Monday, November 26, 2012

MUFINDI WAJIDHATITI KUFIKISHA PEMBEJEO VIJIJINI




Wilaya ya Mufindi imehakikisha usambazaji wa pembejeo unafanikiwa kwa kuhakikisha mbadala wa mawakala waliopungukiwa na uwezo wa kusambaza pembejeo za kukuzia baada ya kutoa taarifa kwa uongozi wa wilaya na wakala mwingine kuendeleza usambazaji huo haraka ili kutokuwachelewesha wakulima.

Hayo yamesemwa na Afisa Kilimo, Mifugo na Ushirika wa Wilaya ya Mufindi, Edna Kaduma wakati akiwasilisha taarifa ya usambazaji wa pembejeo kwa wilaya ya Mufindi mwaka 2011/2012 na 2012/2013 katika kikao cha kamati ya vocha ya mkoa kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa.

Edna amesema kuwa miongoni mwa changamoto ilikuwa ni mawakala kupungukiwa uwezo wa kusambaza pembejeo hasa wakati ilipoanza kutumika mbolea ya kukuzia. Amesema kuwa mawakala hao walitoa taarifa kwa uongozi wa Wilaya na haraka walipatikana mawakala wengine kwa lengo la kuendeleza huduma hiyo pasipo kuwachelewesha wakulima kutumia mbolea hiyo ya kukuzia. Amesema katika kuhakikisha zoezi hilo linafanikiwa, kamati ya vocha Wilaya ya Mufindi ilifanya mikutano mitatu na mawakala wote kwa lengo la kutathmini uwezo wa kila mmoja na kukubaliana maeneo ya kuhudumia kulingana na uwezo wa kila wakala aidha, wale wenye uwezo mkubwa walikubali kutoa huduma kwa maeneo yaliyokosa mawakala.   

Amesema ili kuweka uwazi katika mchakato huo, kamati ya vocha ya wilaya ilifanya mikutano ya hadhara na wananchi kwa kila kata na pamoja na kukutana na kamati za vocha za vijiji kwa ajili ya kutoa maelekezo ya utaratibu wa mpito wa usambazaji wa pembejeo kwa kutumia vocha. Amesema miongoni mwa changamoto ni kupanda kwa bei za pembejeo baadhi ya wakulima wameshindwa kutumia pembejeo bora. Amesema miongoni mwa changamoto pia ni kupungua kwa wanufaika kutokana na kupungua kwa idadi ya vocha na kuchelewa kuwa vocha za ruzuku kusababisha baadhi ya vijiji kutotumia vocha za mbegu bora.

Edna amesema kuwa ili kuhakikisha usambazaji unafika katika maeneo yote suala la mawasiliano lilipewa uzito unaostahili. Amesema mawasiliano na ufuatiliaji wa mara kwa mara ulifanyika kati ya wilaya na vijiji ili kuhakikisha maeneo yote usambazaji unakwenda vizuri na pembejeo zinauzwa kwa bei iliyokubalika katika vikao.

Akiongelea maadalizi ya pembejeo kwa msimu wa mwaka 2012/2013, Afisa Kilimo, Mifugo na Ushirika wilaya ya Mufindi amesema kuwa mahitaji ya mbolea kwa wilaya ya Mufindi, jumla ya tani 13,720 na mahitaji ya mbegu ni jumla ya tani 887. Amesema “msimu huu wilaya imepokea mgao wa vocha seti 22,188 ikiwa ni pungufu kwa asilimia 50 ikilinganishwa na mgao wa msimu uliopita.
=30= 

No comments:

Post a Comment