuwa lengo la mgawanyo huo ni kufanya huduma ya mawasiliano iwe bora kwa wananchi wote.
=30=

No comments:

Post a Comment