Thursday, January 18, 2018

IRINGA WATAKIWA KUTUMIA FURSA YA KULIMA ZAO LA KOROSHO



Na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Wananchi wilayani Iringa wametakiwa kuitumia vizuri fursa ya kilimo cha zao la korosho ili kuweza kujiongezea kipato.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipokuwa akizindua kilimo cha zao la korosho katika kijiji cha Idodi wilayani Iringa jana.

Masenza aliwataka wananchi kutumia kilimo cha zao la korosho kama fursa ya kuondokana na umasikini. 

“Kuanzishwa kwa zao hili wilayani Iringa ni fursa kubwa itakayousaidia Mkoa na watu wake kupambana na umasikini na kuongeza mapato yake.” Alisema Masenza.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa aliwataka maafisa ugani na viongozi wa vijiji, kata na tarafa zinazolima zao hilo kutimiza wajibu wao ili kukifanya kilimo cha zao hicho kiwe chenye tija. 

Tunataka Mkoa ufanikiwe katika kilimo cha zao hili na ushauri wangu itungwe sheria ndogo itakayomlazimisha kila mkulima kushiriki katika kilimo hiki kinachotarajiwa pia kuchochea uanzishwaji wa viwanda vya kubangua korosho,” alisema mkuu wa Mkoa. 

Aidha, aliwataka viongozi wa vijiji kuwa mfano waa kuigwa katika kilimo cha korosho na uhamasishaji wake ili wananchi waweze kujifunza kupitia mashamba hayo.

Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Richard Kasesela alisema kuwa kilimo cha korosho kitampatia mwananchi matokeo ya uhakika kwa sababu bei yake ni nzuri. Alisema kuwa kwa taarifa za karibuni kilo moja ya korosho zilizobanguliwa inauzwa hadi shilingi 4,000.
=30=

No comments:

Post a Comment