Wednesday, September 23, 2015

WATUMISHI FEKI HAWANA NAFASI IRINGA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Mkoa wa Iringa umejipanga kukabiliana na watumishi feki katika sekta ya afya ili kutoa huduma za kitaalam kwa wananchi wake.
Kauli hiyo ilitolewa na Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu alipokuwa akiongea na vyombo vya habari juu ya mkoa ulivyojipanga kukabiliana na changamoto ya watumishi wasio na sifa katika sekta ya afya mkoani hapa kufuatia wimbi la watumishi wasio na sifa kubainika wakitoa huduma katika hospitali za serikali.
Ayubu alisema kuwa mkoa wa Iringa upo makini kimfumo na rasilimali watu kukabiliana na tatizo la watumishi feki. Alisema mifumo ya kuhakiki watumishi imeboreshwa zaidi katika miaka ya hivi karibuni kwa lengo la kukabiliana na watumishi feki.
“Mtumishi yeyote anapoajiliwa anawasilisha vyeti vyake vya kitaaluma alivyonavyo na vinakaguliwa. Kutokana na wimbi la kugushi vyeti, mkoa umepanua wigo kwa kushirikisha taasisi zote zinazohusika na utoaji vyeti husika kama NECTA, NACTE, vyuo vikuu ili wathibitishe uhalali wa vyeti hivyo”, alisisitiza Ayubu.
Aliongeza kuwa mfumo wa kieletroniki wa malipo na mishahara ulioanza mwaka 2011, umeongeza ufanisi katika udhibiti wa vyeti feki kwa sababu mfumo unaingiza vyeti vyote kasha vinaenda kuhakikiwa Menejimenti ya Utumishi wa Umma. Alisema kuwa pamoja na kusaidia kubaini watumishi wenye vyeti feki chini mfumo huo umeondoa tatizo la watumishi kulipwa zaidi ya mara moja na kuondoa changamoto ya mishahara hewa. Katika mfumo huu kama mtumishi alishaajiliwa serikalini mfumo utamgundua kirahisi hivyo kuwa vigumu kulipwa mshahara zaidi ya mmoja. Alisema kuwa hata ule mchezo wa watu kutumia vyeti vya watu wengine unapatiwa tiba.
Ayubu aliongeza kuwa watumishi wote wa serikali wanavaa vitambulisho vya vya kazi vinavyomtambulisha jina kamili na cheo ili iwe rahisi kwa anayepewa huduma kumtambua mtoa huduma. Ameongeza utaratibu huo unaondoa malalamiko kwa wananchi kwa sababu kila mtumishi anafahamika kwa jina na cheo chake.
Ayubu alisema mwaka 2011 mkoa ulifanya uhakiki wa taarifa za watumishi wa umma ili kubaini uwepo wa watumishi hewa. Alisema kuwa anajivunia kutokuwepo kwa watumishi hewa na mishahara hewa.
Afisa utumishi katika ofisi ya mkuu wa mkoa, Gasto Andongwisye alisema katika kuhakikisha mkoa unaendelea kuwa na watumishi wenye sifa kwa mujibu wa taratibu za utumishi wa umma na kudhibiti mishahara hewa, ofisi ya mkuu wa mkoa kupitia sehemu ya utawala na rasilimali watu imeendelea kufanya uhakiki kila mwezi kwa watumishi na ‘payroll’.
Andongwisye aliongeza kuwa katika kuhakikisha hakuna mtumishi mamluki anayejipenyeza katika hospitali za serikali mkoani hapa na kutoa huduma, idara zote katika hospitali wamekuwa wakifanya vikao vya kila siku kupeana taarifa za kazi na vikao vya watumishi wote kila idara kwa lengo la kufahamiana na kujadili changamoto zilizopo.
=30=




No comments:

Post a Comment