Wednesday, August 22, 2012

WAZAZI WASHAURIWA KUSHIRIKI KATIKA MALEZI YA WATOTO



Wazazi wameshauriwa kutoa ushirikiano kwa walimu katika malezi ya wanafunzi ili kuhakikisha jamii inakuwa na watu wenye nidhamu na maadili mema. 

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma alikokuwa akiongea na wananchi, walimu na wanafunzi wa shule ya sekondari Ilambilole iliyopo katika Kata ya Nduli, Wilayani Iringa.

Dkt. Christine amesema kuwa suala la nidhamu kwa wanafunzi haliishii shuleni pekee bali ni jukumu la jamii nzima kuhakikisha inawasaidia walimu katika malezi ya wanafunzi. Amesema “nidhamu inaanzia nyumbani hivyo lazima tusaidiane na walimu katika kudumisha nidhamu ya watoto wetu, lakini tukiwaachia walimu peke yao hatuwezi kufanikiwa. Walimu wana nafasi yao katika kukuza na kudumisha nidhamu na wazazi pia wana nafasi yao katika hili”.

Akiongelea changamoto ya upungufu wa walimu wanaofundisha masomo ya sayansi, Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa upungufu huo upo kwa sababu wanafunzi wengi hawataki kusoma masomo ya sayansi. “Tunaupungufu wa walimu wa masomo ya sayansi kwa sababu watoto wetu hawasomi masomo ya sayansi” alisisitiza Mkuu wa Mkoa wa Iringa. Katika kukabiliana na hali hiyo, alishauri wanafunzi wahamasishwe kusoma masomo ya sayansi ili kuweza kuziba pengo hilo. Aidha, alisema kuwa Serikali inaendelea na mipango ya muda mrefu ya kuhakikisha changamoto hiyo inabaki historia.   

Akiwasilisha taarifa ya shule ya Sekondari ya Ilambilole, Mkuu wa shule hiyo, Vicent Ngaya amesema kuwa shule yake inakabiliwa na changamoto ya upungufu wa vyumba za walimu na walimu wa masomo ya sayansi. Changamoto nyingine ameitaja kuwa ni kukosekana kwa mabweni hasa kwa wanafunzi wa kike na umbali wa makazi ya walimu kutoka shuleni jambo linalosababisha kuchelewa kufika shuleni na kufika wakiwa wamechoka sana.
Kuhusu ufauli, Ngaya amesema kuwa shule imepata mafanikio makubwa katika ufaulu wa wanafunzi, ambapo kwa mwaka 2010 ufaulu ulikuwa ni asilimia 78 na mwaka 2011 ufaulu ulikuwa ni asilimia 61.

Wakati huohuo, suala la wivu limeelezwa kuwa halina nafasi katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi litakalofanyika usiku wa kuamkia tarehe 26 Agosti, mwaka huu. Kauli hiyo imetolewa na Mratibu Msaidizi wa Sensa Mkoa wa Iringa, Conrad Millinga wakati akifafanua masuala mbalimbali ya Sensa katika Kijiji cha Ikengeza, Wilaya ya Iringa. Millinga amewataka akina baba kutokuwa na dhana ya wivu wa aina yoyote pindi wake zao watakapokuwa wakihojiwa na makarani wa Sensa kwa sababu baadhi ya maswali yatawahusu akina mama pekee. Amesema maswali hayo hayatahusiana na ndoa bali ni masuala ya uzazi na kuwataka kuwapatia uhuru na nafasi pindi watakapokuwa wanahojiwa ili kuiwezesha Serikali kupata takwimu sahihi.

Millinga amesema kuwa Sensa ya Watu na Makazi ni muhimu sana kwa nchi kwa sababu pasipo kufahamu idadi sahihi ya watu inawezekana wananchi kupewa huduma pungufu ya mahitaj yao. Amesema Sensa hiyo itawahusisha watanzania wote na wageni watakaokuwa ndani ya nchi siku hiyo ya Sensa.
=30=

No comments:

Post a Comment