Friday, October 7, 2011

TUMIENI SKIMU YA MWAGILIAJI -RUAHA MBUYUNI



Wananchi wa Kata ya Ruaha Mbuyuni wametakiwa kuitumia skimu ya umwagiliaji ya Ruaha Mbuyuni kwa shughuli za kilimo ili kujiletea maendeleo ya kiuchumi.

Kauli hiyo ameitoa Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma wakati alipofanya ziara ya kukagua shughuli za kilimo katika skimu hiyo ya umwagiliaji ya Ruaha Mbuyuni iliyopo katika kata ya Ruaha Mbuyuni.

Dkt. Ishengoma amesema “Ruaha Mbuyuni mnalo bonde zuri sana ila halitumiki ipasavyo kwa shughuli za kilimo cha umwagiliaji, lazima hali za wanaruaha mbuyuni zibadilike kutokana nakuinuka baada ya serikali yenu kuwatengenezea mrefeji na banio la maji”. Amesema baada ya kulitembelea bonde hilo na skimu ya umwagiliaji ya Ruaha Mbuyuni ni dhahili kuwa shuguli za kilimo bado kipo chini sana na kushauri hamasa itolewe kwa wananchi kuitumia skimu hiyo kwa kilimo cha kisasa ili waweze kuvuna zaidi ya mara moja.

Awali akisoma taarifa ya utekelezaji wa mradi wa umwagiliaji wa kijiji cha Ruaha Mbuyuni Afisa Mtendaji wa kijiji hicho, Nassoro Almasi amesema kuwa mwezi Aprili mwaka 2008 mto Lukosi ulihama katika mkondo wake wa asili na kuacha miundombinu ya umwagiliaji ikiwemo banio kutokana na mafuriko yaliyosababishwa na mvua zilizonyesha ukanda wa juu wa Wilaya ya Kilolo. 

Amesema kuwa madhara ya mvua hizo yalisababisha ekari 500 za mazao ya chakula ambayo ni mahindi, mpunga, maharage, vitunguu, nyanya na mbogamboga kuathirika kwa ukame na kusimamisha shughuli za kilimo.

Skimu ya umwagiliaji ya Ruaha Mbuyuni ilianza miaka ya sabini baada ya wakulima wenyewe kuchepusha maji kwa kutumia mawe, magogo, matete na majani ili kumwagilia mashamba yao. 


No comments:

Post a Comment