Saturday, October 8, 2011

MKUU WA MKOA WA IRINGA AONGEA NA WAZEE NA VIONGOZI WA DINI IRINGA

Mkuu wa Mkoa wa Iringa Dkt. Christine Ishengoma amewaomba wazee wa Mkoa wa Iringa kumpatia ushirikiano wa kutosha katika jukumu lake la kuuongoza Mkoa huo kwa pamoja waweze kuuletea maendeleo.
Dkt, Ishengoma ameyasema hayo alipoongea na wazee wa Iringa alipokutana nao katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa.


Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (kulia) akiongea na wazee wa Mkoa wa Iringa, kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Bw. Aseri Msangi
Dkt. Ishengoma amesema kuwa wazee ni hazina kubwa katika Mkoa hivyo ushirikiano wao ni muhumu sana katika kulisukuma mbele gurudumu la maendeleo. Amesema “ninaamini kuwa wazee ni chachu ya kuleta maendeleo kwa sababu mumefanya kazi kwa muda mrefu na kukutana na changamoto na mambo mengi katika Mkoa wetu wa Iringa”.
Mkuu huyo wa Mkoa amewafahamisha wazee hao kuwa Ofisi yake ipo wazi muda wote kwa ajili ya kupokea ushauri, kushauri na kushauriana katika mambo ya kuuendeleza Mkoa wa Iringa.
Aidha, amechukua fursa hiyo kuwafahamisha wazee hao kuwa Mkoa unatarajia kuadhimisha maadhimisho ya miaka 50 ya uhuru tarehe 7 hadi 9 Novemba, 2011 itakayoenda sambamba na kukimbiza Mwenge wa Uhuru Mkoani Iringa. Amesema mwaka huu tofayuti na miaka mingine Mwenge wa Uhuru hautakimbizwa Mkoa mzima bali utakimbizwa katika makao makuu ya Mkoa na Iringa utakesha katika uwanja wa Samora.
Wakati huohuo Mkuu huyo wa Mkoa wa Iringa amekutana na viongozi wa madhehebu ya dini ya Iringa katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa majira ya mchana.
Dkt. Ishengoma amesema “viongozi wa dini ndio mliowashika watu hivyo tukishirikiana kwa pamoja mambo yanayohusu maendeleo yatafikiwa haraka”. Amesema kuwa ushirikiano huo baina ya Serikali na madhuhebu ya dini utasaidia hata malezi ya vijana kwa sababu vijana wengi wanaokengeuka wanatoka katika madhehebu ya dini yanayoongozwa na viongozi hao.
Wazee wa Mkoa wa Iringa wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Iringa (hayupo pichani) 
Askofu wa Kanisa la Aglikana Dayosisi ya Ruaha, Bw Joseph Mgomi amesema kuwa Dayosisi yake imekuwa ikifanya kazi nyingi za kijamii kwa kushirikiana na Serikali ili kumletea maendeleo mwananchi wa Iringa na kuahidi kuendelea kushirikiana na Serikali. Amesema miongoni mwa shughuli hizo kuwa ni miradi ya maji na kilimo.  

MUFINDI WASHAURIWA KUANZISHA CHUO KIKUU

Mkuu wa Mkoa wa Iringa amewashauri wanamufindi kuangalia uwezekano wa kuwa na chuo kikuu ili kuwasogezea karibu huduma hiyo muhimu wananchi.
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma wakati akiongea na watumishi wa Serikali kuu, Halmashauri na taasisi mbalimbali katika ukumbi mikutano wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi.
Karibu Wilayani Mufindi, Mhe. Mkuu wa Mkoa
Dkt. Ishengoma amesema “pamoja na kuwa na mafanikio makubwa katika nyanja za uzalishaji na uchumi, Mufindi tufikirie kuwa na chuo kikuu”. Amesema kuwa chuo kikuu ni muhimu sana katika kuzalisha wanataaluma watakaosaidia kusukuma zaidi gurudumu la maendeleo Wilayani hapo. Amesema uanzishwaji wa chuo kikuu Wilayani Mufindi utawasaidia wananchi wengina wa maeneo ya jirani kuvutika katika kujiendeleza kielimu.
Akiongelea sekta ya maji, Mkuu huyo wa Mkoa amesema kuwa sekta hiyo bado inaasilima zilizo chini jambo linalowakoshesha wananchi wengi huduma hiyo. Amesema “kwa pamoja ni lazima tujitahidi ili kuongeza kasi ili tufikie malengo ya matakwa ya sera ya maji”.
Aidha, ameishauri Halmashauri hiyo kuangalia vyanzo vingine vinavyoweza kuiletea mapato ili kuiwezesha Halmashauri hiyo kujiendesha vizuri zaidi. Amesema kuwa Halmashauri inapojiimarisha kimapato inapanua wigo wake wa utoaji huduma kwa wananchi na kupunguza malalamiko kutoka kwa wananchi.
Akiwasilisha taarifa ya Wilaya ya Mufindi kwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Bibi. Evarista Kalalu amesema kuwa ili kuhakikisha kuwa wananchi wanapata maji safi na salama katika umbali usiozidi mita 400, wilaya yake imeongeza miradi ya maji na kuongeza idadi ya watu wenye uwezo wa kupata maji safi na salama kutoka asilimia 40 mwaka 2005/2006 kwa wakazi wa mjini, hadi asilimia 53 mwaka 2010/2011. Aidha, idadi imeongezeka kutoka asilimia 56 mwaka 2005/2006 kwa wakazi wa vijijini, hadi asilimia 61 mwaka 2010/2011.


Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Bibi. Evarista kalalu akisisitiza jambo

Amesema kuwa miradi hiyo ni ya uchimbaji wa visima 35 ambavyo vimewapatia maji wananchi wapatao 8,750 pamoja na ujenzi wa mtego mmoja wa maji ambao unawanufaisha wananchi 2000.
Bibi. Kalalu amesema kuwa uhifadhi wa vyanzo vya maji na rasilimali za maji umeongezeka kutoka vyanzo 100 vilivyokuwa vimehifadhiwa mwaka 2005 hadi kufikia vyanzo 705 mwaka 2010.  Amesema vyanzo hivyo ni vile ambavyo hutiririsha maji yake katika mto wa Ruaha.