Tuesday, July 26, 2016

WATUMISHI SERIKALI ZA MITAA WATAKIWA KUSHIRIKIANA NA WAKURUGENZI WAPYA IRINGA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Watumishi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa watakiwa kutoa ushirikiano mzuri Wakurugenzi walioteuliwa hivi karibuni na Rais ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

Kauli hiyo ilitolewa na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Selemani Jafo alioikuwa akiongea na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa katika ukumbi wa Siasa ni Kilimo, mjini Iringa jana.


Jafo alisema kuwa ili Wakurugenzi waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo, ushirikiano baina ya watumishi na wakuu wa idara ni muhimu na kuwataka watumishi hao kuwapa ushirikiano mzuri Wakurugenzi hao wateule. “Wakurugenzi wapya hakikisheni mnatengeneza mtandao mzuri na wafanyakazi wote. Wapo baadhi ya watumishi kazi yao ni kutengeneza makundi ya fitna kwa Wakurugenzi ili wawachukie baadhi ya watumishi. Mkurugenzi ukikumbatia watumishi wa aina hiyo, basi watumishi hao watakupeleka mahali pabaya” aliongeza Jafo.


Kuhusu ukusanyaji wa mapato, Naibu Waziri alisema kuwa haridhishwi na ukusanyaji mapato hasa vijijini ambapo maeneo mengi hayatumii mfumo wa kieletroniki katika kukusanya mapato ya serikali. “Mapato ya ndani yanaathiriwa sana na mfumo dhaifu wa ukusanyaji mapato, ndiyo maana maelekezo ya serikali ni kutumia mfumo wa kieletroniki katika kukusanya mapato. Mapato ya ndani yasipokusanywa yanatuathiri sote na kushindwa kutekeleza majukumu yetu ikiwa ni pamoja na kwenda vijijini kwa wananchi kufanya kazi” aliongeza Jafo.

Alisema kuwa wapo baadhi ya watumishi wasio waadilifu ambao wametengeneza mfumo wa ulaji kupitia mfumo wa ukusanyaji mapato ya Halmashauri na kumtaka Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo kuwa makini katika kudhibiti mianya ya uvujaji wa mapato ya serikali.

Naibu Waziri huyo, alisema “agenda ya Rais, John Magufuli ni mabadiliko ya kiuchumi, na wananchi wote wanataka mabadiliko ya kweli. Mabadiliko hayo lazima yaletwe na watumishi wa Halmashauri kwa kutimiza wajibu wao katika kufanya kazi. Kama sekta ya maji, afya, elimu, ujenzi na sekta nyingine hazitaenda sawa katika kutekeleza majukumu yake ni dhahiri kuwa wananchi watailalamikia serikali yao, malalamiko hayo yatatokana na baadhi ya watumishi wa Halmashauri kutotimiza wajibu wao”.

Alimshauri Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo kupitia taarifa za kibenki za Halmashauri hiyo na kujiridhisha na mwenendo wa matumizi ya fedha za serikali kabla ya kuingia katika vikao vya Kamati ya fedha ili kudhibiti matumizi yasiyo sahihi ya fedha za serikali.
=30=

No comments:

Post a Comment