Monday, October 24, 2011

IKAMA YA WATUMISHI 662 IRINGA


MKOA wa Iringa umeidhinishiwa IKAMA ya watumishi 662 katika mwaka wa fedha 2011/ 2012 katika kutekeleza majukumu yake.

Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Sehemu ya Utumishi na Utawala kwa mwezi Julai hadi Septemba 2011/ 2012 katika kikao cha kudhibiti Mapato na Matumizi ya serikali katika ofisi yake, kwa niaba ya Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Utawala na Rasilimali watu Afisa Tawala katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Neema Mwaipopo amesema kuwa “kwa kipindi cha Julai- Septemba 2011/ 2012 Sekretarieti ya Mkoa ilipokea IKAMA iliyoidhinishwa mikoa ya Iringa na Njombe”.

Amesema Mkoa wa umeidhinishiwa kuwa na watumishi 662. Amesema kuwa watumishi waliopo ni 578 na nafasi wazi kuwa 84 na kati ya hizo ajira mbadala ni 48 na ajira mpya ni 36.

 Neema Mwaipopo, Afisa Tawala katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa

Amesema kuwa mkoa wa Njombe umeidhinishiwa kuwa na watumishi 423 kati ya 71 waliopo na nafasi wazi 352. Amesema kati ya hizo ajira mbadala ni 10 na ajira mpya ni 342. Aidha, amesema kuwa maombi ya kujaza nafasi wazi 378 katika Sekretarieti ya Mkoa wa Iringa na Njombe na maombi ya kibali cha ajira mbadala 58 yamewasilishwa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma kwa mujibu wa taratibu zilizopo.

Akiongelea mafunzo kwa watumishi katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mwaipopo amesema katka kipindi hicho watumishi wanne wameanza kuhudhuria mafunzo ya muda mrefu katika chuo kikuu cha Tumaini na chuo cha Uhasibu (TIA). Amesema kuwa madhumuni ya mafunzo hayo ni kuimarisha utendaji kazi na ufanisi katika kazi kwa mujibu wa mpango wa mafunzo wa mkoa.

Akifunga kikao hicho Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma (Mb.) amewataka wafanyakazi katika Ofisi yake kufanya kazi kwa umakini mkubwa na uwajibikaji ili kuleta tija katika mkoa na taifa kwa ujumla. Aidha, amewataka kila mtumishi kurejea kipengele kinachomhusu katika Ilani ya uchaguzi ya chama kinachotawala na kuweka utaratibu wa utekelezaji wake.

Kikao cha kudhibiti mapato na Matumizi hufanyika kila baada ya miezi mitatu na hujadili pamoja na mambo mengine mapato na matumizi ya fedha za serikali.

RC AAGIZA MATUMIZI MAZURI YA FEDHA ZA SERIKALI

MKUU wa Mkoa wa Iringa ameagiza matumizi mazuri ya fedha za serikali kadri zilivyopangwa ili ziweze kuwanufaisha wananchi walio wengi katika jitihada za kuondoa umasikini na kuinua maisha ya kila siku.

Agizo hilo limetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma (Mb.) katika kikao cha robo ya kwanza cha kudhibiti Mapato na Matumizi ya serikali katika ofisi yake kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa ofisi yake. 

 Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. christine Ishengoma (Mb.)

Dk. Ishengoma aliyekuwa mwenyekiti wa kikao hicho amesema “lazima fedha za serikali zitumike vizuri kadri zilivyopangwa hasa upande wa miradi ya maendeleo ili ziwanufaishe wananchi wengi”.
Amesisitiza kufuatwa kanuni na taratibu za kihasibu ikiwa ni pamoja na ulipwaji wa madai mbalimbali kwa muda ili kuongeza ufanisi wa kazi na hatimae mkoa kupata hati safi ya kiukaguzi.

Aidha, Mkuu wa Mkoa ameagiza kufanyiwa kazi mapungufu yote yaliyobainishwa katika ripoti ya Mkaguzi na Mthibiti mkuu wa hesabu za serikali kwa mwaka wa fedha 2009/ 2010 mapema na kuwasilisha taarifa hiyo sehemu husika na kuhakikisha mapungufu hayo hayajitokezi kwa mara nyingine. 

Akiwasilisha taarifa ya Mkaguzi wa Nje kuhusu mapungufu yaliyojitokeza katika ripoti ya Mthibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa mwaka wa fedha 2009/2010 kwa mkoa wa Iringa, Mkaguzi Mkazi, Ismail Mbiru amesema kuwa ripoti hiyo imebaini mapungufu kadhaa yaliyoainishwa kwa kila Halmashauri kwa ajili ya kuyatolea majibu sahihi ili kuleta ufanisi katika kusimamia mapato ya Halmashauri.
Mbiru ameyataja mapungufu hayo kuwa ni pamoja na kuwasilisha taarifa zenye mapungufu makubwa, taarifa zenye nyaraka pungufu, taarifa za halmashauri ambazo fedha za mfuko wa maendeleo ya jimbo hazijatumika na kuwasilisha taarifa zenye hati zenye shaka.

Mapungufu mengine ameyataja kuwa ni kuwasilisha taarifa yenye wadaiwa wasiolipa na wasiolipwa, kuwasilisha taarifa zenye mishahara isiyolipwa na haikurejeshwa Hazina na kuwasilisha taarifa ya vitabu vya maduhuli ambayo hayajarejeshwa na mawakala wa kukusanya mapato.