Friday, September 13, 2013

KISIWA CHA SAANANE CHATANGAZWA RASMI HIFADHI YA TAIFA



HIFADHI ZA TAIFA TANZANIA

TAARIFA KWA UMMA


Kisiwa cha Saanane kimetangazwa rasmi kuwa Hifadhi ya Taifa kufuatia Tangazo la Serikali  Namba 227 lililotolewa hivi karibuni.

Kutangazwa kwa Hifadhi ya Taifa ya Kisiwa cha Saanane kunafuatia kupitishwa kwa Azimio la Bunge mwezi Oktoba mwaka jana lililoridhia kupandishwa hadhi kwa kisiwa hicho kutoka Pori la Akiba na kuwa Hifadhi ya Taifa.

Hifadhi ya Taifa ya Kisiwa cha Saanane itakuwa na ukubwa wa kilomita za mraba 2.18 na itajumuisha maeneo ya lililokuwa Pori la Akiba , Visiwa vya Chankende kubwa na ndogo pamoja na eneo la maji ya Ziwa Victoria linalozunguka visiwa hivyo.

Kuanzishwa kwa Hifadhi mpya ya Taifa ya Saanane kutawezesha haja ya kuongeza spishi mbalimbali za wanyamapori na hivyo kuongeza utalii wa mjini, utalii wa ndani, utafiti na kutoa elimu kwa vitendo kwa wanafunzi na wananchi watakaotembelea hifadhi hii mpya.

Aidha, uamuzi huu utasaidia kutunza hali ya bioanuwai, uhifadhi wa mazalia na makuzio ya samaki na uendelezaji wa utalii wa mjini kuendelea kuimarika.

Kabla ya kupandishwa hadhi, Kisiwa cha Saanane kilikuwa Bustani ya wanyama mwaka 1964 kabla ya kupandishwa hadhi kuwa Pori la Akiba mwaka 1991. Ilipofika mwaka 2006, Serikali ilikikabidhi kisiwa hicho kwa Shirika la Hifadhi za Taifa kwa ajili ya kukiendesha na kusimamia mchakato wa kukipandisha hadhi kuwa Hifadhi ya Taifa.

Kufuatia uamuzi huu, Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA) sasa litakuwa na jumla ya Hifadhi 16 nchi nzima ambazo nyingine ni pamoja na Serengeti; Ziwa Manyara; Tarangire na Arusha.

Nyingine ni pamoja na Kilimanjaro; Mkomazi; Saadani; Mikumi; Milima ya Udzungwa; Ruaha; Kitulo; Katavi; Gombe; Milima ya Mahale na Kisiwa cha Rubondo.

Wakati huohuo, eneo la Hifadhi ya Taifa Gombe limeongezwa ukubwa kutoka Kilometa za mraba 33.74 hadi kufikia kilometa za mraba 56. Uamuzi huu unatokana na Tangazo la Serikali Namba 228 lililotolewa hivi karibuni ambalo linafuatia Azimio la Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lililotolewa mwaka jana  linalohusu kuridhiwa kwa uamuzi wa kurekebisha mipaka ya Hifadhi ya Taifa Gombe kwa kuondoa eneo la makaburi na kuliacha kwa wananchi pamoja na kujumuisha eneo la ufukwe wa maji ya Ziwa Victoria na eneo la ukanda wa maji.

Kuongezeka kwa eneo la ufukwe wa ziwa na ukanda wa maji kwenye eneo la hifadhi kutaongeza wigo wa shughuli za utalii katika Hifadhi kama vile kuogelea, utalii wa boti, mitumbwi na uvuvi wa kitalii.

Imetolewa na Idara ya Uhusiano
Hifadhi za Taifa Tanzania
S. L. P 3134
ARUSHA



TENGA AISHUKURU KAMATI YA LIGI




Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga ameishukuru Kamati ya Ligi kwa usimamizi mzuri tangu ilipokabidhi Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) katika mzunguko wa pili msimu uliopita.


Leodegar Tenga, Rais wa TFF
 
Amesema TFF iliamua kuanzisha Kamati ya Ligi kwa lengo la kutaka klabu zijisimamie zenyewe ili kuongeza ufanisi, jambo ambalo limeleta mabadiliko kwa vile hivi sasa hakuna matatizo katika kuwalipa marefa na makamisha wanaosimamia VPL na Ligi Daraja la Kwanza (FDL).

“Fedha za udhamini sasa zinakwenda moja kwa moja kwenye Kamati ya Ligi. Ni matarajio yangu kuwa ufanisi utaongezeka, kwani tumeanzisha jambo hili kwa lengo la kuleta tija, maendeleo na utulivu,” amesema Rais Tenga wakati akizungumza na Wahariri wa Michezo kutoka vyombo mbalimbali vya habari.

Rais Tenga amesema mahali penye utulivu na utawala bora watu wanakuwa na imani hasa katika masuala ya fedha, hivyo ni lazima kwa kampuni kuwekeza kwa vile kunakuwa hakuna vurugu.

Amesema ukiondoa Afrika Kusini na Angola katika ukanda huu wa Afrika Mashariki, Kati na Kusini, Ligi Kuu ya Tanzania ndiyo yenye udhamini mkubwa kupitia mdhamini wa ligi na udhamini wa matangazo ya televisheni.

Pia amesema kuanzia msimu ujao 2014/2015 klabu za Ligi Kuu hazitaruhusiwa kusajili wachezaji hadi zitakapowasilisha TFF ripoti zao za mapato na matumizi zilizokaguliwa (Audited accounts), hivyo klabu husika zijiandae kwa ripoti hizo za Januari hadi Desemba 2013.

Kuhusu tiketi za elektroniki, Rais Tenga amesema bado linafanyiwa kazi na CRDB ambayo ndiyo iliyoshinda tenda hiyo na liko katika hatua nzuri, kwani nia ya TFF na benki hiyo kuona kuwa linaanza haraka iwezekanavyo.

“Tiketi za elektroniki zimechelewa kuanza kwa sababu ambazo haziwezi kuzuilika, lakini CRDB imeshatengeneza miundombinu katika karibu viwanja vyote. Kulitokea uchelewaji katika kuleta printer (mashine za kuchapia), zilizokuja hazikuwa zenyewe. Kwa upande wa Uwanja wa Taifa, system (mfumo) iliyopo inatofautiana na ile ya CRDB. Hivyo sasa tunaangalia uwezekano wa zote mbili zitumike kwa pamoja, kwa sababu Uwanja wa Taifa una system yake tayari. Printer zimeshafika, tunataka ili suala lisitucheleweshe,” amesema.

=30=

WATUMISHI FANYENI KAZI KWA KUJITUMA




W
atumishi mkoani Iringa wametakiwa kufanya kazi kwa kujituma ili kufikia malengo ya serikali ya kuwaletea wananchi maendeleo na matokeo makubwa yanayoonekana.
Kauli hiyo imetolewa na Muu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma alipokuwa akiongea na wafanyakazi wa serikali wilayani Mufindi katika ukumbi wa Halmashauri ya wilaya ya Mufindi kupitia utaratibu wake wa kuongea na kusikiliza changamoto zinazowakabili wafanyakazi wa serikali mkoani Iringa.
Dkt. Christine amesema kuwa kila mfanyakazi wa serikali lazima afanye kazi kwa nafasi yake na kwa kujituma ili kazi yake iweze kwenda vizuri na kufikia malengo ya serikali ya kuwaletea maendeleo wananchi wake. “Kazi hii ni yetu ya kumuendeleza mwana Mufindi na Iringa kwa ujumla. Hivyo, kila mmoja asipende kufanya kazi kwa kuchungwa ni vizuri kujichunga mwenyewe. Lazima muwe na ratiba zenu za kazi na zenye malengo” alisisitiza Dkt. Christine.
Amesema katika kuhakikisha matokeo makubwa yanapatikana na kuonekana kwa wananchi ni vizuri utaratibu wa matokeo makubwa sasa (BRN) ukaanzia nyumbani ili uweze kufahamika vizuri kuanzia ngazi ya familia. Amesema kuwa kabla ya kufikiria kutoa matokeo makubwa kwa ujumla wake ni vizuri kila mfanyakazi akajiangalia yeye mwenyewe. “Lazima uangalie wewe mwenyewe unaendaje na BRN” alisisitiza Dkt. Christine.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa ameyataja maeneo ya vipaumbele katika utaratibu wa matokeo makubwa sasa kuwa ni maji, kilimo, elimu, uchukuzi, nishati na mapato. 

Akiongelea upande wa mapato, amesema kuwa ni lazima halmashauri ya wilaya ya Mufindi ikajipanga vizuri kuhakikisha inaongeza ukusanyaji wa mapato ya ndani ili iweze kutoa huduma bora kwa wananchi. Amesema “halmashauri hii inasikifa kwa uchapa kazi na ukusanyaji wa mapato hivyo hakikisheni mnaitendea haki halmashauri hii isirudi nyuma”alisisitiza Mkuu wa Mkoa.

Mkuu wa Mkoa amekemea vikali siasa katika utekelezaji wa utaratibu wa matokeo makubwa sasa (BRN). Amesema “kwenye utaratibu wa BRN msiweke siasa, mpo hapa kwa ajili ya kutekeleza Ilani ya uchaguzi ya chama cha mapinduzi ya mwaka 2010-2015.siaka kazini ni marufuku, fanyeni kazi za serikali kwa mujibu wa taratibu zilizopo” aling’aka Mkuu wa Mkoa wa Iringa.

Akiongelea maandalizi ya kilele cha mbio za Mwenge wa Uhuru, Kumbukumbu ya Baba wa Taifa Mwl. Julius Nyerere na Wiki ya Vijana, Mkuu wa Mkoa amewataka wafanyakazi hao kushirikiana na viongozi katika kufanikisha sherehe hizo kubwa mkoani hapa. “Amesema shirikianeni na viongozi wenu ikiwa ni pamoja na kutoa ushauri wa kuboresha maandalizi na maadhimisho ya sherehe hizi muhimu katika mkoa na taifa letu kwa ujumla”. 

Akiongelea miradiitakayotembelewa na Mwenge wa Uhuru mkoani Iringa, Mkuu wa Mkoa amezitaka wilaya kuhakikisha kuwa miradi ya Mwenye inakamilika kwa wakati na kwa ubora unaokubalika.

Mkoa wa Iringa umepewa heshima ya kuwa mwenyeji wa kilele cha mbio za Mwenge wa Uhuru, Kumbukumbu ya Baba wa Taifa Mwl. Julius Nyerere na wikiya Vijana kitaifa kwa mwaka 2013.
=30=


BRN KUTEKELEZWA KWA VITENDO IRINGA



Na. Bruno Machary, IRINGA
Serikali Mkoani Iringa imejipanga kutekeleza kwa vitendo utaratibu wa matokeo makubwa sasa (BRN) ili kufikia malengo yaliyowekwa kitaifa ya kutoa huduma bora kwa wananchi.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma

Hayo yamejidhihirisha jana kwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa Mhe. Dkt. Christine Ishengoma kufanya ziara katika Halimashauri za Mkoa wa Iringa kwa lengo la kuhamasisha utendaji wa kazi kwa wafanyakazi wa kada mbalimbali kupitia utaratibu wa matokeo makubwa sasa. Katika ziara hizo pamoja na mambo mengine amekuwa akisikiliza changamoto na kero na kuzipatia ufumbuzi.

Akiongea na wafanyakazi wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa katika ukumbi wa mikutano wa Siasa ni Kilimo mjini Iringa, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Ishengoma amesema kuwa wataalamu hawapaswi kukaa ofisini tu ila wanapaswa kutoka na kuwasikiliza wananchi ili kutatua kero zinazowakabiri kwa urahisi. 

Amesema kuwa wataalamu hao ndio suluhisho la kero hizo zinazowakabili wananchi katika kufikia maendeleo yao ya kiuchumi na kijamii. Amesema kuwa kila mfanyakazi analo jukumu la kujitazama na kujihoji yeye wenyewe jitihada alizofanya katika kufikia malengo ya Serikali.

“Utendaji kazi ubadilike na kila mmoja aipende kazi yake kulingana na kada aliyonayo” amesema Dkt. Ishengoma.

Akiongelea dhana ya mawasiliano katika kuleta ufanisi wa kazi, Mkuu wa Mkoa amesema kuwa mawasiliano ni jambo la muhimu sana kwa wafanyakazi kwasababu yanasaidia kuleta ushirikiano na upendo miongoni mwa wafanyakazi hatimae kuondoa chuki baina yao. Amesema kuwa mawasiliano yanapokuwa mazuri ufanisi wa kazi unakuwa mzuri pia.

Amewashauri wafanyakazi kuwashirikisha wakuu wa idara zao pale wanapokabiliwa na matatizo mbalimbali katika utendaji kazi wao. Amesema kuwa ni vizuri kutatua matatizo yanayojitokeza kupitia vikao rasmi vya idara kabla ya kuyawasilisha ngazi za juu.

Matokeo makubwa sasa (B.R.N) ni utaratibu wa utendaji kazi ulioanzishwa na Serikali kwa lengo la kutoa ufanisi wa kazi unaopimika haraka. Maeneo ya kipaumbele katika BRN ni elimu, nishati, maji, uchukuzi, mapato na kilimo.
=30=