Monday, September 3, 2012

SENSA YA WATU NA MAKAZI



Wananchi Mkoani Iringa wametakiwa kuhakikisha kuwa wanahesabiwa ndani ya siku saba za zoezi la kuhesabu watu ili kuiwezesha Serikali kupata takwimu sahihi na kupanga mipango shirikishi ya maendeleo.

Kauli hiyo ameitoa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma, katika mahijiano ya moja kwa moja na Redio Furaha ya mjini Iringa kupitia kipindi maarufu cha Nyota ya Asubuhi.

Dkt. Christine amesema “msisubiri mpaka siku saba zifike, ukiona imefika siku ya tano yaani tarehe 30.08.2012 hujahesabiwa toa taarifa kwa kiongozi wa Serikali katika eneo lako”. Amesema kuwa wale wanaokaa mijini watoe taarifa zao kwa wenyeviti wao wa mitaa na wale wanaokaa vijijini wahakikishe wanatoa taarifa zao kwa wenyeviti wa vijiji.

Akifafanua kuhusu changamoto ya lugha katika kufanikisha zoezi hilo, Mkuu wa Mkoa amezishukuru juhudi ya hayati baba wa Taifa, Mwl. Julius Nyerere za kuwaunganisha watanzania wote kwa lugha ya kiswahili. Amesema kuwa kwa wale wachache itakaotokea hawafahamu lugha hiyo ni vema wakawaandaa watu wanaowaamini na kuwa wakalimani wao ili kufanikisha zoezi hilo.

Wakati huohuo, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, amewatoa hofu wananchi wote wanaotaka kulihusisha zoezi la Sensa ya Watu na Makazi na dhana ya u-freemarson kuwa zoezi hili hali uhusiano wowote na dhana hiyo na kuwataka wananchi kuwapuuza wale wote wanaotumia dhana hiyo kwa ajili ya kutaka kukwamisha zoezi hilo. 

Akijibu swali juu ya imani ya Serikali katika kuhakikisha kila mwananchi anahesabiwa ndani ya kipindi cha siku saba na upungufu wa makarani wa Sensa, Mratibu Msaidizi wa Sensa Mkoa wa Iringa, Conrad Millinga amesema kuwa Serikali haina wasiwasi juu ya zoezi hilo kukamilika ndani ya muda uliopangwa. Amesema kuwa katika Sensa ya Majaribio iliyofanyika tarehe 02 Oktoba, 2011, ilikamilika ndani ya siku saba na ilifanyika katika maeneo 44 ya kuhesabu watu katika mikoa tisa, mikoa saba ya Tanzania Bara na mikoa miwili ya Zanzibar. Amesema kuwa makarani wapo wa kutosha na katika maeneo yaliyo na idadi kubwa ya kaya wameongezwa makarani wa ziada ili kuhakikisha kuwa zoezi hilo linakamilika katika muda uliopangwa na kwa ufanisi mkubwa. 

No comments:

Post a Comment