Tuesday, October 4, 2011

RC ASISITIZA MASOMO YA SAYANSI LUDEWA

Mkuu wa Mkoa wa Iringa awataka wanafunzi wa shule ya sekondari ya Lugarawa kitilia mkazo masomo ya sayansi ili waweze kulitumikia taifa katika fani hizo.
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma wakati akifungua daharia ya wasichana katika shule ya sekondari ya Lugarawa iliyopo katika kata ya Lugarawa Wilayani Ludewa.

Dkt. Ishengoma amesema kuwa wanafunzi wengi hasa wa kike wamekuwa wakiyakimbia masomo ya sayansi kwa kisingizio cha ugumu wa masomo hayo jambo alilolikanusha. Amesema “masomo ya sayansi si magumu kama yanavyodaiwa na wengi, masomo yote yanahitaji juhudi na kujituma ili kuweza kufaulu”.  Amesisitiza kuwa elimu ni msingi wa maisha na maendeleo katika kila jamii inayohitaji kustaarabika.
Amesema “wazazi wamekuwa wakijitahidi kujenga miundombinu ya kielimu kama shule, maabara na daharia kutokana na mapenzi yao kwenu (wanafunzi)”. Amesisitiza kuwa kwa msingi huo wanafunzi nao wanajukumu la kurudisha shukrani zao kwa wazazi kwa kufauli vizuri mitihani yao na hatimae kuwa raia wema watakaolijenga taifa lao.
Aidha, amewataka wazazi na jamii ya Ludewa kugeukia pia uwekezaji katika ujenzi wa daharia za wavulana kwa sababu nazo ni muhimu sana katika kudhibiti makuzi ya wanafunzi hao wavulana.
Kwa mujibu wa taarifa ya wananchi wa Kata ya Lugarawa iliyowasilishwa kwa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, ujenzi wa daharia hiyo ulianza mwaka 2008 hadi mwaka 2010 lengo likiwa ni kuwawezesha wanafunzi wa kike 48 katika shule hiyo kukaa shuleni na kufuatilia masomo yao na kuepukana na hadha za kukaa nje ya shule ikiwa ni pamoja na kupata mimba.
Daharia hiyo iligharimu shilingi milioni 30,785,500 na wananchi wamechangia kiasi cha shilingi milioni 28,085,500 zikiwa ni gharama za kufyatua tofari na fedha taslimu. Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa ilichangia shilingi milioni 2,700,000 kwa upigaji bati na saruji.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, yupo katika ziara ya kujitambulisha na kuzifahamu changamoto zinazozikabili Wilaya za Mkoa wa Iringa na kukagua na kuhimiza shughuli za maendeleo.
=30=

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma (Mb.)(katikati) na Mkuu wa Wilaya ya Ludewa Bibi. Georgina Bundala (kushoto) wakibadilishana mawazo alipowasili Wilayani Ludewa.

No comments:

Post a Comment