Saturday, February 28, 2015

MKOA WA IRINGA WAPIGA HATUA UJENZI WA MAABARA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Uongozi wa Mkoa wa Iringa umepongezwa kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika sekta ya elimu kwa kuongeza kiwango cha ufaulu.
Pongezi hizo zimetolewa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mizengo Pinda alipokuwa akifanya majumuisho ya ziara yake ya Mkoa wa Iringa yaliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi.
Mhe. Pinda amesema “napongeza uongozi wa Mkoa na Wilaya zote kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika sekta ya elimu.” Amesema Mkoa umefanya vizuri katika elimu ya msingi na sekondari kwa kuongeza ufaulu wa wanafunzi. Amesema kuwa kwa mujibu wa taarifa ya Mkoa kuhusu sekta ya elimu, ufaulu wa mtihani wa darasa la saba mwaka 2014 ulikuwa asilimia 68.5 na ufaulu wa kidato cha nne ulikuwa asilimia 65.2.
Akiongelea ufaulu wa kidato cha sita mwaka 2013, Waziri Mkuu amesema kuwa Mkoa ulifanya vizuri na katika matokeo ya kidato hicho, asilimia 99 ya watahiniwa wote walifaulu. Amesema katika matokeo hayo, shule ya sekondari Igowole ambayo ni shule ya Kata Wilayani Mufindi iliongoza kitaifa. Aidha, shule ya sekondari Kawawa pia katika Wilaya ya Mufindi ilikuwa katika 10 bora kitaifa. Kutokana na mafanikio hayo mazuri, ameutaka uongozi wa Mkoa kutokurudi nyuma.
Akiongelea agizo la Mhe. Rais la ujenzi wa Maabara za Sayansi, Mhe. Pinda amewatia moyo viongozi wa Mkoa wa Iringa ili waendelee na jitihada ya kukamilisha agizo hilo la Mhe. Rais katika kipindi kilichoongezwa hadi kufikia mwezi Juni, 2015. Aidha, amewataka Wakuu wa Mikoa nchini kufuatilia ujenzi wa Maabara hizo za Sayansi nchini. Amesema “wito wangu ni kwa Wakuu wa Mikoa nchini kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa ujenzi wa Maabara hizo za Sayansi ili Wilaya ziweze kufikia malengo yao kabla ya mwezi Juni 2015.”
Wakati huohuo, amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri nchini kujenga Maabara mpya na za kisasa zinazoendana na mazingira ya sasa. Amekosoa hatua ya baadhi ya Halmashauri kukarabati Maabara za zamani zenye majengo yaliyochakaa na kuwakumbusha kuwa lengo la serikali ni kujenga Maabara mpya za kisasa zitakazodumu.  
Mkoa wa Iringa umefikia asilimia 34 ya ujenzi wa Maabara ambayo ni sawa na Maabara 108 kati ya mahitaji ya Maabara 318. Maabara 210 zipo katika hatua mbalimbali za umaliziaji.
=30=

No comments:

Post a Comment