Wednesday, August 3, 2016

NTINIKA ATAKA ACB KUJITANGAZA



Na Mwandishi Maalum Mbeya 

Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Paul Ntinika ameitaka benki ya kibiashara ya Akiba (Akiba Commercial Bank) kujitangaza zaidi katika vyombo vya habari ili iweze kufahamika zaidi kwa wananchi.

Ushauri huyo aliutoa alipotembelea benki hiyo katika viwanja vya John Mwakangale katika maonesho ya Nanenane jijini Mbeya.

Ntinika alisema kuwa ili benki hiyo na huduma zake ziweze kufahamika zaidi kwa wananchi lazima benki hiyo itengeneze mkakati wa kujitangaza kwa wananchi kupitia vyombo vya habari. “Pamoja na huduma nzuri mnazozitoa lakini kama hamjitangazi si rahisi kwa wananchi kuwafahamu na kufahamu huduma zenu. Tumieni fursa hii ya maonesho ya kilimo Nanenane kujitanga zaidi na hasa kutangaza mipango yenu ya kumnufaisha mkulima pamoja na mambo mengine” alisema Ntinika.

Ntinika ambaye pia ni mtaalam mbobezi katika masuala ya fedha na ukaguzi wa mahesabu, alisema kuwa wananchi wengi hawana uelewa wa masuala ya kibenki hivyo kukosa huduma na fursa nyingi zinazopatikana kupitia taasisi za kifedha. Aliitaka benki hiyo kupanua wigo wake wa huduma ili kuwanufaisha wananchi wengi wa wilaya ya Mbeya.

Nae Afisa mikopo wa benki ya kibiashara ya Akiba, Anthony Kunambi alisema kuwa benki yake inalenga wajasiliamali wadogo na wa kati kwa kuwapa elimu ya ujasiliamali ili waweze kufanya kazi zao kwa tija na faida zaidi. Alisema kuwa miongoni mwa huduma wanazotoa ni pamoja na akaunti za amana, hundi, akaunti maalumu ya wafanyabiashara na huduma za kuwaleta karibu Vicoba na taasisi za kifedha na kuwaelimisha umuhimu wa Vicoba kutumia huduma za kibenki badala ya mfumo wa awali wa kujiwekea akiba majumbani.

Akiongelea jinsi benki yake inavyojishughulisha na kilimo, Kunambi alisema kuwa benki hiyo imekuwa ikitoa huduma ya mikopo kwa wakulima na wafugaji. 

Kwa mkoa wa Mbeya tumekuwa tukitoa mikopo kwa wafugaji wanaofuga kisasa lakini katika mkoa wa Arusha tumekuwa tukifanya kazi na wafugaji wanaofuga kizamani. Katika mkoa wa Arusha tumekuwa tukifadhili mradi wa kunenepesha ng’ombe na wanyama wamekuwa wakikatiwa bima ili kumhakikishia mfugaji uhakika kwa mifugo yake endapo janga litatokea”.

Sabina Stanley ambaye ni msimamizi wa mikopo wa benki hiyo tawi la Mbeya, alisema kuwa benki hiyo imaendelea na mradi wa majaribio katika sekta ya kilimo kwa kuanza na miradi michache katika mikoa ya Mbeya, Arusha na Dodoma. Alisema kuwa benki yake ilitoa mikopo kwa wakulima wa Litenga zaidi ya shilingi bilioni moja kwa vikundi 39 vya wakulima mwaka 2015. Nyingine ni mashine ya kukaushia kahawa yenye thamani ya dola za mimarekani 200 na kampuni ya Rogimwa iliyokopeshwa milioni 200.

Benki ya kibiashara ya Akiba (ACB) ina jumla ya matawi 18 kati ya matawi hayo, 13 yapo mkoani Dar es Salaam, wakati mikoa ya Mbeya, Mwanza, Arusha, Kilimanjaro na Dodoma ikiwa na tawi mojamoja.
=30=


WATEJA WA MAMLAKA YA MAJI MBEYA MJINI WATAKIWA KUWA WALINZI WA MIUNDOMBINU YA MAJI MBEYA



Na Mwandishi Maalum Mbeya

Wateja wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira mjini Mbeya wametakiwa kuwa walinzi wa miundombinu ya maji ili idumu na kuwanufaisha kwa muda mrefu zaidi.

Kauli hiyo ilitolewa na Afisa huduma kwa wateja wa Mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira mjini Mbeya, Hilda Nzary alipokuwa akielezea umuhimu wa mkataba wa huduma kwa mteja wa mamlaka hiyo katika viwanja vya Nanenane jijini Mbeya.
Afisa Huduma kwa Wateja, Hilda Nzary

Nzary alisema “kwa mujibu wa mkataba wa huduma kwa mteja, wajibu wa mteja ni kuzuia wizi, uharibifu mchepusho wa mita na vitendo vya rushwa ikiwa watumishi wa mamlaka wameomba”

Aliongeza kuwa mteja anawajibu wa kutoa taarifa kwa uongozi wa mamlaka juu ya vitendo vyovyote vinavyohatarisha usafi na usalama wa maji ili huduma hiyo iendelee kuwa salama kwa jamii nzima na kuwa endelevu. Mteja pia anawajibu wa kulipia huduma ya majisafi na majitaka na kutunza dira ya maji inayopima wingi wa maji yanayotumika.

Afisa huduma kwa wateja alisema kuwa, kwa wateja kutimiza wajibu huo, watarajie huduma bora ya uhakika na yenye ufanisi wa hali ya juu katika muda mfupi na kurejeshewa huduma ya maji katika muda usiozidi saa 24 baada ya kulipia ankara yake yote. Aliongeza kuwa mteja anayo haki ya kutoa taarifa kwa maandishi iwapo haridhiki na huduma anazopata.

Akiongelea ubora wa huduma zitolewazo na mamlaka hiyo, alisema kuwa mamlaka hiyo itahakikisha inaendelea kuimarisha viwango vya ubora wa huduma zinazotolewa kwa kupitia hali ya utendaji kila baada ya miezi mitatu. Mamlaka imeweka mtandao wa kukusanya habari kutoka kwa wateja wa ndani na wateja wa nje ili iweze kupata taarifa sahihi zitakazoisaidia kufanya maamuzi sahihi ya kuboresha huduma kwa wateja.

Mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira mjini Mbeya ilianzishwa mwaka 1998 kwa Sheria namba 8 ya Maji, ya mwaka 1997 kifungu 3(1) ikiwa inahudumia wateja 48,000.
=30=

MATUKIO KATIKA PICHA YA SHUGHULI ZA MAMLAKA YA MAJI MJINI MBEYA KWENYE MAONESHO YA NANENANE 2016


















Tuesday, July 26, 2016

IRINGA KUWAENZI MASHUJAA KWA KUFANYA KAZI



  Na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Wakazi wa Mkoa wa Iringa wametakiwa kuwaenzi mashujaa waliopigana vita vya ukombozi kwa kufanya kazi kwa juhudi na maarifa kwa lengo la kujiondolea umasikini na kujiletea maendeleo.

Kauli hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipokuwa akitoa salamu za Mkoa katika maadhimisho ya siku ya mashujaa katika mkoa wa Iringa iliyofanyika katika uwanja wa mashujaa Manispaa ya Iringa.
Masenza alisema “leo tunaenzi kumbukumbu ya mashujaa wa nchi yetu, ambao walipigana vita kutetea uhuru na heshima ya nchi yetu na ulinzi wa mipaka yetu. Katika kuwaenzi mashujaa wetu wananchi wanatakiwa kufanya kazi kwa juhudi na maarifa katika kujiondolea umasikini”. Aliongeza kuwa mashujaa wa nchi hii walipigania ukombozi wa nchi kwa lengo la kuwaletea wananchi maendeleo.

Masenza ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Iringa aliwataka wananchi kudumisha umoja na mshikamano mkoani hapa akielezea kuwa umoja na mshikamano ndiyo nyenzo ya kuwaletea maendeleo wananchi. Aliwataka wananchi kupinga matendo yanayolenga kuhatarisha amani na usalama wa nchi. Aliongeza kuwa usalama wa mkoa pamoja na mambo mengine, unategenea pia malezi sahihi ya watoto. 

Aidha, aliwataka wazazi na jamii kwa ujumla kuwalea watoto katika misingi inayokubalika ili wawe raia wema na wazalendo kwa nchi yao. Alisema kuwa uzalendo wa kweli unategemea sana na malezi sahihi ya watoto. 

Nae Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Richard Kasesela alisema kuwa hali ya usalama katika Wilaya ya Iringa ni shwari kutokana na vyombo vya ulinzi kuwa vimejipanga vizuri. “Wilaya ya Iringa tunaweza kulala usingizi vizuri kwa sababu wapo watu wanaokesha kwa ajili ya usingizi wetu na watu hao ni vyombo vya usalama” alisema Kasesela. Aidha, aliwasilisha ombi kwa Meya wa Manispaa ya Iringa kutenga eneo lingine la kuadhimishia maadhimisho ya mashujaa kubwa ambalo litatoa wigo kwa wananchi wengi zaidi kushuhudia maadhimisho hayo tofauti na eneo la sasa.
=30=

WATUMISHI SERIKALI ZA MITAA WATAKIWA KUSHIRIKIANA NA WAKURUGENZI WAPYA IRINGA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Watumishi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa watakiwa kutoa ushirikiano mzuri Wakurugenzi walioteuliwa hivi karibuni na Rais ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

Kauli hiyo ilitolewa na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Selemani Jafo alioikuwa akiongea na watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa katika ukumbi wa Siasa ni Kilimo, mjini Iringa jana.


Jafo alisema kuwa ili Wakurugenzi waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo, ushirikiano baina ya watumishi na wakuu wa idara ni muhimu na kuwataka watumishi hao kuwapa ushirikiano mzuri Wakurugenzi hao wateule. “Wakurugenzi wapya hakikisheni mnatengeneza mtandao mzuri na wafanyakazi wote. Wapo baadhi ya watumishi kazi yao ni kutengeneza makundi ya fitna kwa Wakurugenzi ili wawachukie baadhi ya watumishi. Mkurugenzi ukikumbatia watumishi wa aina hiyo, basi watumishi hao watakupeleka mahali pabaya” aliongeza Jafo.


Kuhusu ukusanyaji wa mapato, Naibu Waziri alisema kuwa haridhishwi na ukusanyaji mapato hasa vijijini ambapo maeneo mengi hayatumii mfumo wa kieletroniki katika kukusanya mapato ya serikali. “Mapato ya ndani yanaathiriwa sana na mfumo dhaifu wa ukusanyaji mapato, ndiyo maana maelekezo ya serikali ni kutumia mfumo wa kieletroniki katika kukusanya mapato. Mapato ya ndani yasipokusanywa yanatuathiri sote na kushindwa kutekeleza majukumu yetu ikiwa ni pamoja na kwenda vijijini kwa wananchi kufanya kazi” aliongeza Jafo.

Alisema kuwa wapo baadhi ya watumishi wasio waadilifu ambao wametengeneza mfumo wa ulaji kupitia mfumo wa ukusanyaji mapato ya Halmashauri na kumtaka Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo kuwa makini katika kudhibiti mianya ya uvujaji wa mapato ya serikali.

Naibu Waziri huyo, alisema “agenda ya Rais, John Magufuli ni mabadiliko ya kiuchumi, na wananchi wote wanataka mabadiliko ya kweli. Mabadiliko hayo lazima yaletwe na watumishi wa Halmashauri kwa kutimiza wajibu wao katika kufanya kazi. Kama sekta ya maji, afya, elimu, ujenzi na sekta nyingine hazitaenda sawa katika kutekeleza majukumu yake ni dhahiri kuwa wananchi watailalamikia serikali yao, malalamiko hayo yatatokana na baadhi ya watumishi wa Halmashauri kutotimiza wajibu wao”.

Alimshauri Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo kupitia taarifa za kibenki za Halmashauri hiyo na kujiridhisha na mwenendo wa matumizi ya fedha za serikali kabla ya kuingia katika vikao vya Kamati ya fedha ili kudhibiti matumizi yasiyo sahihi ya fedha za serikali.
=30=