Tuesday, October 4, 2011

LUDEWA NI PEMBEZONI NA WAPI?? AHOJI RC

Mkuu wa Mkoa wa Iringa Dkt. Christine Ishengoma ametofautiana na uongozi wa Wilaya ya Ludewa katika dhana inayoendelea kuwa Wilaya ya Ludewa ipo pembezoni.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa amehoji alipokuwa akizungunza na watumishi na wananchi wa Wilaya ya Ludewa alipofanya ziara ya kujitambusha na kuzifahamu changamoto zinazoikabili Wilaya ya Ludewa.
Dkt. Ishengoma amesema “kuanzia sasa Ludewa hatupo pembezoni”. Aidha, amehoji kuwa Ludewa ipo pombezoni na wapi? Ameendelea kuhoji kuwa “kama Ludewa ipo pembezoni je, mwanzoni ni wapi”.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (Mb.) akiongea na watumishi na wananchi wa Wilaya ya Ludewa
Amesema kuwa maendeleo ndiyo dira inayoipeleka Wilaya pembezoni au mwanzoni. Amesema kwa mujibu wa taarifa ya Mkuu wa Wilaya na hali halisi aliyokutana nayo njiani inaonesha kuwa Wilaya hiyo inayo maendeleo yanayoonekana na kupimika.
Amewataka viongozi na wananchi wa Wilaya ya Ludewa kuachana na dhana hiyo kwani inawafanya kujiona kuwa ni wanyonge na hivyo kujiweka pembeni na dhana ya maendeleo na uwajibikaji kikamilifu.
Aidha, amewataka wanaludewa kuchangamkia fursa iliyopo ya ujenzi wa viwanda na machimbo Chuma cha Liganga na Makaa ya Mawe ya Mchuchuma ili kujumuika katika mchakato wa kujiletea maendeleo.
Akiongelea kero inayowakabili wananchi wa Wilaya hiyo ambayo ni barabara, amesema kuwa barabara za Wilaya hiyo zitajengwa kwa sababu zimeainishwa katika ilani ya uchaguzi ya chama tawala.
Dkt. Ishengoma ametoa ombi kwa watumishi wote wa Umma kuendelea kuipenda serikali yao kwa sababu inawajali na kutekeleza mahitaji yao ikiwa ni pamoja na kuwaletea maendeleo. Vilevile, amewataka kuwajibika kwa serikali yao kwa kuchapa kazi kwa bidii.
Akiongelea miradi ya maendeleo, amewataka watumishi na viongozi wanaosimamia miradi ya maendeleo kwa kutekeleza wajibu huo kulingana na thamani halisi ya fedha za Umma zinazotolewa.
Awali akiwasilisha taarifa ya Wilaya ya Ludewa, Mkuu wa Wilaya hiyo Bibi. Georgina Bundala amesema kuwa Wilaya yake inajishughulisha na shughuli za kiuchumi ikiwa ni pamoja na kilimo (90%), biashara (3%), uvuvi, sekta binafsi (4%) na ajira rasmi (3%).  Amesema kuwa Wilaya yake ina fursa nyingi zinazohitaji kuendelezwa ili ziweze kuchangia katika pato la Wilaya na uchumi wa mwananchi. Amezitaja fursa hizo kuwa ni utajiri mkubwa wa madini ya chuma, makaa ya mawe, dharabu, chokaa na vito mbalimbali vya thamani.
Bibi. Bundala amesema kuwa kwa takwimu za mwaka 2008 wastani wa pato la mwananchi Wilayani Ludewa lilikuwa ni shilingi 125,000 kwa mwaka. Amesisitiza kuwa pato hilo ni dogo sana kukidhi mahitaji muhumu ya kibinadamu. Amesema kuwa mkakati wa Wilaya yake ni kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara ili kuongeza pato la mwananchi kuendana na viwango vya kimataifa.
Amesema kuwa Wilaya yake inaendelea kuhamasisha jamii kuweza kukuza kilimo cha kahawa, pareto, chai, korosho, alizeti, ufuta, karanga na kupanua kilimo cha umwagiliaji.
=30=

No comments:

Post a Comment