Tuesday, March 12, 2013

SERIKALI YATHAMINI MCHANGO WA VYOMBO VYA HABARI



Serikali inatambua na kuthamini mchango wa vyombo vya habari nchini katika kuhabarisha na kuhamasisha jamii katika kufanikisha kampeni za afya kuanzia ngazi ya kijiji hadi Taifa.

Kauli hiyo imetolewa na Gloria Tesha alipokuwa akitoa mada juu ya majukumu ya vyombo vya habari katika huduma za chanjo nchini katika ukumbi wa Chuo kikuu Hurua tawi la Iringa.

Gloria amesema “vyombo vya habari vina uwezo na ushawishi mkubwa katika kuhamasisha jamii kupitia mfumo na uongozi uliopo kuanzia ngazi ya kijiji hadi Taifa katika mikakati yote ya maendeleo ya nchi ikiwemo huduma za afya”.

Amesema kuwa uwezo wa vyombo vya habari umejidhihirisha katika kutoa habari sahihi na muhimu kwa muda muafaka kwa jamii kwa lengo la kuelimisha, kuhabarisha na kuhamasisha wananchi kushiriki katika huduma na kampeni mbalimbali. “Habari zinaiwezesha jamii kufahamu mambo mbalimbali na kuwa na uwezo wa kufanya maamuzi sahihi” alisisitiza Gloria.

Akielezea mchango wa vyombo vya habari katika kufanikisha kampeni za afya, amesema kuwa ushiriki wa vyombo vya habari katika uanzishwaji wa chanjo mpya ni nyenzo muhimu katika mchakato mzima wa kuboresha afya ya watoto nchini na kufikia malengo ya milenia. Amesema dhana hii inakubalika kutokana na ukweli ulivyo kulingana na historia ya mchango wa vyombo vya habari ilivyo katika maendeleo ya Tanzania. Amesema Wizara inategemea kuwa vyombo vya habari vitawakilisha ujumbe kwa jamii katika uanzishwaji wa chanjo mpya; pamoja na lengo la nne la milenia linalolenga kupunguza vifo vya watoto chini ya miaka mitano kwa theluthi mbili ifikapo 2015.

Kuhusu ujumbe kwa jamii kupitia vyombo vya habari juu ya chanjo ya Rotavirus amesema magonjwa ya kuharisha husababishwa na vimelea vya aina mbalimbali lakini virusi vya Rota huchangia kwa kiwango kikubwa katika magonjwa ya kuharisha kwa watoto walio na umri wa chini ya miaka mitano. Amesema virusi vya Rota huenezwa kwa njia ya kula na /au kunywa maji yaliyochafuliwa na kinyesi chenye virusi hivyo.

Amesema kuwa dalili kuu za ugonjwa huo ni kutapika na kuharisha na mara nyingine huambatana na homa. Ameongeza kuharisha huchukua kati ya siku 4 hadi 7 sambamba na upungufu wa maji mwilini.

Mtoa mada huyo ameelezea njia za kujikinga kuwa ni kumnyoshesha mtoto maziwa ya mama pekee kwa miezi sita ya mwanzo tangu anapozaliwa bila kumpa kitu chochote kingine chochote yakiwemo maji. Kinga nyingine ameitaja kuwa ni usafi wa mazingira na kunawa mikono kwa maji safi na sabuni husaidia kupunguza maambukizo ya magonjwa ya kuharisha kwa ujumla. Aidha, amesisitiza kuwa wazazi na walezi ni vizuri wafuate ratiba ili watoto wasipitishe umri wa kupata dozi ya chanjo ya Rotavirus kwasababu umri ukizidi ataikosa chanjo hiyo na wazazi na walezi watapewa tarehe ya kurudi tena wiki nne baada ya dozi ya kwanza.

Akielezea mategemeo ya Wizara baada ya semina hiyo kwa waandishi wa habari, Gloria amesema kuwa anategemea kuwa waandishi wa habari wataweka habari za chanjo hiyo kuwa habari kuu kwa sababu inahusu kunusuru watoto na vifo vinavyozuilika. Amesema pia anategemea kupata habari nyingi katika makala, habari, majarida na vipindi vya kutosha vya kuelimisha jamii.
=30=


No comments:

Post a Comment