Monday, August 26, 2013

KUPUNGUA KWA UPENDO CHANZO CHA KUVUNJIKA AMANI




Kupungua kwa upendo baina ya wananchi ni chanzo cha kuvunjika kwa amani nchini kutokana na watu kukosa hofu ya Mungu.

              Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma


Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma alipokuwa akifungua mkutano wa kuzungumzia mchango wa uislam katika kuleta amani Duniani ulioandaliwa na Jumuiya ya waislamu wa Ahmadiyya Tanzania uliofanyika katika ukumbi wa Siasa ni Kilimo, mjini Iringa.

Dkt. Christine amesema kuwa uvunjifu wa amani nchini unatokana na kupungua kwa upendo baina ya wananchi. Amesema kuwa watu wanapungukiwa upendo kwa sababu wanakosa hofu ya Mungu. Amesema “natumaini kuwa wote tu mashaidi kuwa katika siku za hivi karibuni tumeshuhudia au kusikia matukio yasiyo ya kawaida ya ukiukaji na uvunjifu wa amani nchini katika maeneo mbalimbali. Tumuombe Mwenyezi Mungu, apishe mbali, tuweze kudumisha amani na utulivu kwa kila mmoja”. 

Amesmea “matukio haya ni dalili mbaya kwa nchi yetu ambayo waasisi wetu walitujengea misingi mizuri ya umoja, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa. Kutonaka na misingi hiyo ndiyo maana watanzania hatuna ubaguzi katika misingi ya udini na ukabila. Misingi hii ni mizuri na hatunabudi kuidumisha muda wote”. 

Aidha, Mkuu wa Mkoa amewataka wananchi kuhakikisha wanadumisha misingi ya amani iliyowekwa na waasisi wa Taifa kuanzia kwa Baba wa Taifa Mwl. Julius Nyerere. “Nawaomba sana ndugu zangu wa Mkoa wa Iringa, kwa umoja wetu tuhakikishe tunasimamia na kudumisha misingi hiyo ili kizazi cha sasa na kijacho kiweze kufurahia amani hii tuliyonayo. Tusikubali kuyumbishwa na kuacha amani na utulivu ipotee” alisisitiza Dkt. Christine.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa amewataka viongozi wote kutikomeza vitendo vinavyopelekea uvunjifu wa amani katika mkoa wa Iringa na Taifa kwa ujumla. Amesema “ni wajibu wetu viongozi wa serikali na dini kuhakikisha tunatokomeza kabisa vitendo vyote vinavyopelekea uvunjifu wa amani katika mkoa wetu wa Iringa na nchi yetu kwa ujumla” Mkuu wa Mkoa wa Iringa.  

Akiongelea mchango wa uislamu katika kuleta amani duniani, Amir na mbashiri mkuu wa Jumuiya ya waislamu waahmadiyya Tanznaia, Sheikh Tahir Mahmood Chaudhry amesema kuwa uislamu maana yake ni amani na utii hivyo ni kitu cha ajabu kuitumia dini kufundisha kinyume na amani. Amesema kwa msingi huo, mwanadamu anatakiwa aishi kwa amani na muumba wake, nafsi yake, wanadamu wenzake na viumbe wengine. Amesmea kuwa muislamu wa kweli siku zote anakuwa ni mtu mnyenyekevu, mpole, mwenye huruma na anayejali haki za kila mtu na kila kitu.  

Sheikh Chaudhry amesema kuwa katika kusisitiza amani, uislamu unafundisha udugu wa wanadamu wote na kuhimiza uadilifu uliokamilika hata mbele ya maadui na kufundisha uhuru kamili wa kuabudu. 

Akiongelea sababu za kuvunjika kwa amani, amezitaja sababu hizo kuwa ni sababu za kiuchumi, kijamii, kisiana na kidini. Amesema kuwa miongoni mwa sababu hizo zote sababu za kidini ndizo zinazopelekea uvunjifu mkubwa wa amani pamoja na kuwa zimeungana na sababu nyingine.
=30=

No comments:

Post a Comment