Friday, May 1, 2015
HONGERA WAFANYAKAZI WOTE NCHINI
MTANDAO WA MAKTABA YA HABARI UNAWAPONGEZA WAFANYAKAZI WOTE KATIKA SIKUKUU YA WAFANYAKAZI DUNIANI.
MTANDAO HUU UNAENDELEA KUWATAKIA HERI WAFANYAKAZI WOTE KWA KIPINDI CHOTE KINACHOENDELEA ILI WAWEZE KUJILETEA MAENDELEO.
MTANDAO HUU UNAAMINI KUWA UWAJIBIKAJI NA NIDHAMU NI MSINGI WA MAENDELEO YA KIUCHUMI NA KIMKAKATI KWA KILA MFANYAKAZI
Thursday, March 26, 2015
MYUYU AWATAKA WATENDAJI WA KATA KUOMARISHA MAWASILIANO IRINGA
Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Uimarishaji wa mawasiliano baina ya
watendaji wa kata na maafisa tarafa umeelezwa kuwa ni nyenzo muhimu katika
utekelezaji wa kazi za serikali.
Kauli hiyo imetolewa na Katibu Tawala
Msaidizi, Sehemu ya Menejimenti ya Serikali za Mitaa, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa
Iringa, Bw. Wilfred Myuyu alipokuwa akiwasilisha mada kuhusu majukumu ya
watendaji wa kata katika usimamizi wa shughuli mbalimbali za maendeleo wilayani
Kilolo.
Bw. Myuyu amesema kuwa katika
kutekeleza majukumu, mtendaji wa kata anatakiwa kuwasiliana mara kwa mara na
afisa tarafa. Amesema kuwa kwa mujibu wa miongozo ya mawasiliano serikalini,
afisa tarafa anajukumu la kusimamia watendaji wa kata ili watekeleze majukumu
yao ipasavyo. Amesema kuwa kwa mujibu wa sheria ya Tawala za Mikoa Na. 19 ya
mwaka 1997 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2006 inaweka wazi kuwa majukumu ya
afisa tafara ni kusimamia shughuli za watendaji wa kata, vijiji na mitaa katika
eneo lake.
Akiongelea majukumu ya watendaji wa
kata katika ujenzi wa maabara unaoendelea, Bw. Myuyu amesema kuwa watendaji wa
kata wanawajibu wa kuwatambua wadau mbalimbali wa maendeleo wanaoweza kuchangia
na kuwahamasisha kwenye shughuli za ujenzi wa maabara ikiwa ni pamoja na
wananchi. Ameongeza kuwa wanalo jukumu la kufanya ufuatiliaji na tathmini ya
ujenzi unaoendelea ili kujiridhisha na uzingatiwaji wa viwango kusudiwa pamoja
na kasi ya ujenzi. Amesema kuwa katika ufuatiliaji huo wanalojukumu la kufahamu
changamoto zilizopo kushauri na kuzipatia ufumbuzi.
Jukumu linguine amelitaja kuwa ni
kuhakikisha michango inayotolewa na wananchi na wadau inatumika kwa kuzingatia
taratibu zinazoongoza matumizi ya fedha za umma na kutoa taarifa ya matumizi ya
fedha hizo kwa wananchi.
Bw. Myuyu ameongeza kuwa jukumu
lingine ni kutoa taarifa za maendeleo ya ujenzi wa maabara juu ya hatua za
utekelezaji zilizofikiwa, changamoto zilizopo na hatua za utatuzi wa
changamoto.
=30=
MAJI MBEYA KUTOA LITA ZA UJAZO 51,000
Na. Mamlaka ya
Majisafi na Usafi wa Mazingira Jiji la Mbeya
Mamlaka ya Majisafi na usafi wa mazingira Jiji la Mbeya
ina uwezo wa kutoa maji lita za ujazo 51,000 kupitia vyanzo vyake 13 vya maji.
Katika risala ya wafanyakazi wa Mamlaka ya Majisafi
na usafi wa mazingira Jiji la Mbeya iliyosomwa kwa mgeni rasmi na Fundi Mkuu,
Kanda namba 1 Amiri Abdallah Sapi Mkwawa amesema kuwa mahitaji halisi ya maji
katika Jiji la Mbeya ni mita za ujazo 38,000 kwa siku. Amesema kuwa mahitaji
hayo hupanda wakati wa kiangazi kufikia mita za ujazo 43,000 kwa siku katika
miezi ya Septemba hadi Novemba. Amesema kuwa Mamlaka ina jumla ya vyanzo 13 vya
maji vyenye uwezo wa kutoa mita za ujazo 49,000-51,000 kwa siku. Amevitaja
vyanzo hivyo kuwa ni Ivumwe I na Ivumwe II, Nzovwe, Imeta, Sisimba, Hanzya,
Mfwizimo. Vyanzo vingine ni Nsalaga, Lunji, Mwatezi, Mkwanana, Iduda na Halewa.
Amesema kuwa baadhi ya vyanzo vinapungukiwa maji wakati wa kiangazi kutokana na
ukame na shughuli za kibinadamu kama uchomaji wa moto, kilimo na ukataji wa miti
kwa ajili ya kuni na mkaa.
Mkwawa amesema kuwa katika kuhakikisha rasilimali
maji inaendelea kuwepo, Mamlaka kwa kushirikiana na wadau imeendelea na
jitihada za kuhakikisha kuwa vyanzo vya maji vinahifadhiwa. Amesema kuwa
Mamlaka yake inahakikisha kuwa miundombinu ya majisafi na majitaka iliyopo
inatunzwa. “Ili kulipa uzito suala hili Mamlaka kwa kushirikiana na wadau
mbalimbali wakiwemo Jeshi la Polisi, Jeshi la kujenga Taifa, JWTZ, Wakala wa
Misitu Tanzania (TFS), Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira
(NEMC) imeunda kamati ya mazingira kwa lengo la kuhifadhi vyanzo vya maji
vilivyomo kwenye safu za mlima Mbeya ambapo leo hii utaikabidhi kamati sehemu
ya vitendea kazi” Mkwawa.
Mkuu, Kanda namba 1 amesema kuwa Mamlaka imeweza
kuzalisha majisafi na salama na kuyasambaza kwa asilimia 96 ya wakazi wa Jiji
la Mbeya. Amesema katika kuboresha miundombinu ya majisafi na majitaka katika Jiji
la Mbeya fedha za ndani na fedha za wafadhili zimeendelea kutumika. Mradi wa
awamu ya pili na mradi wa kupeleka maji uwanja wa Ndege wa Songwe ni miongoni
mwa maboresho yaliyofanyika.
Amesema katika kukabiliana na uharibifu wa
miundombinu dira za maji, Mamlaka imeendelea kuwabaini na kuwachukulia hatua za
kisheria baadhi ya wezi wa maji. Hatua nyingine ni kuhifadhi vyanzo vya maji
kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.
Akiongelea changamoto zinazoikabili Mamlaka ya Maji,
Mkwawa amezitaja kuwa ni baadhi ya wateja hasa taasisi za umma kutokulipa ankara
za maji kwa wakati au kutokulipa kabisa. Changamoto nyingine ni baadhi ya
vyanzo vya maji vimeendelea kupungukiwa na maji, kutokana na uharibifu wa
mazingira na mabadiliko ya tabia nchi akitolea mfano chanzo cha mto Lunji na
Mfwizimo na Iduda.
Friday, March 20, 2015
KILELE CHA MAADHIMISHO YA WIKI YA MAJI JIJINI MBEYA
Mamlaka ya
Majisafi na usafi wa mazingira jiji la mbeya itaadhimisha kilelel cha wiki ya
maji mwaka 2015 katika viwanja vya Ofisi za Mamlaka ya Maji.
Kilele hicho
kilitanguliwa na Uzinduzi wa wiki ya Maji uliofanyika kuanzia tarehe 16 Machi,
2015 kwa kufanya kazi za usafi wa mazingira katika eneo la ofisi na kwenye
vituo vyote vya kutolea huduma. Aidha, shughuli nyingine ni kuhamasisha
wananchi juu ya ulipaji wa ankara za maji kwa wakati.
Kazi nyingine
zilizofanywa katika wiki hiyo ni pamoja na kutembelea taasisi pamoja na shule
kuhamasisha taasisi kujiunga na mtandao wa majitaka na kupanda miti eneo la
Ivumwe.
Katika kilelel
cha Maadhimisho hayo mada ya Usafi wa Mazingira na Utunzaji wa vyanzo vya Maji
itatolewa.
Michezo na
burudani mbalimbali vitaanikiza ikiwa ni pamoja na mchezo wa kuvuta kamba na
ngoma.
Mgeni rasmi
anatarajiwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Mbeya. Maadhimisho ya wiki ya maji
yanaongozwa na Kaulimbiu isemayo:
Maji
kwa Maendeleo endelevu.
=30=
Tuesday, March 17, 2015
UTUNZAJI MAZINGIRA NI MUHIMU KUENDELEZA RASILIMALI MAJI
Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Tabia
ya utunzaji wa mazingira imeelezwa kuwa ni muhimu katika kuendeleza rasilimali
maji mkoani Iringa.
Kauli
hiyo imetolewa na Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Bw. Adam Swai katika
hotuba yake ya uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya maji katika mkoa wa Iringa
yaliyofanyika katika Kata ya Ruaha, Manispaa ya Iringa.
Bw.
Swai amesema “utunzaji wa mazingira ni
kitu muhimu katika kuhakikisha uendelevu wa rasilimali maji. Sote tunafahamu
kuwa rasilimali maji ni muhimu kwa maisha na maendeleo ya binadamu zikiwepo
shughuli za kiuchumi. Bila maji hakuna maendeleo na bila maendeleo hakuna maji,”.
Akiongelea
kusuasua kwa ujenzi wa miradi ya maji, Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Iringa
amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri kusimamia kikamilifu ujenzi wa miradi ya
maji. Aidha, amewataka kuwapatia kazi makandarasi na wataalamu washauri wenye
uwezo na sifa za kufanya kazi zenye ubora. Amewataka kujiridhisha na uwezo wa
makandarasi kabla ya kuwapatika kazi juu ya ubora wa utendaji kazi wao ili miradi
ikamilike kwa wakati.
Akiongelea
juhudi za kuongeza upatikanaji huduma ya maji mijini na vijijini, ameshauri kutumia
teknolojia ya uvunaji wa maji ya mvua. Ameongeza utumiaji wa teknolojia ya
nguvu ya jua na nguvu ya upepo katika kusukuma maji katika ngazi ya kaya na
taasisi kutokana na urahisi wa teknolojia hizo.
Akiongelea hali ya upatikanaji huduma ya maji mkoani
Iringa, Mhandisi wa Maji Mkoa wa Iringa, Mhandisi Shaban Jellan amesema kuwa
hadi kufikia Disemba, 2014, idadi ya watu waliokuwa wakipata huduma ya maji
ndani ya umbali usiozidi mita 400 toka kwenye makazi yao ni 651,917 sawa na
69.3% ya wakazi wote wa Mkoa wa Iringa.
Akiongelea huduma ya maji vijijini, amesema kuwa
wakazi wa vijijini wanaopata huduma ya maji ni 452,524 sawa na 66.1% ya wakazi wote
waishio vijijini. Ameitaja idadi ya wanaopata huduma ya maji kwa kila Halmashauri
kuwa ni 90% sawa na wananchi 14,213 katika Halmashauri ya Manispaa
(vijijini-peri-urban), 69% sawa na wananchi 175,282 katika Halmashauri ya
Wilaya ya Iringa. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo ni 60.8% sawa na wananchi
93,722 na Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi 64.8 sawa na wananchi 172,258
wanaopata huduma ya maji.
Maadhimisho ya wiki ya maji
mwaka huu yanaongozwa na kauli mbiu isemayo maji na maendeleo endelevu.
=30=
Saturday, March 14, 2015
WIKI YA MAJI TAREHE 16-22 MACHI, 2015
WIKI IJAYO KUANZIA TAREHE 16-22 MACHI NI WIKI YA MAJI.
JIANDAE KUSOMA MAFANIKIO YALIYOPATIKANA KATIKA SEKTA YA MAJI NCHINI KATIKA MTANDAO WAKO UUPENDAO
JIANDAE KUSOMA MAFANIKIO YALIYOPATIKANA KATIKA SEKTA YA MAJI NCHINI KATIKA MTANDAO WAKO UUPENDAO
Saturday, February 28, 2015
DC MBONI AAPISHWA RASMI
Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa IRINGA
Ushirikishaji wananchi na makundi
mengine katika jamii ni njia rahisi ya kuleta tija katika utekelezaji wa Ilani
ya CCM na miradi ya maendeleo mkoani Iringa.
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa
wa Iringa, Amina Masenza muda mfupi baada ya kumuapisha Mkuu mpya wa Wilaya ya
Mufindi, Mboni Mhita katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa
Iringa.
Mhe. Mboni Mhita (kulia) walio kaa na Mhe. Amina Masenza (kushoto). Waliosimama ni Maafisa waandamizi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa |
Masenza amesema kuwa katika
kutekeleza Ilani ya uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010 na miradi yote ya maendeleo
katika Wilaya na Mkoa dhana ya ushirikishaji wananchi na wadau wengine ni
muhimu sana katika kuleta tija ya kazi. Amesema wananchi na makundi mengine
yanaposhirikishwa uelewa wa pamoja unakuwepo na kufanya utekelezaji wake kuwa
ni jukumu la jamii nzima. Amesema kuwa mara nyingi mtafaruku na wananchi
unatokea pale ambapo ushirikishwaji unakuwa mdogo au hakuna kabisa.
Mkuu wa Mkoa amemtaka Mkuu huyo wa Wilaya
kusoma kwa umakini nakala ya wajibu wa Mkuu wa Wilaya na kuuelewa kwa sababu
ndiyo muongozo katika utendaji kazi wa Mkuu wa Wilaya. Amesema kuwa hakuna
jambo lisilowezekana na kumtaka kutumia vizuri vyombo vya usalama na wataalamu
waliopo katika Wilaya ya Mufindi. Aidha, amemtaka kufanya kazi bega kwa bega na
Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Mufindi ili kazi yake iwe nyepesi. Amesema
kuwa Kamati hiyo inawajibu wa kumshauri na kumsaidia katika kutekeleza majukumu
katika Wilaya ya Mufindi.
Mkuu wa Mkoa amesema kuwa wananchi wote
wanamatumaini na Wakuu wa Wilaya katika kutatua matatizo yao. “Wewe ni lulu,
wananchi wote wataangaika sehemu zote watakazokwenda lakini wakifika kwako
watasema hapa tumefika na hapa ndiyo mwisho. Unamwambia mwananchi nenda
mahakamani hataki, nenda polisi hataki nenda kwa Mkurugenzi hataki anajua wewe
ndiye utaweza kumsimamia na wewe peke yako ndiye unaweza.” Alisisitiza Masenza.
Amesema kuwa wananchi wengi
wanamatumaini sana na Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa kwa sababu wanamajibu
ya papo kwa papo kwa matatizo ya wananchi kwa vile vyombo walivyonavyo
vinawafanya kuwa na majibu.
Akitoa shukrani zake, Mkuu wa Wilaya
ya Mufindi, Mboni Mhita amemshukuru Mhe. Rais kwa imani aliyonayo kwake na
kumteua katika nafasi hiyo. Aidha, ameomba ushirikiano na ushauri kadri
inavyowezekana ili kazi yake iwe rahisi. Amemshukuru Mkuu wa Mkoa kwa kumpatia
nasaha na vitendea kazi. “Mbali na vitabu ambavyo umenipa vya Ilani pamoja na Katiba,
maneno yako yamekuwa na uzito sana naomba nikuahidi kwamba nitayazingatia na
pindi nitakapoona kwamba nimekwama au nahitaji ushauri basi sitasita kuja kwako
kuomba ushauri.” Alisisitiza Mboni.
Tukio hilo la kuapishwa kwa Mkuu wa
Wilaya ya Mufindi limeshuhudiwa na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, familia
ya Mboni, watumishi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Wilaya ya Mufindi, waandishi wa
habari na wananchi kwa ujumla.
=30=
MKOA WA IRINGA WAPIGA HATUA UJENZI WA MAABARA
Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Uongozi wa Mkoa wa Iringa umepongezwa kwa
mafanikio makubwa yaliyopatikana katika sekta ya elimu kwa kuongeza kiwango cha
ufaulu.
Pongezi hizo zimetolewa na Waziri Mkuu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mizengo Pinda alipokuwa akifanya
majumuisho ya ziara yake ya Mkoa wa Iringa yaliyofanyika katika ukumbi wa
mikutano wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi.
Mhe. Pinda amesema “napongeza uongozi wa
Mkoa na Wilaya zote kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika sekta ya
elimu.” Amesema Mkoa umefanya vizuri katika elimu ya msingi na sekondari kwa
kuongeza ufaulu wa wanafunzi. Amesema kuwa kwa mujibu wa taarifa ya Mkoa kuhusu
sekta ya elimu, ufaulu wa mtihani wa darasa la saba mwaka 2014 ulikuwa asilimia
68.5 na ufaulu wa kidato cha nne ulikuwa asilimia 65.2.
Akiongelea ufaulu wa kidato cha sita mwaka
2013, Waziri Mkuu amesema kuwa Mkoa ulifanya vizuri na katika matokeo ya kidato
hicho, asilimia 99 ya watahiniwa wote walifaulu. Amesema katika matokeo hayo,
shule ya sekondari Igowole ambayo ni shule ya Kata Wilayani Mufindi iliongoza
kitaifa. Aidha, shule ya sekondari Kawawa pia katika Wilaya ya Mufindi ilikuwa
katika 10 bora kitaifa. Kutokana na mafanikio hayo mazuri, ameutaka uongozi wa
Mkoa kutokurudi nyuma.
Akiongelea agizo la Mhe. Rais la ujenzi wa
Maabara za Sayansi, Mhe. Pinda amewatia moyo viongozi wa Mkoa wa Iringa ili
waendelee na jitihada ya kukamilisha agizo hilo la Mhe. Rais katika kipindi
kilichoongezwa hadi kufikia mwezi Juni, 2015. Aidha, amewataka Wakuu wa Mikoa
nchini kufuatilia ujenzi wa Maabara hizo za Sayansi nchini. Amesema “wito wangu
ni kwa Wakuu wa Mikoa nchini kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa ujenzi wa
Maabara hizo za Sayansi ili Wilaya ziweze kufikia malengo yao kabla ya mwezi
Juni 2015.”
Wakati huohuo, amewataka Wakurugenzi wa
Halmashauri nchini kujenga Maabara mpya na za kisasa zinazoendana na mazingira
ya sasa. Amekosoa hatua ya baadhi ya Halmashauri kukarabati Maabara za zamani
zenye majengo yaliyochakaa na kuwakumbusha kuwa lengo la serikali ni kujenga Maabara
mpya za kisasa zitakazodumu.
Mkoa wa Iringa umefikia asilimia 34 ya ujenzi wa Maabara ambayo ni
sawa na Maabara 108 kati ya mahitaji ya Maabara 318. Maabara 210 zipo katika hatua
mbalimbali za umaliziaji.
=30=
Subscribe to:
Posts (Atom)