Wednesday, January 31, 2018

IRINGA YAPONGEZWA USIMAMIZI UJENZI WA HOSPITALI WILAYA KILOLO



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa
Ofisi ya mkuu wa Mkoa wa Iringa imepongezwa kwa usimamizi makini unaozingatia thamani ya fedha katika ujenzi wa hospitali ya Wilaya ya Kilolo unaoendelea.

Pongezi hizo zilitolewa na makamu mwenyekiti wa kamati ya Bunge ya utawala na serikali za mitaa, Mwanne Mchemba alipokuwa akiongea na wataalam wa Mkoa wa Iringa na Wilaya ya Kilolo katika kumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo baada ya kamati yake kukagua ujenzi wa hospitali hiyo hivi karibuni.
 
Mwanne Mchemba, Makamu Mwenyekiti Kamati ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa
Mchemba alisema kuwa ofisi ya mkuu wa Mkoa wa Iringa imefanya kazi nzuri kusimamia ujenzi wa hospitali ya Wilaya ya Kilolo. 

Najua mipango mizuri ya ujenzi wa hospitali hii mliiratibu vizuri tangu mwanzo ndiyo sababu ujenzi unaenda vizuri. Kamati yangu imeridhishwa na hatua ya ujenzi kwa kuzingatia thamani ya fedha” alisema Mchemba. 

Alipongeza wazo hilo kuwa linalenga kuboresha afya za wananchi wa Wilaya ya Kilolo na taifa kwa ujumla kwa kuwapatia huduma bora za afya.

Mchemba aliishauri ofisi ya Rais TAMISEMI kutoa kipaumbele katika ujenzi wa chumba cha upasuaji na chumba cha kuhifadhia maiti. Alisema kuwa ujenzi wa majengo hayo utasaidia kuiwezesha hospitali hiyo kuanza ikiwa na maeneo muhimu ya utoaji huduma. Aidha, alielekeza hospitali hiyo kupatiwa gari la wagonjwa. 

Kutokana na jiografia ya Wilaya ya Kilolo ni muhimu hospitali ya Wilaya kupewa gari la wagonjwa. Gari hilo ni muhumu sana kwa sababu litasaidia kuokoa maisha ya wananchi watakaohitaji huduma ya haraka na dharura hospitali hapo” alisema Mchemba.  

Awali katika taarifa ya ujenzi wa hospitali ya Wilaya ya Kilolo iliyosomwa na mganga mkuu wa Wilaya, Dr. Mohamed Mang’una alisema kuwa mradi huo ulianza kwa gharama ya shilingi 259,451,899 kugharamia ujenzi awamu ya kwanza na ya pili. Alisema kuwa kupitia ruzuku ya maendeleo ya serikali za mitaa kwa mwaka 2011/2012 zilitolewa shilingi 145,744,500 na mwaka 2012/2013 zilitolewa shilingi 113,707,399 kujenga jengo la wagonjwa wa nje.

Hospitali ya Wilaya ya Kilolo imelenga kuhudumia wakazi wanaokadiriwa kuwa 229,146 kutokana na sense ya watu na makazi ya mwaka 2012.
=30=

No comments:

Post a Comment