Tuesday, January 7, 2014

SERIKALI IONGEZE SHULE ZA VIPAJI MAALUM



Serikali imeshauriwa kuandaa mkakati wa kitaifa wa kuongeza idadi ya shule za sekondari za bweni na vipaji maalum kutokana na idad ya wanafunzi kufaulu na kupanda kila mwaka ili kuwatendea haki na kulinda vipaji vya watoto.

Ushauri huo umetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Bibi. Evarista Kalalu wakati akichangia katika kikao cha uchaguzi wa wanafunzi wa kujiunga na kidato cha kwanza kwa mkoa wa Iringa kilchofanyika katika ukumbi wa Siasa ni Kilimo mjini Iringa.

Bibi. Kalalu amesema ufaulu wa wanafunzi unapanda na kuongezeka lakini sekondari za bweni na vipaji maalum haziongezeki jambo linalosababisha kutokuwatendea haki wanafunzi wengi waliofaulu vizuri kukosa nafasi katika shule hizo. Ameshauri kuwa uwepo mkakati wa kitaifa wa kuongeza shule za bweni na vipaji maalum ili kuwapatia fursa watoto wengi zaidi.

Wakati huohuo, Mbunge wa Mufindi Kusini, Bw. Menrad Kigola ameshauli viwepo vyuo vikuu vya vipaji maalum nchini ili kulinda vipaji vya wanafunzi wanaomaliza shule za sekondari. “Tunazo shule za sekondari za vipaji maalum chakushangaza watoto wetu wanapomaliza sekondari wanajiunga na vyuo vikuu vya kawaida jambo linalochangia kupoteza vipaji vya watoto wetu. Umefika wakati wa serikali kuwa na vyuo vikuu vya vipaji maalum ili kulnda na kuendeleza vipaji vya watoto wetu” amesisitiza Bw. Kigola.  

Akifunga kikao hicho, Mwenyekiti wa kikao hicho ambae pia ni Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Iringa, Bibi. Wamoja Ayubu amewataka wakurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha wanafunzi wote waliochaguliwa wanaripoti na kuanza masomo shule zitakapofunguliwa. Aidha, amewataka kuhakikisha vikao vya tathmini ya elimu na kuzipongeza shule zilizofanya vizuri katika mtihani wa kumaliza elimu ya msingi mwaka 2013. 

Bibi. Ayubu amewata kuweka mikakati endelevu ili mwaka 2014 Mkoa wa Iringa ufikie asilimia 70 ambalo ni lengo la Matokeo Makubwa Sasa kwa mwaka huo. Vilevile, amewataka kuhakikisha Kata ambazo zimechukua wanafunzi wengi zaidi kuliko uwezo wa vyumba vya madarasa vilivyopo, kuhakikisha madarasa yanajengwa haraka ili kukidhi idadi ya wanafunzi stahili. Katika kuendeleza ubora wa elimu mkoani, Kaimu Katibu Tawala Mkoa amewataka wakurugenzi kuhakikisha usimamizi na ufuatiliaji unakuwa wa karibu zaidi na kufanya ukaguzi wa mara kwa mara shuleni ili kuondoa tatizo la wanafunzi wasiojua kusoma na kuandika.  
=30=

No comments:

Post a Comment