Tuesday, October 20, 2015

DC IRINGA SIMAMIA ULINZI NA USALAMA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Mkuu wa wilaya ya Iringa Richard Kasesela ametakiwa kusimamia ulinzi na usalama katika wilaya ya Iringa ili mkoa uwe salama katika kipindi cha kampeni kuelekea uchaguzi mkuu.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza muda mfupi baada ya kumuapisha mkuu wa wilaya mteule wa Iringa katika ofisi ya mkuu wa mkoa leo.
 
Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Iringa Amina Masenza
Masenza alisema “suala la ulinzi na usalama ni muhimu sana katika wilaya ya Iringa ili mkoa uwe salama. Hivyo, lazima ulisimamie ipasavyo. Binafsi nina imani na wewe na utendaji wako wa kazi hivyo hautashindwa katika kutekeleza majukumu yako”. Alisema kuwa wilaya ya Iringa ikiwa salama wananchi wataendelea kushiriki katika mampeni za kisiasa kwa uhuru na amani na hatimae kupiga kura salama.

Mkuu wa mkoa alimtaarifu masuala ya kipaumbele kwa mkoa wa Iringa kuwa ni lishe, ukimwi na usafi wa mazingira. Alimtaarifu kuwa katika ratiba yake ya kazi lazima ijikite katika utekelezaji wa mpango mkakati wa mkoa unaolenga kukabiliana na changamoto za lishe, hali ya maambukizi ya ukimwi na usafi wa mazingira.

Katika salamu za mkuu wa wilaya ya Iringa mteule Richard Kasesela alimshukuru Rais wa Jamhuri kwa imani aliyonayo kwake. Aidha, alisema kuwa katika kipindi hiki suala la amani ni agenda yake ya mwanzo kuelekea uchaguzi mkuu wa tarehe 25 Oktoba, 2015. Alisema kuwa yeyote katika wilaya ya Iringa atakayetishia watu kwenda kupiga kura hasa wanawake atashughulikiwa. Alisema kuwa lazima wananchi wote katika wilaya ya Iringa washiriki katika zoezi la kupiga kura kikamilifu pasipo woga ili wafurahie haki yao ya kupiga kura kikatiba.

Akiongelea masuala ya kimkakati katika mkoa, mkuu wa wilaya mteule alisema “nitajitahidi kuhakikisha suala la lishe bora kwa wananchi hasa wanawake wajawazito na watoto wachanga linaboreka katika wilaya ya Iringa na mkoa kwa ujumla. Tatizo hili lazima liishe”.
 
Mkuu wa wilaya ya Iringa, Mhe. Richard Kasesela
Aidha, suala la ukimwi aliahidi kukabiliana nalo ipasavyo. Alisema kuwa ngono zembe ni jambo linalohitaji kuangaliwa kwa umakini zaidi. Wilaya itaangalia upya viashiria vya ukimwi na mitego ili kuangalia jinsi ya kuitegua mitego hiyo hatimae kupunguza maambukizi mapya. Akiongelea usafi wa mazingira alisema “mtu ni afya hivyo usafi wa mazingira ni afya pia. Lazima usafi wa mazingira uanzie kwa mtu mwenyewe katika mazingira ya nyumbani kwake na mazingira yanayomzunguka”.

Mkuu wa wilaya ya Iringa aliapishwa leo mjini Iringa kufuatia uteuzi wa Rais wa wakuu wapya wa wilaya 13 na kuhamishwa kwa wakuu saba wa wilaya tarehe 4/10/2015.
=30=

No comments:

Post a Comment