Thursday, November 2, 2017

MATUKIO KATIKA PICHA ZIARA YA MKUU WA MKOA KATIKA KATA YA NDULI

MATUKIO KATIKA PICHA ZIARA YA MKUU WA MKOA KATIKA KATA YA NDULI

MENEJA UWANJA WA NDEGE IRINGA APONGEZWA NA MKUU WA MKOA



Na Mwandishi Maalum, Iringa

Meneja wa kiwanja cha ndege cha Iringa amepongezwa kwa kutatua matatizo ya jamii inayouzunguka uwanja wa ndege wa Iringa.

Pongezi hizo zilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, mhe Amina Masenza alipokagua ujenzi wa matundu 10 ya vyoo katika shule ya msingi Nduli iliyopo pembeni mwa uwanja wa ndege wa Iringa katika kata ya Nduli.

Mhe Masenza alisema “pongezi nyingi kwa meneja wa uwanja wa ndege wa Iringa. Tukiwa na watumishi wa umma 10 kama meneja huyu, shule zote zingekuwa na vyoo bora na miundombinu madhubuti”

Alisema kuwa miundombinu bora inawafanya watoto kuipenda shule na walimu kuwahudumia vizuri wanafunzi kwa kuwafundisha kwa moyo. Aliutaka uongozi wa shule hiyo kuvitunza vizuri vyoo hivyo ili viweze kudumu na kuwahudumia wanafunzi wengi zaidi.

Katika taarifa ya mradi wa ujenzi wa choo matundu 10 ya wanafunzi iliyosomwa na mwl Erick Kadope, alisema kuwa shule ya msingi Nduli ilikuwa na vyoo ambavyo si rafiki kwa wanafunzi. 

Mheshimiwa mkuu wa mkoa, kutokana na hali ya choo kuwa si rafiki kwa wanafunzi wetu, kiasi cha kupelekea hofu ya kupatwa na magonjwa ya mlipuko, hivyo meneja wa uwanja wa ndege wa Iringa, bi Hana Kibopile alichukulia uzito wa kipekee ili kunusuru afya za watoto ili wafurahie masomo yao. Aliamua kutafuta mfadhili ambaye ni mdau mkubwa wa maendeleo katika mkoa wa Iringa, anatoka kampuni ya Makota farm” alisema mwl Kadope.    

Akiongelea ujenzi wa choo hicho, alisema kuwa ujenzi ulianza mwaka 2017 na umefikia 90% ikiwa imebaki kazi ya kuweka mabomba ya ndani na kupaka rangi. Alisema kuwa mradi huo umegharimu shilingi 28,000,000.

Ikumbukwe kuwa Shule ya msingi Nduli ilianzishwa mwaka 1969.
=30=


BENDERA NYEKUNDU NYUMBA ZISIZO NA CHOO MANISPAA IRINGA



Na Mwandishi Maalum, Iringa

Mkuu wa mkoa wa Iringa, mhe Amina Masenza ameiagiza halmashauri ya Manispaa ya Iringa kuziwekea bendera nyekundu nyumba zote ambazo hazina vyoo bora na kuzipa muda maalum wa kujenga na kukamilisha vyoo hivyo.

Agizo hilo alilitoa katika shule ya msingi Nduli baada ya kupokea taarifa ya utekelezaji wa ujenzi wa vyoo bora na usafi wa mazingira ya halmashauri ya Manispaa ya Iringa kwa robo ya kwanza Julai-Septemba, 2017.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe Amina Masenza

Mhe Masenza alisema kuwa halmashauri ya Manispaa haina sababu ya kuwa na nyumba isiyo na choo. “Sioni sababu ya halmashauri ya Manispaa kuwa na nyumba ambayo haina choo bora, kwa sabababu nyumba zote zinajengwa kwa ramani baada ya kutolewa kibali cha ujenzi kilichokubaliwa na bwana afya baada ya kujiridhisha kuwa mchoro umebainisha ujenzi wa choo bora” alisema mhe Masenza. 

Aidha, aliitaka Manispaa ya Iringa kuziwekea bendera nyekundu nyumba zote ambazo hazina vyoo bora na kuzipa muda maalum kukamilisha ujenzi wa vyoo na kaya zitakazoshindwa kufanya hivyo hatua za kisheria zichukuliwe. Aliitaka Manispaa ya Iringa kuweka mkakati wa kukamilisha ujenzi wa vyoo kwa kaya ambazo hazina vyoo.

Wakati huohuo, mkuu wa mkoa alimtaka mkuu wa wilaya ya Iringa kutoa maelezo ya sababu zinazofanya baadhi ya nyumba katika Manispaa ya Iringa kutokuwa na vyoo.

Mkuu wa mkoa wa Iringa, alifanya ziara ya siku moja katika kata ya Nduli, Manispa ya Iringa kukagua hali ya usafi wa mazingira na ujenzi wa vyoo.
=30=

NGOs ZATAKIWA KUFANYA KAZI ZINAZOONEKANA



Na Mwandishi Maalum, Iringa
Mashirika yasiyo ya kiserikali yanayotaka kufanya kazi kuwahudumia wananchi mkoani Iringa yatakiwa kufanya kazi zinazoonekana na kupimika.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, Mhe Amina Masenza alipokuwa akiongea na jumuiya ya shule ya msingi Nduli iliyopo katika Manispaa ya Iringa alipofanya ziara ya siku moja ya kukagua hali ya usafi wa mazingira na ujenzi wa vyoo katika kata ya Nduli.

Mhe Masenza alisema kuwa mashirika yote yasiyo ya kiserikali yanayotaka kufanya kazi za kuwahudumia wananchi mkoani Iringa, lazima yaeleze kazi zitakazofanyika na ziwe zinazoonekana na kupimika. 

Alisema kuwa yapo mashirika yasiyo ya kiserikali ambayo yamekuwa yakipata fedha kwa kusingizio cha kuwahudumia wananchi katika usafi wa mazingira lakini yamekuwa hayafanyi hivyo. Alisema kuwa anataka mashirika makini na yanayowajibika kwa wananchi na serikali katika utekelezaji wa majukumu yake.

Akiongelea hali ya usafi wa mazingira katika kata ya Nduli, mkuu wa mkoa alisema kuwa hali ya usafi wa mazingira hairidhishi. 

“Katika ziara hii tumejionea jinsi maeneo mengi yalivyotapakaa takataka, nichukue nafasi hii kuwaagiza watendaji wote, kusimamia ipasavyo zoezi la usafi katika maeneo wanayoyasimamia. Haipendezi kusimamiwa na viongozi katika kazi ambazo ni majukumu yenu ya kila siku” alisema mhe Masenza.
=30=