Tuesday, March 12, 2013

TANZANIA YAPUNGUZA VIFO VYA WATOTO




Tanzania imefanikiwa kupunguza idadi ya vifo vya watoto walio na umri chini ya miaka mitano kwa asilimia 45 kutokana na kuhimiza matumizi ya chanjo dhidi ya kujikinga na magonjwa mbalimbali nchini.

Hayo yamesemwa na mratibu wa chanjo kitaifa toka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Zebina Msumi wakati akiwasilisha mada juu ya hali ya chanjo nchini katika semina ya waandishi wa habari wa mikoa ya Iringa, Njombe na Ruvuma kuhusu kuanzishwa kwa chanjo mpya za pneumococcal na rotavirus iliyofanyika katika ukumbi wa chuo kikuu huria tawi la Iringa.

Zebina amesema kuwa Tanzania kama nchini nyingine zinazoendelea inafanya juhudi kubwa ili kufikia malengo ya milenia ya nne na tano ifikapo mwaka 2012. Amesema katika juhudi hizo, Tanzania imefanikiwa kupunguza vifo vya watoto walio na umri chini ya miaka mitano kutoka 147 mwaka 1999 hadi kufikia vifo 81 kwa kila watoto 1,000 waliozaliwa hai, hilo likiwa ni punguzo la asilimia 45. Aidha, vifo vya watoto chini ya mwaka mmoja vimepungua kutoka 99 hadi kufikia 51 ilikuwa ni punguzo la asilia 49. 

Amesema kuwa mafanikio hayo yanatokana na viwango vya chanjo kuendelea kupanda kutoka asilimia 50 miaka ya 60 hadi kupindukia asilimia 90 mwaka 2011.

Akielezea huduma ya chanjo nchini, mratibu huyo amesema kuwa imethibitika kitaalamu kuwa chanjo mkakati muafaka katika kutokomeza maradhi na kupunguza vifo vya watoto na kupunguza gharama kubwa ambazo familia na taifa kwa ujumla limetumia katika kutibu maradhi yatokanayo na magonjwa yanayozuilika kwa chanjo. Ameyataja magonjwa yanayokingwa kupitia mpango wa chanjo kuwa ni kifua kikuu, polia, dondakoo, pepopunda, kifaduro, homa ya ini, homa ya uti wa mgongo, surua na vichomi.

Kwa upande wa changamoto zilizopo, Zenina amezitaja kuwa ni vimelea vya  Streptococcus pneumoniae ni kisababishi kikuu cha maradhi na vifo vitokanavyo ugonjwa wa vichomi na homa ya uti wa mgongo. Ameongeza kuwa vimelea vya “rotavirus” kwa upande mwingine husababisha takribani asilimia 80 ya maradhi na vifo vitokanavyo na kuharisha kukali kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano duniani.

Ameitaja mikakati iliyopo kuwa ni chanjo ya “pneumococcal” (PCV13) kukinga maambukizi ya vichomi kwa asilimia 38 na homa ya uti wa mgongo kwa karibia asilimia 87 na chanjo ya “rotavirus” inayokinga kuharisha kukali kunakosababisha vifo vya watoto kwa asilimia 80; na kwa sehemu kubwa kukinga ugonjwa wa kuharisha unaosababishwa na vimelea vya aina nyingine pia.

Mikakati mingine ameitaja kuwa ni Serikali na Wadau wa maendeleo  kuhakikisha kuwa chanjo zinapatikana kwa walengwa wote na kwa muda unaotakiwa na miundombinu ya kuhifadhi na kusafirisha chanjo imeimarishwa  kuwezeshwa kutunza.

Vilevile, chanjo za PCV13 na Rotarix zimeshawasili nchini na zimesambazwa mikoa yote  na watumishi kupatiwa mafunzo ya jinsi ya kutoa chanjo hizi mpya.
Mtoa mada amewata wanahabari hao kuwahimiza akina mama kunyonyesha maziwa ya mama pekee kwa miezi sita na kuimarisha usafi wa mazingira na kunawa mikono kwa sabuni husaidia kupunguza mambukizo ya magonjwa ya kuhara.   

Vilevile, amesisitiza kuwa chanjo ya Rotarix itatolewa pamoja na chanjo zingine  zinazotolewa katika kliki na ratiba ya chanjo  inatolewa mtoto akiwa na wiki 6 na 10. Chanjo hii inatolewa bure katika vituo vinavyotoa huduma za chanjo nchini kama ilivyo kwa chanjo zingine.
=30=

No comments:

Post a Comment