Tuesday, July 26, 2016

IRINGA KUWAENZI MASHUJAA KWA KUFANYA KAZI



  Na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Wakazi wa Mkoa wa Iringa wametakiwa kuwaenzi mashujaa waliopigana vita vya ukombozi kwa kufanya kazi kwa juhudi na maarifa kwa lengo la kujiondolea umasikini na kujiletea maendeleo.

Kauli hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipokuwa akitoa salamu za Mkoa katika maadhimisho ya siku ya mashujaa katika mkoa wa Iringa iliyofanyika katika uwanja wa mashujaa Manispaa ya Iringa.
Masenza alisema “leo tunaenzi kumbukumbu ya mashujaa wa nchi yetu, ambao walipigana vita kutetea uhuru na heshima ya nchi yetu na ulinzi wa mipaka yetu. Katika kuwaenzi mashujaa wetu wananchi wanatakiwa kufanya kazi kwa juhudi na maarifa katika kujiondolea umasikini”. Aliongeza kuwa mashujaa wa nchi hii walipigania ukombozi wa nchi kwa lengo la kuwaletea wananchi maendeleo.

Masenza ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Iringa aliwataka wananchi kudumisha umoja na mshikamano mkoani hapa akielezea kuwa umoja na mshikamano ndiyo nyenzo ya kuwaletea maendeleo wananchi. Aliwataka wananchi kupinga matendo yanayolenga kuhatarisha amani na usalama wa nchi. Aliongeza kuwa usalama wa mkoa pamoja na mambo mengine, unategenea pia malezi sahihi ya watoto. 

Aidha, aliwataka wazazi na jamii kwa ujumla kuwalea watoto katika misingi inayokubalika ili wawe raia wema na wazalendo kwa nchi yao. Alisema kuwa uzalendo wa kweli unategemea sana na malezi sahihi ya watoto. 

Nae Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Richard Kasesela alisema kuwa hali ya usalama katika Wilaya ya Iringa ni shwari kutokana na vyombo vya ulinzi kuwa vimejipanga vizuri. “Wilaya ya Iringa tunaweza kulala usingizi vizuri kwa sababu wapo watu wanaokesha kwa ajili ya usingizi wetu na watu hao ni vyombo vya usalama” alisema Kasesela. Aidha, aliwasilisha ombi kwa Meya wa Manispaa ya Iringa kutenga eneo lingine la kuadhimishia maadhimisho ya mashujaa kubwa ambalo litatoa wigo kwa wananchi wengi zaidi kushuhudia maadhimisho hayo tofauti na eneo la sasa.
=30=

No comments:

Post a Comment