Thursday, August 9, 2012

KILIMO HAI KIPEWE MSISITIZO ZAIDI



Wakulima wa Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini wameshauriwa kutumia kilimo hai katika kujihakikishia uhai wa mazingira na usalama wa chakula kwa kukuza kipato na kupunguza gharama za uwekezaji katika kilimo.

Ushauri huo umetolewa na Lawrence Mgora, mkulima mwezeshaji wa kilimo hai kutoka taasisi ya uenezi wa elimu ya ugani na kilimo hai.

Akiongelea maana ya kilimo hai amesema kuwa ni kilimo kinachoangalia uhai wa mazingira, uhakika na usalama wa mlaji na usalama wa chakula jambo ambalo linamuhakikishia mkulima kipato kwa kutumia fursa alizonazo mkulima.

Mgora amesema kuwa ili kilimo kiwe kilimo hai ni lazima ulimaji wake ufuate kanuni za kilimo hicho. Amezitaja kanuni hizo kuwa ni pamoja na matumizi ya mbolea ya asili kama mchuzi wa mmea, uji wa mmea na lishe ya mmea katika uzalishaji wa mazao kwa kupandia na kukuzia. Kanuni nyingine amezitaja kuwa ni dawa za asili katika kudhibiti mmea shambani na katika hifadhi ya mazao pamoja na tiba asilia kwa mifugo wa aina yote. 

Akiongelea kwa mifano hai mafanikio ya kilimo hai kwa mkulima na jamii, Mkulima mwezeshaji huyo ameyataja kuwa ni kuongezeka kwa mapato kwa heka. Amesema kuwa kwa mujibu wa tafiti walizofanya, mavuno ya mahindi yanayopatikana ni magunia 34 kwa heka kwa kutumia kanuni za kilimo hai ukilinganisha na magua 18 kwa kutumia kilimo cha kisasa. Ameongeza kuwa uzito wa mazao nao huongezeka, kwa debe la mahindi lililolimwa kwa kanuni za kilimo hai huwa na uzito wa kilo 22 ukilinganisha na kilo 18 kwa debe la mahindi lililolimwa kisasa. Akiongelea uhufadhi wa mazingira, amesema kuwa kilimo cha kisasa uharibu udongo jambo linalomlazimu mkulima kutumia mbolea mara kwa mara wakati kilimo hai kinahifadhi mazingira.

Akielezea nafasi ya ushirika katika kumsaidia mkulima wa Wilaya ya Kilolo, Afisa Uhirika Wilaya, Biezel Malia, amesema kuwa ushirika katika wilaya ya Kilolo umekuwa unalenga katika kumuwezesha mkulima kupata masoko ya mazao na mitaji kupitia Saccos na taasisi za kifedha. Amesema pia kupitia ushirika wilaya ya Kilolo imeweza kuwahakikishia wakulima upatikanaji wa pembejeo za kilimo na zana za kilimo kama pawatila, matrekta.

Amesema pamoja na juhudi za wilaya kuwawezesha wakulima kupata mikopo kupitia Saccos na taasisi za kifedha, ipo changamoto ambayo wanachama wengi sio waaminifu katika kurejesha marejesho ya mikopo yao. Aidha, amesema kuwa changamoto nyingine ambayo wilaya yake inaifanyia kazi ni uhamasishaji juu ya umuhimu wa kuweka akiba ili kuweza kukopa baadae. Afisa Ushirika huyo amesema kuwa katika kukabiliana na changamoto hiyo ngazi ya wilaya, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2012/2013 wilaya yake imetenga fedha za kutosha kutoa mafunzo ya kina kwa wakulima na wajasiliamali itakayoenda sambamba na elimu ya mikopo kwa wanachama wa Saccos.

Wilaya ya Kilolo ina aina nne ya vyama vya ushirika, vikiwepo vyama vya ushirika vya mazao (9), vyama vya akiba na mikopo (13), ushirika wa wapiga picha (1) na vyama vya wavuvi (2).
=30=

No comments:

Post a Comment