Tuesday, September 11, 2012

RC IRINGA AZINDUA KAMATI YA UTALII NA MAZINGIRA





Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma amezindua kamati ya kuendeleza Utalii na Mazingira mkoani Iringa na kuitaka ijiwekee malengo mahususi ya kuendeleza utalii katika mkoa huo na ukanda wa kusini kwa ujumla wake.

Dkt. Christine amesema kuwa lengo la kuunda kamati hiyo ni kuufanya utalii uweze kushamiri katika ukanda huo kama ulivyoshamiri katika ukanda wa kaskazini na kusisitiza kuwa mkoa wa Iringa uliteuliwa kuwa kitovu cha utalii kwa ukanda wa nyanda za juu kusini.

Ameitaka kamati hiyo iliyosheheni wataalamu mbalimbali kutoka katika sekta ya utalii, mazingira, habari na sekta mtambuka kufanya kazi kwa kujituma na kujitoa ili kufanikisha malengo ya kamati hiyo. 

Mkuu wa Mkoa ameyataja majukumu ya Kamati hiyo kuwa ni pamoja na kujadili mawazo, maoni na mbinumbalimbali za kuhamasisha na kuendeleza utalii mkoani Iringa. Kuratibu maonesho, matukio na vikao vya wadau wa utalii mkoani Iringa. Majukumu mengine ameyataja kuwa kuandaa mipango mikakati na shughuli za kuhamasisha na kuendeleza utalii mkoani Iringa pamoja na kufuatilia upatikanaji wa eneo la maonesho ya utalii. Mengine ni kufanya jitihada za kutambua vivutio vya utalii vilivyopo mkoani Iringa na kuvitangaza ndani na nje ya nchi na kusaidiana na vyombo vya usalama na usafiri kuhakikisha kuwepo kwa usalama na usafiri wa watalii wa ndani na nje ya nchi.

Katibu wa Kamati hiyo, Risala Kabongo alishauri kuwa dhana ya utalii ni vema ikajikita katika kuhusisha kilimo, maji na usalama. Amesema utalii ni sekta mtambuka hivyo unahusisha mambo sekta mbalimbali za kimaendeleo. 

Wakati huohuo, Afisa Utalii Manispaa ya Iringa, Fidelis Mrute alihusisha nafasi ya idara ya uhamiaji katika kuimarisha usalama katika sekta ya utalii. Amesema idara hiyo ni muhimu katika kubaini kati ya mtalii halisi hasa wa nje ili kutofautisha na watu wasiokuwa na nia njema na sekta ya utalii. 

Mkuu wa Mkoa wa Iringa ameteua kamati ya kuendeleza utalii na Mazingira kwa mkoa wa Iringa na kamati hiyo itahudumu kwa muda wa miaka mitatu.
=30=   



No comments:

Post a Comment