Tuesday, February 20, 2018

PICHA ZA ZIARA YA NAIBU WAZIRI- MADINI KATIKA MACHIMBO YA NYAKAVANGALA, IRINGA

































MATUKIO KATIKA PICHA ZIARA YA NAIBU WAZIRI BITEKO IRINGA

SERIKALI YATOA MASHARTI MATATU KUFUNGULIWA NGODI WA NYAKAVANGALA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Serikali yatoa masharti matatu kufungua mgodi wa kuzalisha dhahabu Nyakavangala na kuelekeza yatekelezwe ndani ya wiki mbili.

Masharti hayo ambayo ni kupitisha kanuni za uchimbaji madini, wataalam kutoka wizara ya madini kukagua mashimo yote ya kuchimba dhahabu na mafunzo ya usalama katika machimbo yalitolewa na naibu waziri wa Madini, Dotto Biteko aliyefanya ziara ya siku moja katika mgodi wa Nyakavangala uliopo katika Kata ya Malengamakali wilayani Iringa jana.
 
Naibu Waziri wa Madini, Dotto Biteko (Mb)
Biteko alisema kabla ya kufunguliwa mgodi huo mambo hayo matatu lazima yafanyiwe kazi ili kufanya mazingira ya uchimbaji dhahabu kuwa salama. Katika kuhakikisha mazingira yanakuwa sawa, aliwataka wachimbaji hao kuwa wakweli na wazalengo kwa nchi yao katika kiasi cha dhahabu kinachozalishwa mgodini hapo. Akiongelea utoroshaji madini hayo, alisema “mchimbaji anayedhani serikali ya Dr. John Magufuli anaweza kutorosha dhahabu atafute kazi nyingine” alisema Biteko. 

Aliongeza kuwa serikali ipo makini kuhakikisha madini hayo yanawanufaisha watanzania na kuchangia katika uchumi wa Taifa.

Awali mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza alisema kuwa katika kuhakikisha hali ya machimbo dhahabu ya Nyakavangala inakuwa salama, kamati ya ulinzi na usalama Mkoa wa Iringa iliagiza ufanyike ukaguzi katika mashimo yote yanayochimba dhahabu katika mgodi huo. Alisema lengo la ukaguzi huo ni kuwahakikishia usalama wachimbaji hao na kuepuka vifo vitokanavyo na mashimo hayo kuanguka.
=30=

MASENZA AWATAKA WAFANYA BIASHARA KULIPA KODI



Na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa
Serikali mkoani Iringa imewataka wafanyabiashara wote kulipa kodi kwa mujibu wa sheria ili serikali iweze kuwaletea maendeleo wananchi wake.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipokuwa akisalimia wachimbaji wadogo wa mgodi wa nyakavangala katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kijiji cha Nyakavangala kilichopo wilayani Iringa alipokuwa akiongea na wachimbaji wadogo wakati wa ziara ya naibu waziri wa Madini, Dotto Biteko mkoani Iringa jana.
 
Mkuu wa Mkoa, Amina Masenza
Masenza alisema “katika Mkoa wangu, siruhusu mtu yeyote kufanya biashara bila kulipa kodi. Lazima kulipa kodi. Kodi ndiyo inajenga zahanati, kodi ndiyo inajenga shule na miundombinu yote na kodi ndiyo inalipa mishahara”

Alisema kuwa utamaduni wa kulipa kodi ndiyo utawezesha ujenzi wa barabara ya kuelekea katika machimbo ya Nyakavangala kwa kiwango kinachoridhisha.

Aidha, pamoja na kuwapa pole wachimbaji wa dhahabu wa Nyakavangala kufuatia vifo vilivyotokana na ajali zilizotokea siku za nyuma katika mgodi huo, aliwataka kuzingatia kanuni za usalama. “Sitaki vifo katika Mkoa wangu. Lazima kanuni za usalama zizingatiwe wakati wa uchimbaji wa dhahabu”. 

Alisema kuwa ushauri wa wakaguzi wa madini uzingatiwe ili machimbo ya Nyakavangala yawe eneo salama kwa wachimbaji wadogo mkoani Iringa.

Wakati huohuo, mkuu wa Mkoa wa Iringa alimuagiza mkuu wa Wilaya hiyo kwenda kuwasikiliza wananchi waliojaribu kubeba mabango katika ziara ya naibu waziri wa Madini ili kufahamu hoja zao na kuzitafutia ufumbuzi.

Akiongea katika majumuisho ya ziara yake yaliyofanyika katika ofisi ya mkuu wa Mkoa, naibu waziri wa Madini, Dotto Biteko alisema kuwa nchi imempata kiongozi anayethubutu kuhakikisha madini yanawanufaisha watanzania. 

Rais, Dr John Magufuli ana dhamira ya dhati kuyafanya madini yawanufaishe wananchi wa Tanzania na kuchangia katika pato la taifa. Dhamira yake ni kuona madini yanawanufaisha wachimbaji wadogo na hatimae kufikia hatua ya uchimbaji mkubwa” alisema Biteko.
=30=

WACHIMBAJI NYAKAVANGALA WATAKIWA KUJIHADHARI NA UKIMWI



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, IRINGA
Serikali mkoani Iringa imewataka wachimbaji wadogo wa madini ya dhahabu katika mgodi wa Nyakavangala wilayani Iringa kujihadhari ya maambukizi ya virus vya Ukimwi mgodini hapo.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipokuwa akihutubia mkutano wa hadhara wa wachimbaji wadogo katika kijiji cha Nyakavanga wilayani Iringa leo.
 
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza
Masenza alisema kuwa maambukizi ya virus vya Ukimwi katika Mkoa wa Iringa yapo kwa kiwango cha juu. Aliwataka wachimbaji wadogo katika mgodi wa Nyakavangala kujitunza ili kutokupata maambukizi hayo. Alisema asilimia kubwa ya wachimbaji ni vijana ambao ndiyo nguvu kazi ya Taifa. 

Iwapo nguvu kazi hiyo itaugua ugonjwa wa Ukimwi familia zao zitapoteza nguvu kazi na Taifa pia. Vilevile, aliwakumbusha kuwa kipindupindu bado ni changamoto katika baadhi ya maeneo yenye mikusanyiko ya watu wengi.
=30=