Tuesday, September 18, 2012

MITIHANI YA DARASA LA SABA KUANZA KESHO


Mikoa ya Iringa na Njombe imejipanga kuhakikisha kuwa mitihani ya kumaliza elimu ya msingi kwa mwaka 2012 inafanyika katika hali nzuri na kutokuruhusu mianya yoyote ya udanganyifu na kusababisha kufutiwa kwa matokeo kwa baina ya shule za msingi.

Akifafanua maandalizi ya mitihani hiyo ofisini kwake, Afisa Elimu Mkoa wa Iringa, Mwalimu Joseph Mnyikambi aliyepewa pia jukumu la kusimamia mitihani hiyo kwa mikoa ya Iringa na Njombe amesema kuwa tayari semina zimeendeshwa na kamati ya usimamizi wa mitihani ya mkoa katika Halmashauri zote nane za mikoa ya Iringa na Njombe. Amezitaja Halmashauri hizo kuwa ni Njombe, Mufindi, Makete, Ludewa, Kilolo, Iringa, Njombe Mji na Iringa Manispaa.

Akiongelea maandalizi amesema kuwa maandalizi yote yamekamilika na leo ndiyo siku ya kuwapeleka wasimamizi katika vituo vyao ya kusimamia mitihani hiyo. Amesema “kwa mujibu wa sheria zetu huwezi kumwambia msimamizi atasimamia wapi mtihani huo”. Amesema kuwa lengo ni kuzuia udanganyifu na hongo kutoka kwa jamii kwenda kwa msimamizi na kutoka kwa msimamizi kwenda kwa jamii pamoja na wanafunzi.

Kuhusu taratibu, Mwalimu Mnyikambi amesema kuwa taratibu ni za kawaida na zilizozoeleka isipokuwa kitu kipya ni mwaka huu watahiniwa wote watatumia penseli na fomu maalumu kujibu mitihani hiyo kwa kusiliba kwa sababu kwa mara ya kwanza itatumika teknolojia mpya ya ‘optical mark reader’ (OMR). Amesema kuwa majibu yatasahihishwa kwa kutumia kompyuta.

Amesema kuwa mitihani hiyo itafanyika kwa siku mbili na itaanza kesho tarehe 19 -20 Septemb, 2012. masomo yatakayotahiniwa ameyataja kuwa ni Sayansi, Hisabati na Kiswahili. Mengine ni Kiingereza na Maarifa ya Jamii.

Ni kwa namna gani mkoa umejipanga kukabiliana na udanganyifu unaoweza kusababisha wanafunzi kufutiwa matokea, Afisa elimu mkoa wa Iringa amesema “kama mkoa tumejipanga vizuri kuhakikisha kuwa udanganyifu haufanyiki katika mikoa ya Iringa na Njombe kwa kuzingatia taratibu zote za mitihani”. Ameitaja miongoni mwa mikakati hiyo kuwa ni pamoja na kila mwanafunzi kukaa katika dawati lake na kukaa mmoja ili kuondoa uwezekano wa kutizamiana. Amesema katika semina kwa wasimamizi wa mitihani, msisitizo ulikuwa ni kuhakikisha hakuna udanganyifu wowote utakaopewa nafasi katika mtihani huo ili kuhakikisha kila mwanafunzi anayeingia kidato cha kwanza anajua kusoma na kuandika na anakwenda kwa kufaulu vizuri.

Mwalimu Mnyikambi ameitaja idadi ya wanafunzi watakaofanya mitihani hiyo ya kumaliza elimu ya msingi kwa mikoa ya Iringa na Njombe kuwa ni 43,499 kati yao wasichana ni 23,015 na wavulana ni 20,484. amesema jumla ya shule zote ni 887.
=30=

No comments:

Post a Comment