Saturday, October 8, 2011

MKUU WA MKOA WA IRINGA AONGEA NA WAZEE NA VIONGOZI WA DINI IRINGA

Mkuu wa Mkoa wa Iringa Dkt. Christine Ishengoma amewaomba wazee wa Mkoa wa Iringa kumpatia ushirikiano wa kutosha katika jukumu lake la kuuongoza Mkoa huo kwa pamoja waweze kuuletea maendeleo.
Dkt, Ishengoma ameyasema hayo alipoongea na wazee wa Iringa alipokutana nao katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa.


Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (kulia) akiongea na wazee wa Mkoa wa Iringa, kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Bw. Aseri Msangi
Dkt. Ishengoma amesema kuwa wazee ni hazina kubwa katika Mkoa hivyo ushirikiano wao ni muhumu sana katika kulisukuma mbele gurudumu la maendeleo. Amesema “ninaamini kuwa wazee ni chachu ya kuleta maendeleo kwa sababu mumefanya kazi kwa muda mrefu na kukutana na changamoto na mambo mengi katika Mkoa wetu wa Iringa”.
Mkuu huyo wa Mkoa amewafahamisha wazee hao kuwa Ofisi yake ipo wazi muda wote kwa ajili ya kupokea ushauri, kushauri na kushauriana katika mambo ya kuuendeleza Mkoa wa Iringa.
Aidha, amechukua fursa hiyo kuwafahamisha wazee hao kuwa Mkoa unatarajia kuadhimisha maadhimisho ya miaka 50 ya uhuru tarehe 7 hadi 9 Novemba, 2011 itakayoenda sambamba na kukimbiza Mwenge wa Uhuru Mkoani Iringa. Amesema mwaka huu tofayuti na miaka mingine Mwenge wa Uhuru hautakimbizwa Mkoa mzima bali utakimbizwa katika makao makuu ya Mkoa na Iringa utakesha katika uwanja wa Samora.
Wakati huohuo Mkuu huyo wa Mkoa wa Iringa amekutana na viongozi wa madhehebu ya dini ya Iringa katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa majira ya mchana.
Dkt. Ishengoma amesema “viongozi wa dini ndio mliowashika watu hivyo tukishirikiana kwa pamoja mambo yanayohusu maendeleo yatafikiwa haraka”. Amesema kuwa ushirikiano huo baina ya Serikali na madhuhebu ya dini utasaidia hata malezi ya vijana kwa sababu vijana wengi wanaokengeuka wanatoka katika madhehebu ya dini yanayoongozwa na viongozi hao.
Wazee wa Mkoa wa Iringa wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Iringa (hayupo pichani) 
Askofu wa Kanisa la Aglikana Dayosisi ya Ruaha, Bw Joseph Mgomi amesema kuwa Dayosisi yake imekuwa ikifanya kazi nyingi za kijamii kwa kushirikiana na Serikali ili kumletea maendeleo mwananchi wa Iringa na kuahidi kuendelea kushirikiana na Serikali. Amesema miongoni mwa shughuli hizo kuwa ni miradi ya maji na kilimo.  

No comments:

Post a Comment