Wednesday, December 12, 2012

MKOA WAHIMIZA KILIMO CHA UMWAGILIAJI MAJI





Mkoa wa Iringa umedhamilia kuhakikisha kilimo kinainuka na kukua zaidi kwa kuhamasisha matumizi ya zana bora za kilimo kwa lengo la kumletea maendeleo mwananchi kupitia sekta ya kilimo.

Rai hiyo imetolewa na Mhandisi wa Kilimo, Victor Byanjweli wakati akifafanua mipango ya Mkoa katika kukuza kilimo na kukifanya kiwe cha kisasa katika mkutano wa hadhara katika kijiji cha Ifunda kilichopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa.

Mhandisi Byanjweli amesema kuwa kilimo ni sekta kubwa inayoajiri idadi kubwa ya wananchi katika mkoa wa Iringa, kwa msingi huo uongozi wa mkoa umedhamilia kuhakikisha kilimo kinasonga mbele na kuwaletea maendeleo makubwa wananchi wake. Amesema katika kuhakikisha hilo, Mkoa unaendelea kuhamasisha matumizi ya zana bora za kilimo kwa lengo la kumletea maendeleo mwananchi. Amezitaja zana hizo kuwa ni pamoja na matrekta makubwa na madogo na kilimo cha kutumia wanyama kazi. 

Mhandisi Byanjweli ambaye pia amebobea katika umwagiliaji na zana za kilimo amesema kuwa mkakati mwingine wa Mkoa ni kuhakikisha kilimo kinakua kupitia kilimo cha umwagiliaji. Amesema kutokana na mabadiliko ya tabia nchi na tabia za kibinadamu za ukataji miti ovyo, sehemu kubwa ya Mkoa wa Iringa imekuwa ikipata ukame mkubwa kutokana na upungufu wa mvua usio wa kawaida, Mkoa unahimiza kilimo cha umwagiliaji ili kuondokana na changamoto ya upungufu wa chakula. 

Mhandisi Byanjweli amesema kuwa kupitia kilimo cha umwagiliaji Mkoa utakuwa na uhakika wa chakula na kuondokana na aibu ya kuomba chakula cha njaa.

Wakati huohuo, Afisa Elimu Mkuu, Mwl. Euzebio Mtavangu ametoa wito kwa ubia baina ya walimu na wazazi katika kuhakikisha mwanafunzi anahudumiwa na kulelewa vizuri ili aweze kufanya vizuri katika masomo yao. Amesema miongoni mwa ubai huo ni kuhakikisha kuwa wazazi wanawapokea vizuri walimu wanaopangiwa katika maeneo yao jambo litakalowafanya walimu hao nao kujiona ni miongoni mwa wanajamii na wazazi wa wanafunzi wao. Amesema kufanya hivyo si tu kunamchango kwa mwalimu kujisikia yupo nyumbani na mikononi mwa watu wanaomjali lakini pia kwa utoaji mzuri wa elimu kwa wanafunzi.

Aidha, amewataka wazazi kuhakikisha wanajipanga na kuwapatia wanafunzi chakula cha mchana. Akielezea umuhimu wa chakula cha mchana kwa wanafunzi, Afisa Elimu Mkuu amesema kuwa wanafunzi wanapokula chakula cha mchana kunawasaidia kurudi katika hali ya kawaida na kuondokana na njaa na uchovu jambo linalowafanya wasome kwa bidii na maarifa. Amesema kuwa mwanafunzi anapokuwa ameshiba hata uwezo wa kufikiri na kufaulu unaongezeka sambamba na kupunguza utoro usio wa lazima.

Akihitinisha mkutano huo, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma amewataka wananchi wa kijiji cha Ifunda kuhakikisha wanaunda vikundi kwa ajili ya shughuli za kiuchumi na kuimarisha vyama vya kuweka na kukopa Saccos kwa manufaa yao. Amesema kuwa Serikali muda si mrefu pembejeo zitapitishiwa katika Saccos imara hivyo wananchi watakao mufaika ni wale watakao kuwa wamejiunga katika saccos hizo. Amesema kuwa mkoa wake unahamasisha uundaji wa vikundi vya vijana na vikundi vya kiuchumi kwa malengo ya kuwafanya wananchi wawe na vikundi vya kuzalisha mali kwa kuunganisha nguvu pamoja. Amesema kuwa umoja ni nguvu hivyo watu wakiwa pamoja ni tofauti na anavyokuwa mtu mmoja mmoja.
=30=

No comments:

Post a Comment