Wednesday, October 16, 2013

MKE WA RAIS AZINDUA JENGO LA WATOTO KATIKA HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA




Serikali inatambua na kuthamini mchango unaotolewa na wananchi wa Italia katika kuboresha huduma za matibabu kwa watoto kwa lengo la kupunguza vifo vya watoto.

Kauli hiyo imetolewa na Mke wa Rais, Mama Salma Kikwete katika hotuba yake kwenye uzinduzi wa jengo la huduma za watoto katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa.


            Mama Salma Kikwete akizindua jengo la Watoto 
 
Mama Salma amesema “tupo hapa kuzindua jengo la kutolea huduma za watoto. Lakini kabla ya kuzindua jengo hili, naomba niwashukuru sana serikali ya Italia kwa msaada waliotoa kulijenga jengo wa Tshs. 1,842,000,000”. Amesema kuwa serikali ya Tanzania inatambua na kuthamini mchango mkubwa waliotoa wananchi wa Italia kwa wananchi wa Tanzania. “Kwa mchango huu, wananchi wa Italia wametambua umuhimu wa kuboresha huduma za matibabu kwa watoto, ambazo zitasaidia kupunguza vifo vya watoto” alisisitiza Mama Salma. Ameongeza kuwa jengo hilo litapunguza msongamano wa watoto wagonjwa wodini na kuboresha huduma za afya ya watoto katika hospitali ya rufaa ya mkoa.

Akiongelea uhusiano kati ya hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa na hospitali ya Vicenza ya mkoa wa Veneto nchini Italia Mama Salma amesema kuwa uhusiano huo unapaswa kuimarishwa na kuheshimiwa kwa sababu unaboresha utoaji wa huduma za afya katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Iringa.

Kutokana na hospitali nyingi kulalamikiwa kuhusu utoaji huduma usiridhisha, Mama Salma ameitaka hospitali ya rufaa ya mkoa kuwa mfano katika utoaji huduma bora kwa wananchi. Amewataka madaktari na wauguzi wa hospitali hiyo kutoa huduma kwa kujituma, uadilifu, uzalendo na kutumia lugha rafiki inayoweza kumfariji mgonjwa.

Akiwasilisha taarifa ya mradi wa kuboresha huduma za mama na mtoto inayohusisha ujenzi wa jengo la kujifungulia mama wajawazito na ujenzi wa wodi ya watoto katika hospitali ya rufaa ya mkoa, mganga mkuu wa mkoa wa Iringa, Dk. Robert Salim amesema kuwa lengo la mradi ni kuboresha huduma za kujifungua, kupunguza vifo vya wajawazito na vifo vya watoto wachanga vinavyotokana na baridi, kukosa hewa na kupunguza msongamano. Amesema mradi huo pia utapunguza maambukizi ya magonjwa kwa mama waliojifungua na kuboresha utoaji wa huduma kwa urahisi kwa mama wajawazito wanaojifungua wanaojifungua kwa kuwa na eneo kubwa la kufanyia kazi.

Dk. Salim amesema kuwa kutokana na kuongezeka kwa magonjwa ya kuambukiza na vifo vya watoto chini ya miaka mitano, msongamato katika wodi ya watoto, kukosekana kwa chumba cha kuhudumia watoto walio mahututi, chumba cha kuhudumia watoto njiti na wenye utapia mlo mkali, ofisi ya mkuu wa mkoa wa Iringa kwa kushirikiana na hospitali rafiki ya Vicenza ya Italia iliona ni vema kuwa na wodi maalumu kwa ajili ya kuwahudumia watoto katika hospitali ya rufaa ya mkoa.
=30=




No comments:

Post a Comment