Sunday, August 5, 2012

DR. ISHENGOMA ASISITIZA KILIMO CHA KISAYANSI



Zana ya Kilimo Kwanza itafanikiwa kwa wakazi wa kanda ya Nyanda za Juu Kusini kulima kilimo cha kisayansi na kiteknolojia zaidi na kukifanya kilimo kiwe cha kibiashara.

Ushauri huo umetolewa katika majumuisho baada ya mgeni rasmi Dkt. Christine Ishengoma kutembelea mabanda ya maonesho ya Nanenane kanda ya nyanda za Juu Kusini katika siku ya mkoa wa Iringa (Iringa Day) iliyofanyika katika uwanja wa maonesho ya Nanenane wa John Mwakangale Uyole Mbeya.

Dkt. Chrisrine ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema “kimsingi kilimo kwanza ni Nyanda za Juu Kusini yaani Mikoa ya Iringa, Njombe, Ruvuma, Mbeya, Rukwa na Katavi kwa kuwa mikoa hii ndio wazalishaji wakubwa nchini, hivyo huwezi kutenganisha Kilimo Kwanza na Nyanda za Juu Kusini”.  Amesema katika kuendeleza kilimo katika ukanda huo ni lazima kilimo kiwe cha kisayansi na kiteknolojia zaidi ili kuwawezesha wakulima kulima maeneo madogo lakini kwa kupata mazao mengi zaidi na yenye ubora unaotakiwa. Amesema kuwa wakulima wameendelea kupata hasara katika kilimo kwa kutokufuata kanuni za kilimo bora jambo linalowafanya waweke nguvu nyingi katika kilimo lakini matokeo wanayoyapata hayaendani na nguvi halisi waliyowekeza katika kilimo hicho. Aidha, ametoa wito kwa wataalam wa kilimo kuwa karibu zaidi na wakulima ili kuwafundisha waweze kuepukana na kilimo cha kizamani na kimazoea.
Hapa huitaji maelezo zaidi ya picha kujieleza yenyewe

Akiongelea kuhama kutoka katika kilimo kidogo kwa ajili ya kujitosheleza kwa chakula, amesema “umefika wakati sasa wa kuhama kutoka katika kilimo cha kawaida na kukifanya kilimo chetu kiwe cha kibiashara. “Na hili litawezekana pale tu tutakapokifanya kilimo chetu kuwa kilimo cha kisayansi zaidi” amesema Dkt. Christine.

Mkuu huyo wa Mkoa wa Iringa amesema baada ya kutembelea mabanda ya maonesho mikoa yote inafanya vizuri. Amesisitiza kuwa ili maonesho hayo yawe mazuri zaidi ni vema maandalizi yake yakaanza mapema zaidi katika Halmashauri zote.

Akielezea nini amejifunza katika maonesho hayo, amesema kuwa amejifunza mambo mengi sana ambayo baadhi hakuwa akiyafahamu kabisa, baadhi amejikumbusha baada ya kupita muda mrefu tokea ayafahamu na kusema “maonesho yaha yamekuwa ni shamba darasa kwa watu wengi”. Baada ya kujionea ubunifu wa kiteknolojia kutoka kwa wananchi mbalimbali, ametoa wito kwa mikoa hiyo ya nyanda za juu kusini kuwaangalia wabunifu hao kwa jicho la pekee ili waweze kuwaendeleza zaidi na wao kunufaika na ubunifu wao. Amesema kuwa imani yake ni kwamba pale juhudi za pamoja zitakapowekwa hakika kilimo kitatoka katika hali yake ya sasa na kuwa bora zaidi.

Wakati huohuo, Mkuu wa Mkoa wa Iringa ameweka rekodi katika maonesho hayo ya Nanenane baada ya kutembelea mabanda 40 ya maonesho kwa siku na kupokea maelezo na kuuliza baadhi ya maswali kwa waoneshaji mbalimbali.

=30=

No comments:

Post a Comment