Thursday, March 26, 2015

MAJI MBEYA KUTOA LITA ZA UJAZO 51,000



Na. Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Jiji la Mbeya
Mamlaka ya Majisafi na usafi wa mazingira Jiji la Mbeya ina uwezo wa kutoa maji lita za ujazo 51,000 kupitia vyanzo vyake 13 vya maji.

Katika risala ya wafanyakazi wa Mamlaka ya Majisafi na usafi wa mazingira Jiji la Mbeya iliyosomwa kwa mgeni rasmi na Fundi Mkuu, Kanda namba 1 Amiri Abdallah Sapi Mkwawa amesema kuwa mahitaji halisi ya maji katika Jiji la Mbeya ni mita za ujazo 38,000 kwa siku. Amesema kuwa mahitaji hayo hupanda wakati wa kiangazi kufikia mita za ujazo 43,000 kwa siku katika miezi ya Septemba hadi Novemba. Amesema kuwa Mamlaka ina jumla ya vyanzo 13 vya maji vyenye uwezo wa kutoa mita za ujazo 49,000-51,000 kwa siku. Amevitaja vyanzo hivyo kuwa ni Ivumwe I na Ivumwe II, Nzovwe, Imeta, Sisimba, Hanzya, Mfwizimo. Vyanzo vingine ni Nsalaga, Lunji, Mwatezi, Mkwanana, Iduda na Halewa. Amesema kuwa baadhi ya vyanzo vinapungukiwa maji wakati wa kiangazi kutokana na ukame na shughuli za kibinadamu kama uchomaji wa moto, kilimo na ukataji wa miti kwa ajili ya kuni na mkaa.

Mkwawa amesema kuwa katika kuhakikisha rasilimali maji inaendelea kuwepo, Mamlaka kwa kushirikiana na wadau imeendelea na jitihada za kuhakikisha kuwa vyanzo vya maji vinahifadhiwa. Amesema kuwa Mamlaka yake inahakikisha kuwa miundombinu ya majisafi na majitaka iliyopo inatunzwa. “Ili kulipa uzito suala hili Mamlaka kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo Jeshi la Polisi, Jeshi la kujenga Taifa, JWTZ, Wakala wa Misitu Tanzania (TFS), Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) imeunda kamati ya mazingira kwa lengo la kuhifadhi vyanzo vya maji vilivyomo kwenye safu za mlima Mbeya ambapo leo hii utaikabidhi kamati sehemu ya vitendea kazi” Mkwawa. 

Mkuu, Kanda namba 1 amesema kuwa Mamlaka imeweza kuzalisha majisafi na salama na kuyasambaza kwa asilimia 96 ya wakazi wa Jiji la Mbeya. Amesema katika kuboresha miundombinu ya majisafi na majitaka katika Jiji la Mbeya fedha za ndani na fedha za wafadhili zimeendelea kutumika. Mradi wa awamu ya pili na mradi wa kupeleka maji uwanja wa Ndege wa Songwe ni miongoni mwa maboresho yaliyofanyika. 

Amesema katika kukabiliana na uharibifu wa miundombinu dira za maji, Mamlaka imeendelea kuwabaini na kuwachukulia hatua za kisheria baadhi ya wezi wa maji. Hatua nyingine ni kuhifadhi vyanzo vya maji kwa kushirikiana na wadau mbalimbali. 

Akiongelea changamoto zinazoikabili Mamlaka ya Maji, Mkwawa amezitaja kuwa ni baadhi ya wateja hasa taasisi za umma kutokulipa ankara za maji kwa wakati au kutokulipa kabisa. Changamoto nyingine ni baadhi ya vyanzo vya maji vimeendelea kupungukiwa na maji, kutokana na uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabia nchi akitolea mfano chanzo cha mto Lunji na Mfwizimo na Iduda.

No comments:

Post a Comment