Wednesday, May 6, 2015

SHULE ZA IGOWOLE NA KAWAWA ZAPONGEZWA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Shule za sekondari za Igowole na Kawawa zimepongezwa kwa kufanya vizuri katika mitihani ya kidato cha sita mwaka 2014 na kuung’arisha mkoa wa Iringa kitaifa.

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya mitihani wa Mkoa wa Iringa, bibi. Wamoja Ayubu alipokuwa akiongea na waandishi wa habari kuhusu mitihani inayoendelea ya kidato cha sita nchini ofisini kwake.

Wamoja amesema “nichukue nafasi hii kipekee kuzipongeza shule za sekondari za Igowole na Kawawa zote zipo katika halmashauri ya wilaya ya Mufindi kwa kufanya vizuri katika mitihani ya kidato cha sita mwaka 2014, ambapo Igowole iliahika nafasi ya kwanza kitaifa na Kawawa ilishika nafasi ya kumi. Hongereni sana kwa matokeo hayo yaliyoufanya mkoa wetu kung’ara.” “Aidha, nichukue nafasi hii pia kuzipongeza shule zote za mkoa wa Iringa kwa kuwa kwa ujumla wake zilifanya vizuri katika matokeo hayo kati ya shule 22 zilizokuwa na watahiniwa wa kidato cha sita mwaka 2014 shule 18 zilifaulisha kwa asilimia 100 kwa maana hakukuwa na mwanafunzi aliyepata daraja la 0”, aliongeza bibi. Wamoja.

Akiongelea mitihani inayoendelea ya kidato cha sita, Mwenyekiti wa Kamati ya Mitihani wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa mkoa unavyo vituo 23 vya mtihani wa kidato cha sita vyenye jumla watahiniwa 2,162. Amesema kuwa vituo hivyo vitasimamiwa na wasimamizi 73 kati yao wasimamizi wakuu 23 na wasimamizi wasaidizi kutoka nje wapatao 50. 

Kwa mitihani ya ualimu, amesema vipo vituo 4 vyenye jumla ya watahiniwa 324 kati yao 122 ni ngazi ya Cheti na 202 ngazi ya Diploma. Ameongeza kuwa vituo hivyo vitasimamiwa na wasimamizi wakuu wanne na wasimamizi wasaidizi saba kutoka nje.
Mwenyekiti huyo ambaye pia ni Katibu Tawala Mkoa wa Iringa amewataka wasimamizi kutokuwa na tamaa ya fedha itakayowasababishia kujiingiza katika vitendo vya uvujishaji mitihani. Aidha, amewataka kuzingatia ratiba zilizotolewa ili kila mtihani ufanyike kwa wakati uliopangwa na kuwepo katika chumba cha mtihani kipindi chote ili kutotoa mwanya kwa watahiniwa kutazamiana.

Wakati huohuo Mkuu wa Mkoa wa Iringa, bibi. Amina Masenza amewatakia heri watahiniwa wote wa mitihani ya kidato cha sita mkoani Iringa na kuwataka kutokuwa na hofu na kufanya mitihani hiyo kwa kujiamini kwa kuzingatia yale yote waliyojifunza.

Mitihani wa kumaliza kidato cha sita na ualimu imeanza tarehe 04 Mei na itaendelea hadi tarehe 27 nchini kote.
=30=

Friday, May 1, 2015

HONGERA WAFANYAKAZI WOTE NCHINI


MTANDAO WA MAKTABA YA HABARI UNAWAPONGEZA WAFANYAKAZI WOTE KATIKA SIKUKUU YA WAFANYAKAZI DUNIANI.

MTANDAO HUU UNAENDELEA KUWATAKIA HERI WAFANYAKAZI WOTE KWA KIPINDI CHOTE KINACHOENDELEA ILI WAWEZE KUJILETEA MAENDELEO.

MTANDAO HUU UNAAMINI KUWA UWAJIBIKAJI NA NIDHAMU NI MSINGI WA MAENDELEO YA KIUCHUMI NA KIMKAKATI KWA KILA MFANYAKAZI

Thursday, March 26, 2015

MYUYU AWATAKA WATENDAJI WA KATA KUOMARISHA MAWASILIANO IRINGA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Uimarishaji wa mawasiliano baina ya watendaji wa kata na maafisa tarafa umeelezwa kuwa ni nyenzo muhimu katika utekelezaji wa kazi za serikali.

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Menejimenti ya Serikali za Mitaa, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Bw. Wilfred Myuyu alipokuwa akiwasilisha mada kuhusu majukumu ya watendaji wa kata katika usimamizi wa shughuli mbalimbali za maendeleo wilayani Kilolo.

Bw. Myuyu amesema kuwa katika kutekeleza majukumu, mtendaji wa kata anatakiwa kuwasiliana mara kwa mara na afisa tarafa. Amesema kuwa kwa mujibu wa miongozo ya mawasiliano serikalini, afisa tarafa anajukumu la kusimamia watendaji wa kata ili watekeleze majukumu yao ipasavyo. Amesema kuwa kwa mujibu wa sheria ya Tawala za Mikoa Na. 19 ya mwaka 1997 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2006 inaweka wazi kuwa majukumu ya afisa tafara ni kusimamia shughuli za watendaji wa kata, vijiji na mitaa katika eneo lake.

Akiongelea majukumu ya watendaji wa kata katika ujenzi wa maabara unaoendelea, Bw. Myuyu amesema kuwa watendaji wa kata wanawajibu wa kuwatambua wadau mbalimbali wa maendeleo wanaoweza kuchangia na kuwahamasisha kwenye shughuli za ujenzi wa maabara ikiwa ni pamoja na wananchi. Ameongeza kuwa wanalo jukumu la kufanya ufuatiliaji na tathmini ya ujenzi unaoendelea ili kujiridhisha na uzingatiwaji wa viwango kusudiwa pamoja na kasi ya ujenzi. Amesema kuwa katika ufuatiliaji huo wanalojukumu la kufahamu changamoto zilizopo kushauri na kuzipatia ufumbuzi.

Jukumu linguine amelitaja kuwa ni kuhakikisha michango inayotolewa na wananchi na wadau inatumika kwa kuzingatia taratibu zinazoongoza matumizi ya fedha za umma na kutoa taarifa ya matumizi ya fedha hizo kwa wananchi.    

Bw. Myuyu ameongeza kuwa jukumu lingine ni kutoa taarifa za maendeleo ya ujenzi wa maabara juu ya hatua za utekelezaji zilizofikiwa, changamoto zilizopo na hatua za utatuzi wa changamoto.
=30=

MAJI MBEYA KUTOA LITA ZA UJAZO 51,000



Na. Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Jiji la Mbeya
Mamlaka ya Majisafi na usafi wa mazingira Jiji la Mbeya ina uwezo wa kutoa maji lita za ujazo 51,000 kupitia vyanzo vyake 13 vya maji.

Katika risala ya wafanyakazi wa Mamlaka ya Majisafi na usafi wa mazingira Jiji la Mbeya iliyosomwa kwa mgeni rasmi na Fundi Mkuu, Kanda namba 1 Amiri Abdallah Sapi Mkwawa amesema kuwa mahitaji halisi ya maji katika Jiji la Mbeya ni mita za ujazo 38,000 kwa siku. Amesema kuwa mahitaji hayo hupanda wakati wa kiangazi kufikia mita za ujazo 43,000 kwa siku katika miezi ya Septemba hadi Novemba. Amesema kuwa Mamlaka ina jumla ya vyanzo 13 vya maji vyenye uwezo wa kutoa mita za ujazo 49,000-51,000 kwa siku. Amevitaja vyanzo hivyo kuwa ni Ivumwe I na Ivumwe II, Nzovwe, Imeta, Sisimba, Hanzya, Mfwizimo. Vyanzo vingine ni Nsalaga, Lunji, Mwatezi, Mkwanana, Iduda na Halewa. Amesema kuwa baadhi ya vyanzo vinapungukiwa maji wakati wa kiangazi kutokana na ukame na shughuli za kibinadamu kama uchomaji wa moto, kilimo na ukataji wa miti kwa ajili ya kuni na mkaa.

Mkwawa amesema kuwa katika kuhakikisha rasilimali maji inaendelea kuwepo, Mamlaka kwa kushirikiana na wadau imeendelea na jitihada za kuhakikisha kuwa vyanzo vya maji vinahifadhiwa. Amesema kuwa Mamlaka yake inahakikisha kuwa miundombinu ya majisafi na majitaka iliyopo inatunzwa. “Ili kulipa uzito suala hili Mamlaka kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo Jeshi la Polisi, Jeshi la kujenga Taifa, JWTZ, Wakala wa Misitu Tanzania (TFS), Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) imeunda kamati ya mazingira kwa lengo la kuhifadhi vyanzo vya maji vilivyomo kwenye safu za mlima Mbeya ambapo leo hii utaikabidhi kamati sehemu ya vitendea kazi” Mkwawa. 

Mkuu, Kanda namba 1 amesema kuwa Mamlaka imeweza kuzalisha majisafi na salama na kuyasambaza kwa asilimia 96 ya wakazi wa Jiji la Mbeya. Amesema katika kuboresha miundombinu ya majisafi na majitaka katika Jiji la Mbeya fedha za ndani na fedha za wafadhili zimeendelea kutumika. Mradi wa awamu ya pili na mradi wa kupeleka maji uwanja wa Ndege wa Songwe ni miongoni mwa maboresho yaliyofanyika. 

Amesema katika kukabiliana na uharibifu wa miundombinu dira za maji, Mamlaka imeendelea kuwabaini na kuwachukulia hatua za kisheria baadhi ya wezi wa maji. Hatua nyingine ni kuhifadhi vyanzo vya maji kwa kushirikiana na wadau mbalimbali. 

Akiongelea changamoto zinazoikabili Mamlaka ya Maji, Mkwawa amezitaja kuwa ni baadhi ya wateja hasa taasisi za umma kutokulipa ankara za maji kwa wakati au kutokulipa kabisa. Changamoto nyingine ni baadhi ya vyanzo vya maji vimeendelea kupungukiwa na maji, kutokana na uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabia nchi akitolea mfano chanzo cha mto Lunji na Mfwizimo na Iduda.

Friday, March 20, 2015

KILELE CHA MAADHIMISHO YA WIKI YA MAJI JIJINI MBEYA



Mamlaka ya Majisafi na usafi wa mazingira jiji la mbeya itaadhimisha kilelel cha wiki ya maji mwaka 2015 katika viwanja vya Ofisi za Mamlaka ya Maji. 

Kilele hicho kilitanguliwa na Uzinduzi wa wiki ya Maji uliofanyika kuanzia tarehe 16 Machi, 2015 kwa kufanya kazi za usafi wa mazingira katika eneo la ofisi na kwenye vituo vyote vya kutolea huduma. Aidha, shughuli nyingine ni kuhamasisha wananchi juu ya ulipaji wa ankara za maji kwa wakati.

Kazi nyingine zilizofanywa katika wiki hiyo ni pamoja na kutembelea taasisi pamoja na shule kuhamasisha taasisi kujiunga na mtandao wa majitaka na kupanda miti eneo la Ivumwe.

Katika kilelel cha Maadhimisho hayo mada ya Usafi wa Mazingira na Utunzaji wa vyanzo vya Maji itatolewa.
Michezo na burudani mbalimbali vitaanikiza ikiwa ni pamoja na mchezo wa kuvuta kamba na ngoma.

Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Mbeya. Maadhimisho ya wiki ya maji yanaongozwa na Kaulimbiu isemayo:

Maji kwa Maendeleo endelevu.

=30=

Tuesday, March 17, 2015

UTUNZAJI MAZINGIRA NI MUHIMU KUENDELEZA RASILIMALI MAJI



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Tabia ya utunzaji wa mazingira imeelezwa kuwa ni muhimu katika kuendeleza rasilimali maji mkoani Iringa.

Kauli hiyo imetolewa na Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Bw. Adam Swai katika hotuba yake ya uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya maji katika mkoa wa Iringa yaliyofanyika katika Kata ya Ruaha, Manispaa ya Iringa. 
Bw. Swai amesema “utunzaji wa mazingira ni kitu muhimu katika kuhakikisha uendelevu wa rasilimali maji. Sote tunafahamu kuwa rasilimali maji ni muhimu kwa maisha na maendeleo ya binadamu zikiwepo shughuli za kiuchumi. Bila maji hakuna maendeleo na bila maendeleo hakuna maji,”. 

Akiongelea kusuasua kwa ujenzi wa miradi ya maji, Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Iringa amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri kusimamia kikamilifu ujenzi wa miradi ya maji. Aidha, amewataka kuwapatia kazi makandarasi na wataalamu washauri wenye uwezo na sifa za kufanya kazi zenye ubora. Amewataka kujiridhisha na uwezo wa makandarasi kabla ya kuwapatika kazi juu ya ubora wa utendaji kazi wao ili miradi ikamilike kwa wakati.

Akiongelea juhudi za kuongeza upatikanaji huduma ya maji mijini na vijijini, ameshauri kutumia teknolojia ya uvunaji wa maji ya mvua. Ameongeza utumiaji wa teknolojia ya nguvu ya jua na nguvu ya upepo katika kusukuma maji katika ngazi ya kaya na taasisi kutokana na urahisi wa teknolojia hizo.

Akiongelea hali ya upatikanaji huduma ya maji mkoani Iringa, Mhandisi wa Maji Mkoa wa Iringa, Mhandisi Shaban Jellan amesema kuwa hadi kufikia Disemba, 2014, idadi ya watu waliokuwa wakipata huduma ya maji ndani ya umbali usiozidi mita 400 toka kwenye makazi yao ni 651,917 sawa na 69.3% ya wakazi wote wa Mkoa wa Iringa.

Akiongelea huduma ya maji vijijini, amesema kuwa wakazi wa vijijini wanaopata huduma ya maji ni 452,524 sawa na 66.1% ya wakazi wote waishio vijijini. Ameitaja idadi ya wanaopata huduma ya maji kwa kila Halmashauri kuwa ni 90% sawa na wananchi 14,213 katika Halmashauri ya Manispaa (vijijini-peri-urban), 69% sawa na wananchi 175,282 katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo ni 60.8% sawa na wananchi 93,722 na Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi 64.8 sawa na wananchi 172,258 wanaopata huduma ya maji. 

Maadhimisho ya wiki ya maji mwaka huu yanaongozwa na kauli mbiu isemayo maji na maendeleo endelevu.
=30=

Saturday, March 14, 2015

WIKI YA MAJI TAREHE 16-22 MACHI, 2015

WIKI IJAYO KUANZIA TAREHE 16-22 MACHI NI WIKI YA MAJI.
JIANDAE KUSOMA MAFANIKIO YALIYOPATIKANA KATIKA SEKTA YA MAJI NCHINI KATIKA MTANDAO WAKO UUPENDAO

Saturday, February 28, 2015

DC MBONI AAPISHWA RASMI



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa IRINGA
Ushirikishaji wananchi na makundi mengine katika jamii ni njia rahisi ya kuleta tija katika utekelezaji wa Ilani ya CCM na miradi ya maendeleo mkoani Iringa.
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza muda mfupi baada ya kumuapisha Mkuu mpya wa Wilaya ya Mufindi, Mboni Mhita katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa. 
Mhe. Mboni Mhita (kulia) walio kaa na Mhe. Amina Masenza (kushoto). Waliosimama ni Maafisa waandamizi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa
 Masenza amesema kuwa katika kutekeleza Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010 na miradi yote ya maendeleo katika Wilaya na Mkoa dhana ya ushirikishaji wananchi na wadau wengine ni muhimu sana katika kuleta tija ya kazi. Amesema wananchi na makundi mengine yanaposhirikishwa uelewa wa pamoja unakuwepo na kufanya utekelezaji wake kuwa ni jukumu la jamii nzima. Amesema kuwa mara nyingi mtafaruku na wananchi unatokea pale ambapo ushirikishwaji unakuwa mdogo au hakuna kabisa.
Mkuu wa Mkoa amemtaka Mkuu huyo wa Wilaya kusoma kwa umakini nakala ya wajibu wa Mkuu wa Wilaya na kuuelewa kwa sababu ndiyo muongozo katika utendaji kazi wa Mkuu wa Wilaya. Amesema kuwa hakuna jambo lisilowezekana na kumtaka kutumia vizuri vyombo vya usalama na wataalamu waliopo katika Wilaya ya Mufindi. Aidha, amemtaka kufanya kazi bega kwa bega na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Mufindi ili kazi yake iwe nyepesi. Amesema kuwa Kamati hiyo inawajibu wa kumshauri na kumsaidia katika kutekeleza majukumu katika Wilaya ya Mufindi.
 Mkuu wa Mkoa amesema kuwa wananchi wote wanamatumaini na Wakuu wa Wilaya katika kutatua matatizo yao. “Wewe ni lulu, wananchi wote wataangaika sehemu zote watakazokwenda lakini wakifika kwako watasema hapa tumefika na hapa ndiyo mwisho. Unamwambia mwananchi nenda mahakamani hataki, nenda polisi hataki nenda kwa Mkurugenzi hataki anajua wewe ndiye utaweza kumsimamia na wewe peke yako ndiye unaweza.” Alisisitiza Masenza.
Amesema kuwa wananchi wengi wanamatumaini sana na Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa kwa sababu wanamajibu ya papo kwa papo kwa matatizo ya wananchi kwa vile vyombo walivyonavyo vinawafanya kuwa na majibu.
Akitoa shukrani zake, Mkuu wa Wilaya ya Mufindi, Mboni Mhita amemshukuru Mhe. Rais kwa imani aliyonayo kwake na kumteua katika nafasi hiyo. Aidha, ameomba ushirikiano na ushauri kadri inavyowezekana ili kazi yake iwe rahisi. Amemshukuru Mkuu wa Mkoa kwa kumpatia nasaha na vitendea kazi. “Mbali na vitabu ambavyo umenipa vya Ilani pamoja na Katiba, maneno yako yamekuwa na uzito sana naomba nikuahidi kwamba nitayazingatia na pindi nitakapoona kwamba nimekwama au nahitaji ushauri basi sitasita kuja kwako kuomba ushauri.” Alisisitiza Mboni.
Tukio hilo la kuapishwa kwa Mkuu wa Wilaya ya Mufindi limeshuhudiwa na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, familia ya Mboni, watumishi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Wilaya ya Mufindi, waandishi wa habari na wananchi kwa ujumla.
=30=