Saturday, November 5, 2011

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Jakaya Mrisho Kikwete ametoa salamu za Iddi El Hajji kwa watoto wa makao ya watoto ya Tosamaganga akiwatakia heri katika sherehe hiyo.

Salaam hizo zimetolewa na katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Gertrude Mpaka kwa niaba ya Rais, Dk. Kikwete katika kituo cha makao ya kulelea watoto ya Tosamaganga.
 Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Gertrude Mpaka (kulia) akikabidhi zawadi ya mbuzi kutoka kwa Rais Kikwete kwa kituo cha makao ya watoto cha Tosamaganga




 Baadhi ya watoto wqanaolelewa katika kituo cha makao ya watoto Tosamaganga


Gertrude amesema “nimekuja hapa kufanya mambo makubwa mawili: jambo la kwanza nimekuja kuwafikishia salamu za Iddi El Hajji kutoka kwa Mhe. Dk. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anawatakia heri na fanaka kwa iddi El Hajji”.

Gertrude amesema Mhe. Rais amefarijika sana kushiriki na watoto hao katika kusherehekea sikukuu hiyo ya Iddi El Hajji “alipenda kuwa nanyi hapa, lakini kutokana na majukumu kuwa mengi ametuma salamu za kuwatakia heri na fanaka kwa Iddi El Hajji”. Vilevile, amesema kuwa Mhe. Rais anawatakia watoto wote kusherehekea sikukuu ya Iddi El hajji kwa furaha, amani na kudumisha upendo.

Katibu Tawala Mkoa amelitaja jambo la pili kuwa ni zawadi alizotoa mhe. Rais. “ili muweze kusherehekea vizuri sikukuu hii, Mhe. Rais ametoa zawadi kwenu akiamini mtasherehekea pamoja nae kwa furaha”.

Zawadi alizotoa Rais Kikwete ni mchele kilo 150, mbuzi watatu na mafuta ya chakula lita 40 vyote vikiwa na thamani ya shilingi 555,000.

Akimkaribisha Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Tinna Sekambo amesema Halmashauri yake inavituo vine vinavyotoa huduma ya kulea watoto na kusema kuwa kituo hiki cha Makao ya watoto Tosamaganga ndicho kikubwa na kuushukuru uongozi wa kitaifa kwa kuutambua mchango wa kituo hicho na kuweza kuungana nao katika malezi ya watoto.

Akitoa shukrani zake kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, msimamizi wa kituo hicho Sr Hellen Kihwele amesema “namshukuru sana Rais. Kikwete kwa kutukumbuka mara kwa mara hali inayoonesha upendo wake kwetu sote”.

Sr. Hellen ameyataja matarajio ya baadae ya kituo hicho kuwa ni kukamilisha jingo la shule ya chekechea ambalo halijamalizika kutokana na ukosefu wa fedha na kuiomba jamii iweze kusaidia kukamilisha ujenzi huo.

Thursday, November 3, 2011

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

OFISI YA WAZIRI MKUU 

TAWALA ZA MIKOA ZA SERIKALI ZA MITAA






OFISI YA MKUU WA MKOA WA IRINGA



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU MAADHIMISHO YA MIAKA 50 YA UHURU KIMKOA NA MAPOKEZI YA MBIO ZA MWENGE WA UHURU TAREHE 7-11/11/2011


IMETOLEWA NA;    
MHE. DR. CHRISTINE G. ISHENGOMA (Mb.)
          MKUU WA MKOA WA IRINGA



Sanduku la Posta: 858, IRINGA
Simu: 255 026 2702715/2702021/2702191
Fax:   255 026 2702082
Barua pepe: rasiringa@pmoralg.go.tz


Ndugu Wananchi wa Mkoa wa Iringa:
Tarehe 7 hadi 9 Novemba, 2011 tutakuwa na maadhimisho ya Miaka 50 ya Uhuru kimkoa ambayo yatafanyika katika uwanja wa Kumbukumbu ya Hayati Samora uliopo katika Manispaa ya Iringa. Maadhimisho haya ni maalum kwa ajili ya kufanya tathmini ya shughuli mbalimbali za kimaendeleo na kijamii tulizofanya kimkoa kwa kipindi cha miaka 50.

Ndugu Wananchi wa Mkoa wa Iringa:
Wakati wa maadhimisho haya ambapo kutakuwa na maonesho mbalimbali ya shughuli za maendeleo tunazofanya hapa Mkoani, burudani ya ngoma, sanaa, michezo na hotuba mbalimbali za viongozi katika ngazi za Vijiji, Kata, Tarafa, Wilaya na Mkoa tunapaswa kufanya tathmini kuona wapi tumetoka, wapi tulipo na wapi tunakwenda. Hii itatusaidia kujiwekea malengo mapya ambayo yataongeza kasi ya maendeleo katika Mkoa wetu kama kauli mbiu ya Maadhimisho haya inavyosema “TUMETHUBUTU, TUMEWEZA NA TUNAZIDI KUSONGA MBELE”.

Ndugu Wananchi wa Mkoa wa Iringa;
Maadhimisho haya ya miaka 50 ya UHURU yanakwenda sambamba na mapokezi ya Mwenge wa Uhuru ambao utapokelewa hapa Mkoani Iringa tarehe 09 Novemba, 2011 katika Tarafa ya Wanging’ombe iliyopo katika Wilaya ya Njombe (Mwenge utapokelewa toka Mkoa wa Mbeya) na tutaukabidhi Mkoa wa Ruvuma tarehe 11 Novemba, 2011.

Ukiwa hapa Mkoani, Mwenge wa Uhuru utafungua miradi minne  (4), kuweka mawe ya msingi miradi minne (4) kuzinduliwa mradi mmoja (1) jumla miradi tisa (9) yenye jumla ya thamani ya Tshs. Tshs. 486,833,845/=  Pamoja na kufungua miradi hiyo kutakuwa na mikesha ya Mwenge katika viwanja vya Samora katika Manispaa ya Iringa tarehe 9 na Uwanja wa Sabasaba tarehe 10 katika Halmashauri ya Mji wa Njombe.
Wakiwa Manispaa ya Iringa, wakimbiza Mwenge watapata fursa ya kutembelea mabanda ya maonesho ya shughuli mbalimbali ya miaka 50 ya Uhuru.
TUMETHUBUTU, TUMEWEZA NA TUNAZIDI KUSONGA MBELE.

Ndugu Wananchi wa Mkoa wa Iringa:
Shughuli hizi mbili ni za kihistoria, kwa sababu kila mmoja wetu atapata fursa ya kushuhudia mafanikio tuliyofikia. Hivyo, ninawaomba mjitokeze kwa wingi kuanzia tarehe 7 hadi 11 Novemba, 2011 kwenye maonesho tutakayofanya katika uwanja wa Samora na kwenye mapokezi ya Mwenge wa Uhuru ili tuweze kwa pamoja kuiandika historia ya Mkoa wetu vizuri kwa manufaa yetu wenyewe na vizazi vijavyo.


ASANTENI KWA KUNISIKILIZA

TUMETHUBUTU, TUMEWEZA NA TUNAZIDI KUSONGA MBELE.

Wednesday, November 2, 2011

KWANZA JAMII LIPEWE USHIRIKIANO

Serikali Mkoani Iringa imeahidi kuendelea kutoa ushirikiano kwa vyombo vya habari vya Mkoani hapa na nje ya Mkoa ili kuhakikisha uhuru wa upatikanaji habari unashamiri na wananchi wanapata habari zinazohusu maendeleo yao.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma akizundua gazeti la Kwanza Jamii-Iringa  

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma akiongea na mmoja wa wajumbe wa bodi wa gazeti la Kwanza Jamii Maggid Mjengwa

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma wakati akizindua gazeti la Kwanza Jamii-Iringa katika sherehe za uzinduzi zilizofanyika katika uwanja wa shule ya sekondari Mwembetogwa katika Manispaa ya Iringa.

Dk. Ishengoma amesema “ieleweke kuwa serikali imekuwa na ushirikiano mkubwa na mzuri na vyombo vya habari, mara nyingi Mhe. Rais amehimiza ushirikiano huo kwa watendaji wengine, huku akiwataka wananchi kuvitumia vyombo hivyo kwa manufaa ya taifa”.

Aidha, amewataka wananchi wa Mkoa wa Iringa kujitokeza na kutoa ushirikiano wao kwa gazeti hilo kwa manufaa ya maendeleo ya Mkoa wa Iringa. Amewataka kuwa wadau kwa kununua nakala na kutoa matangazo yao ili kulifanya gazeti hilo kuwa endelevu.

Mkuu wa Mkoa amewataka wananchi wa Mkoa wa Iringa, kulitumia gazeti hilo kama jukwaa la kusemea na kuwaunganisha na viongozi wao kwa manufaa ya maendeleo ya wana Iringa.

WALIMU WATOE DARASA LA VVU/UKIMWI

Walimu Mkoani Iringa wameshauriwa kutumia muda wao kuzungumzia masuala ya VVU/UKIMWI na madhala yake katika jamii pindi wanapokuwa wakifundisha katika utaratibu wao wa kawaida ili kuongeza uelewa kwa wanafunzi.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma alipokuwa akiongea na waandishi wa habari wa Mkoa wa Iringa ofisini kwake katika utaratibu wake wa kawaida wa kukutana na waandishi wa habari mara kwa mara na kujadili masuala ya maendeleo na changamoto katika Mkoa.

Dk. Ishengoma amesema “ukimwi ni tatizo sana katika Mkoa wetu wa Iringa hivyo hata kama haupo katika mitala ya elimu lakini ni vizuri kila mwalimu akachukua angalau dakika tano anapoanza au anapomaliza kipindi kuelezea masuala ya UKIMWI”.

Amesema katika kukabiliana na janga hili ni lazima elimu itolewe kwa umakini mkubwa kuanzia darasa la tatu na kuendelea kwa misingi ya kuwaandaa vijana na mapambano hayo.

Akiongelea dawa ya kudumu dhidi ya UKIMWI amesema ipo wazi nayo ni wananchi kubadili tabia sambamba na elimu dhidi ya kujikinga na maambukizi. Amesema kwa wale waaminio basi watumie maandiko matakatifu kama kinga na wale wasioweza kabisa basi zana zitumike, “ila dawa ni wewe mwenyewe kubadili tabia”.

Mkuu wa Mkoa huyo aliwaagiza waandishi wa habari kujikita katika kuandika habari na makala zinazoelezea madhara ya UKIMWI katika jamii ili kuweza kueneza habari hizo na hatimae kuifikishia jamii taarifa sahihi ili kuweza kuinusuru na kuongeza nguvu kazi katika Mkoa na Taifa.  

IRINGA YAPATA MGAO WA VOCHA

Mkoa wa Iringa unatarajia kupata mgao wa jumla ya vocha 693,000 za pembejeo za kilimo kwa mwaka wa fedha 2011/ 2012.

Akiwasilisha mapendekezo ya mgao wa vocha za pembejeo za kilimo kwa kila Halmashauri kwa msimu wa mwaka 2011/2012 katika kamati ya vocha ya mkoa wa Iringa, Afisa Kilimo Mkoa wa Iringa, Shenal Nyoni ameyataja mapendekezo hayo kwa kila Halmashauri kuwa ni Mufindi (kupandia 44,300, kukuzia 44,300, chotara 44,000, mpunga 300), Makete (kupandia 23,700, kukuzia 23,700, chotara 23,700), Iringa (kupandia 45,000, kukuzia 45,000, chotara 43,500, mpunga 2,500), Njombe Mji (kupandia 21,000, kukuzia 21,000, chotara 21,000), Manispaa (kupandia 4,000, kukuzia 4,000, chotara 4,000), Kilolo (kupandia 26,000, kukuzia 26,000, chotara 25,800, mpunga 200), Njombe (kupandia 42,500, kukuzia 42,500, chotara 42,500) na Ludewa (kupandia 24,500, kukuzia 24,500, chotara 24,000 na mpunga 500).

Akiongelea thamani za vocha moja moja msimu katika msimu wa mwaka 2011/ 2012  Nyoni amesema kuwa vocha za kupandia kilo 50 ni shilingi 28,000, kukuzia kilo 50 ni shilingi 18,500, mahindi chotara kilo 50 ni shilingi 20,000 na mpunga kilo 50 ni shilingi 12,000.

Ili kuhakikisha usimamiaji wa vocha hizo za pembejeo unakuwa madhubuti, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma amewaagiza wakuu wa Wilaya kusimamia vizuri mchakato mzima wa vocha katika wilaya zao. Vilevile, amewaagiza Wakuu hao wa Wilaya kutokuwafumbia macho mawakala wasio na vigezo ili huduma hiyo iweze kufanikiwa na kuwanufaisha wananchi kama yalivyo madhumuni ya Serikali.

Amesema “mfumo huu wa vocha ni mzuri sana ila una mianya ya rushwa hivyo tusichague mawakala matapeli bali  tuchague mawalaka wenye rekodi nzuri na wasio na madeni” alisisitiza Mkuu wa Mkoa.

KAMATI YA VOCHA NAYO YANYOOSHEWA KIDOLE

Kamati ya vocha ya ruzuku ya pembejeo za kilimo ngazi ya Mkoa wa Iringa imetakiwa kufanya kazi kwa uangalifu mkubwa katika kusimamia menejimenti ya vocha za pembejeo za kilimo ikiwa ni pamoja na mfumo wa uchaguzi wa mawakala unaozingatia vigezo na uwezo.

Rai hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya vocha za ruzuku ya pembejeo za kilimo ngazi ya mkoa ambae pia ni Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma “kamati na kila mmoja ni lazima awe mwangalifu katika kusimamia menejimenti ya ugawaji na usambazaji wa vocha za pembejeo za kilimo ili kuhakikisha zoezi zima linafanikiwa”. Ameongeza kuwa lazima utumike mfumo mzuri na madhubuti wa kuwapata mawakala utakaozingatia vigezo na uwezo wao ili kuondoa ubabaishaji ambao umekuwa ukijitokeza na kusababisha wakulima kutokunufaika na ruzuku hiyo ya serikali wakati mawakala wakiendelea kutajirika kupitia migogo ya wakulima. Amesisitiza kuwa ni vizuri kuwa na mawakala wachache wenye vigezo kuliko kuwa na mawakala wengi wasio na vigezo.     

Akiwakilisha taarifa ya upatikanaji na usambazaji wa vocha za ruzuku ya pembejeo za kilimo kwa mwaka 2010/2011, Afisa Kilimo katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Shenal Nyoni amesema kuwa Mkoa umepokea vocha zenye thamani ya shilingi Bilioni 21.6. Amesema vocha za ruzuku ya pembejeo za kilimo zilizopokelewa na Mkoa ni za kutosha Kaya 336,635 ambazo ni sawa na vocha 1,009,905 kwa ujumla wa nakala moja moja ya vocha.

Akiongelea idadi ya mawakala kwa Mkoa wa Iringa katika kipindi husika, Nyoni amesema kuwa Mkoa ulikuwa na mawakala 514 waliofanya kazi ya kusambaza pembejeo za kilimo. Amesema miongoni mwa mawakala hao mawakala 390 ndio waliofanya kazi ya kusambaza pembejeo katika ngazi ya vijiji na kata kwa utaratibu wa mfumo wa ruzuku ya pembejeo.

Nyoni amesema changamoto kubwa ni malalamiko kutoka kwa wakulima juu ya kuongezeka kwa bei ya mbolea ilikinganishwa na msimu uliopita. Amesema msimu uliopita bei mkulima alichangia shilingi 48,000 hadi 65,000 ikilinganishwa na msimu 2010/2011 aliochangia shilingi 85,000 hadi 90,000 kwa pembejeo za ekari moja yaani mbegu bora, mbolea ya kupandia na kukuzia. 

MA DC WAAGIZWA KUSIMAMIA VOCHA



MKUU wa Mkoa wa Iringa amewaagiza Wakuu wa Wilaya kusimamia vizuri mchakato wa vocha za pembejeo za kilimo kwa kutokuwafumbia macho mawakala wababaishaji na wanaojinufaisha kupitia migongo ya wakulima ili kuondoa manung’uniko na wakulima kunufaika na mfumo huu wa vocha za ruzuku za serikali.


Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma 
Agizo hilo limetolewa na Mwenyekiti wa kamati ya vocha za pembejeo ambae pia ni Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma katika kikao cha kamati ya vocha za pembejeo mkoa wa Iringa kilichofanyika katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa.   

Dk. Ishengoma amesema “ili kuhakikisha usimamiaji wa vocha hizo za pembejeo unakuwa madhubuti, ni lazima wakuu wa Wilaya kusimamia vizuri mchakato mzima wa vocha katika wilaya zenu”. Aidha, amewataka Wakuu hao wa Wilaya kutokuwafumbia macho mawakala wasio na vigezo ili huduma hiyo iweze kufanikiwa na kuwanufaisha wananchi kama yalivyo madhumuni ya Serikali.

Amesema “mfumo huu wa vocha ni mzuri sana ila una mianya ya rushwa hivyo tusichague mawakala matapeli bali  tuchague mawalaka wenye rekodi nzuri na wasio na madeni na wasio wababaishaji kwa sababu lengo la serikali ni kumsaidia mkulima kwa kumpunguzia gharama katika pembejeo za kilimo” alisisitiza Mkuu wa Mkoa.

Aidha, Mkuu wa Mkoa aliagiza kamati ya vocha ya Wilaya na Wataalam wa kilimo kuwaelimisha wakulima juu ya utaratibu wa awali wa kufikisha pembejeo kwa wakulima kulingana na fomu zalizowasilishwa ma Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika.

Akiwasilisha mapendekezo ya mgao wa vocha za pembejeo za kilimo kwa kila Halmashauri kwa msimu wa mwaka 2011/2012 katika kamati ya vocha ya Mkoa wa Iringa, Afisa Kilimo Mkuu katika Ofisi ya Mkuu Mkoa wa Iringa, Shenal Nyoni ameyataja mapendekezo hayo kwa kila Halmashauri kuwa ni Mufindi (kupandia 44,300, kukuzia 44,300, chotara 44,000, mpunga 300), Makete (kupandia 23,700, kukuzia 23,700, chotara 23,700), Iringa (kupandia 45,000, kukuzia 45,000, chotara 43,500, mpunga 2,500), Njombe Mji (kupandia 21,000, kukuzia 21,000, chotara 21,000), Manispaa (kupandia 4,000, kukuzia 4,000, chotara 4,000), Kilolo (kupandia 26,000, kukuzia 26,000, chotara 25,800, mpunga 200), Njombe (kupandia 42,500, kukuzia 42,500, chotara 42,500) na Ludewa (kupandia 24,500, kukuzia 24,500, chotara 24,000 na mpunga 500).

Akiongelea thamani za vocha moja moja msimu katika msimu wa mwaka 2011/ 2012  Nyoni amesema kuwa vocha za kupandia kilo 50 ni shilingi 28,000, kukuzia kilo 50 ni shilingi 18,500, mahindi chotara kilo 50 ni shilingi 20,000 na mpunga kilo 50 ni shilingi 12,000.

Nyoni amesema kuwa Mkoa unatarajia kupata mgao wa jumla ya vocha 693,000 za pembejeo za kilimo kwa mwaka wa fedha 2011/2012.

VIJANA PUNGUZENI KASI YA VVU/ UKIMWI


VIJANA mkoani Iringa wametakiwa kuwa wajumbe makini katika kupunguza kasi ya maambukizi ya virusi vya UKIMWI na kujilinda kwa kutumia mafundisho ya MUNGU kama silaha kubwa katika kujilinda na ugonjwa huo.

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma wakati akifunga semina ya siku mbili ya vijana iliyoandaliwa na Kanisa Katoliki Parokia ya Kihesa katika manispaa ya Iringa.

Dk. Ishengoma amesema “mkoa wetu sasa unaongoza kwa maambukizi ya UKIMWI ukiwa na kiasi cha asilimia 15.7 ya maambukizi”. “Naomba kila mmoja wetu awe mjumbe katika kupunguza kasi ya maambukizi haya”. Amesema kwa kufanya hivyo kiasi cha maambukizi kitapungua sana. Aidha, amewasisitiza vijana kujilinda kwa kufuata mafundisho ya Mungu kama silaha kubwa katika kujilinda huko. Akikariri Kitabu cha Waefeso 6:11 “vaeni silaha zote za Mungu mpate kuweza kuzipinga hila za shetani”.

Vilevile, amewaasa vijana wote kujenga tabia ya kushiriki kikamilifu katika michezo mbalimbali kwa malengo ya kuimarisha afya zao, uwezo wa kufikiri na kujipatia ajira.

Amewaomba walimu na viongozi wa dini kuhakikisha vijana wanafanikiwa. Amesema “walimu wa mafundisho ya dini ni nguzo muhimu katika kuhakikisha vijana wanafanikiwa, nawaomba walimu wote na viongozi mbalimbali wa taasisi za dini tutumie nguvu zetu zote kuwapa elimu vijana wetu” alisisitiza Mkuu wa Mkoa wa Iringa.

Ameshauri kuwa vijana ni taifa linalotegemewa hivyo kwa kutumia karama ya ualimu. Ni vizuri wakatumia tunu hiyo kuufikisha ujumbe wa Mungu kwa vijana na waumini wote. Ameshauri kuendelea kuwafundisha maadili mema ili wafanikiwe katika maisha. Amesema kuwa wapo vijana wakorofi ambao huchangia pia kuharibu nidhamu ya vijana wengine hao wanahitaji mtumie bisara na utu zaidi ili warudi katika nidhamu inayotakiwa.

Akiongelea suala la anami iliyopo nchini, Dk. Ishengoma amesema  “niwakumbushe suala la amani iliyopo nchini kwa sasa”. Watanzania siku zote tunaishi kwa amani na mshikamano mkubwa. Amesema “hivi vyote vimejengwa na waasisi wetu ambao walituunganisha tukawa kitu kimoja”. Amesisitiza kuwa wote kwa pamoja kuimarisha na kudumisha zaidi mshikamano na amani iliyopo ili watanzania waendelee kuishi kwa utulivu na upendo.

Katika mmomonyoko wa maadili, Dk. Ishengoma amesema “katika jamii yetu wote tumeshuhudia mmomonyoko wa maadili, tumeshuhudia vijana wakilewa, wakikosa hekima na busara, dharau, vijana kuvuta na kusafirisha dawa za kulevya”. Amesema mmomonyoko huu unatokana na kutofuata mafundisho ya Mungu. Aidha, aliuomba uongozi wa kanisa kusaidia kwa kadri iwezekanavyo kuwafundisha maadili mema vijana na waumini wao kwa ujumla.

Kanisa Katoliki Parokia ya Kihesa kupitia umoja wa vijana umeandaa semina kwa vijana kwa lengo la kuwaimarisha kimwili na kiroho pamoja na kuwapokea vijana waliohitimu shule ya msingi na kujiunga na umoja huo ili kuweza kuepukana na majanga mbalimbali yanayowakumba vijana kulingana na hali halisi ya utandawazi.


Monday, October 24, 2011

IKAMA YA WATUMISHI 662 IRINGA


MKOA wa Iringa umeidhinishiwa IKAMA ya watumishi 662 katika mwaka wa fedha 2011/ 2012 katika kutekeleza majukumu yake.

Akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Sehemu ya Utumishi na Utawala kwa mwezi Julai hadi Septemba 2011/ 2012 katika kikao cha kudhibiti Mapato na Matumizi ya serikali katika ofisi yake, kwa niaba ya Katibu Tawala Msaidizi, Sehemu ya Utawala na Rasilimali watu Afisa Tawala katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Neema Mwaipopo amesema kuwa “kwa kipindi cha Julai- Septemba 2011/ 2012 Sekretarieti ya Mkoa ilipokea IKAMA iliyoidhinishwa mikoa ya Iringa na Njombe”.

Amesema Mkoa wa umeidhinishiwa kuwa na watumishi 662. Amesema kuwa watumishi waliopo ni 578 na nafasi wazi kuwa 84 na kati ya hizo ajira mbadala ni 48 na ajira mpya ni 36.

 Neema Mwaipopo, Afisa Tawala katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa

Amesema kuwa mkoa wa Njombe umeidhinishiwa kuwa na watumishi 423 kati ya 71 waliopo na nafasi wazi 352. Amesema kati ya hizo ajira mbadala ni 10 na ajira mpya ni 342. Aidha, amesema kuwa maombi ya kujaza nafasi wazi 378 katika Sekretarieti ya Mkoa wa Iringa na Njombe na maombi ya kibali cha ajira mbadala 58 yamewasilishwa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma kwa mujibu wa taratibu zilizopo.

Akiongelea mafunzo kwa watumishi katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mwaipopo amesema katka kipindi hicho watumishi wanne wameanza kuhudhuria mafunzo ya muda mrefu katika chuo kikuu cha Tumaini na chuo cha Uhasibu (TIA). Amesema kuwa madhumuni ya mafunzo hayo ni kuimarisha utendaji kazi na ufanisi katika kazi kwa mujibu wa mpango wa mafunzo wa mkoa.

Akifunga kikao hicho Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma (Mb.) amewataka wafanyakazi katika Ofisi yake kufanya kazi kwa umakini mkubwa na uwajibikaji ili kuleta tija katika mkoa na taifa kwa ujumla. Aidha, amewataka kila mtumishi kurejea kipengele kinachomhusu katika Ilani ya uchaguzi ya chama kinachotawala na kuweka utaratibu wa utekelezaji wake.

Kikao cha kudhibiti mapato na Matumizi hufanyika kila baada ya miezi mitatu na hujadili pamoja na mambo mengine mapato na matumizi ya fedha za serikali.

RC AAGIZA MATUMIZI MAZURI YA FEDHA ZA SERIKALI

MKUU wa Mkoa wa Iringa ameagiza matumizi mazuri ya fedha za serikali kadri zilivyopangwa ili ziweze kuwanufaisha wananchi walio wengi katika jitihada za kuondoa umasikini na kuinua maisha ya kila siku.

Agizo hilo limetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma (Mb.) katika kikao cha robo ya kwanza cha kudhibiti Mapato na Matumizi ya serikali katika ofisi yake kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa ofisi yake. 

 Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. christine Ishengoma (Mb.)

Dk. Ishengoma aliyekuwa mwenyekiti wa kikao hicho amesema “lazima fedha za serikali zitumike vizuri kadri zilivyopangwa hasa upande wa miradi ya maendeleo ili ziwanufaishe wananchi wengi”.
Amesisitiza kufuatwa kanuni na taratibu za kihasibu ikiwa ni pamoja na ulipwaji wa madai mbalimbali kwa muda ili kuongeza ufanisi wa kazi na hatimae mkoa kupata hati safi ya kiukaguzi.

Aidha, Mkuu wa Mkoa ameagiza kufanyiwa kazi mapungufu yote yaliyobainishwa katika ripoti ya Mkaguzi na Mthibiti mkuu wa hesabu za serikali kwa mwaka wa fedha 2009/ 2010 mapema na kuwasilisha taarifa hiyo sehemu husika na kuhakikisha mapungufu hayo hayajitokezi kwa mara nyingine. 

Akiwasilisha taarifa ya Mkaguzi wa Nje kuhusu mapungufu yaliyojitokeza katika ripoti ya Mthibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa mwaka wa fedha 2009/2010 kwa mkoa wa Iringa, Mkaguzi Mkazi, Ismail Mbiru amesema kuwa ripoti hiyo imebaini mapungufu kadhaa yaliyoainishwa kwa kila Halmashauri kwa ajili ya kuyatolea majibu sahihi ili kuleta ufanisi katika kusimamia mapato ya Halmashauri.
Mbiru ameyataja mapungufu hayo kuwa ni pamoja na kuwasilisha taarifa zenye mapungufu makubwa, taarifa zenye nyaraka pungufu, taarifa za halmashauri ambazo fedha za mfuko wa maendeleo ya jimbo hazijatumika na kuwasilisha taarifa zenye hati zenye shaka.

Mapungufu mengine ameyataja kuwa ni kuwasilisha taarifa yenye wadaiwa wasiolipa na wasiolipwa, kuwasilisha taarifa zenye mishahara isiyolipwa na haikurejeshwa Hazina na kuwasilisha taarifa ya vitabu vya maduhuli ambayo hayajarejeshwa na mawakala wa kukusanya mapato.

Wednesday, October 19, 2011

WELLINGTON HARRISON TURNER GONDWE-Jr


Wellington Harrison Turner Gondwe, alizaliwa tarehe 11 Oktoba, 1987 mjini Morogoro.

Alibatizwa mwaka 1990 katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, Usharika wa Bugando na alipata Kipaimara mwaka 2001 katika Usharika huohuo.

Alijiunga na shule ya msingi Mlimani mwaka 1994 na kuhitimu darasa la Saba katika Shule ya Msingi ya Lake mwaka 2002.
Aidha, alijiunga na Shule ya Sekondari ya Murutunguru iliyopo Wilayani Ukerewe mwaka 2003 hadi Juni, 2004.

Baada ya hapo alihamia katika Shule ya Sekondari ya Thaqaafa Julai, 2004- 2006. Kutokana na ugonjwa hakuweza kufanya mitihani yake ya kidato cha Nne iliyotarajiwa kuanza 22 Oktoba, 2006.

Wellington alianza kuugua Malaria kali tarehe 3 Oktoba, 2006. Aidha, alilazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando tarehe 10 Oktoba, 2006.

Pamoja na jitihada za Madaktari za kunusuru maisha yake kushindikana na roho kushindana na mauti, alifariki tarehe 20 Oktoba, 2006 saa 12 kamili jioni.

BWANA alitoa na BWANA ametwaa jina lake lihimidiwe.


WATUMISHI WA UMMA NA HUDUMA BORA


Watumishi wa Umma wamekumbushwa kuendelea kutoa huduma bora kwa jamii na kuhakikisha jamii inaridhika na huduma hiyo pamoja na changamoto zilizopo.
Rai hiyo imetolewa na Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, George Masaju alipokuwa akiongea na wafanyakazi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa katika ukumbi wa mikutano wa ofisi hiyo.
Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Bw. George Masaju (kulia) akiongea na wafanyakazi wa Ofisi ya mkuu wa Mkoa wa Iringa hawapo pichani na Kaimu mkuu wa Mkoa wa Iringa, Bw. Aseri Msangi (kushoto)
Masaju amesema “tunatambua kuwa sisi ni watumishi wa Umma na tuna maadili yetu ya kazi kwa mujibu wa Sheria ya Utumishi wa Umma Na. 8 ya mwaka 2002 na mabadiliko yake Na. 17 ya mwaka 2007”. Amesema kwa msingi huo wa utumishi wetu wa Umma “sote kwa pamoja lazima huduma zetu tuzitoe kwa ubora na kwa viwango vya kuridhisha kwa Umma”.
Amesema “nawajibika kuwakumbusha wajibu wetu sote kwa Serikali na tukumbuke kuwa sisi ndio watendaji wa kuwasaidia viongozi wetu wa juu”.
Aidha, amewakumbusha kuwa wafanyakazi katika ngazi za mikoa na Halmashauri ndio walio karibu zaidi na wananchi hivyo wanawajibika kufanya kazi kwa uwezo wao na viwango kwa kutoa huduma bora kwa wananchi.

Amesema utoaji wa huduma bora kwa wananchi unasaidia katika kuondoa kero na kupunguza malalamiko ya wananchi dhidi ya Serikali yao.
Akisisitiza dhana ya ubora wa huduma kwa wananchi, Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali amesema kuwa ubora huo ujikite katika utoaji wa maamuzi sahihi na yanayotolewa katika muda muafaka.
Ametolea mfano wa huduma zikitolewa vizuri katika idara ya polisi na mahakama kutasaidia kupunguza uhalifu.
Vilevile, amesisitiza kuwa jukumu la kudhibiti uhalifu nchini si la idara ya polisi na mahakama pekee bali ni jukumu linalohitaji msukumo wa pamoja baina ya mamlaka zinazohusika na wananchi kwa umoja wao.

Sunday, October 9, 2011

KKKT DAYOSISI YA KUSINI KUJENGA CHUO KIKUU

Askofu mteule wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Dayosisi ya Kusini Njombe ameazimia kuanzisha ujenzi wa chuo kikuu cha dayosisi katika ukanda wa kusini ili kuendeleza na juhudi za kanisa katika kuiletea jamii ustawi.
Kauli hiyo imetolewa na Askofu mteule Isaya Japhet Mengele baada ya kusimikwa kazini na Mkuu wa KKKT nchini Askofu. Dk. Alex Malasusa katika kanisa kuu, Dayosisi ya Kusini-Njombe.
Akiongelea mipango yake ya baadae Askofu Mengele amesema ni ujenzi wa chuo kikuu cha dayosisi katika ukanda huo wa kusini ili kuwanufaisha wananchi wengi katika sekta ya elimu.
Aidha, akiongelea dhana ya kilimo kwanza, Askofu. Mengele ameipongeza serikali kwa hatua hiyo na kuishauri kuwa kilimo kwanza ili kitoe matokeo mazuri kifanyike kwa kanda kutokana na mazao yanayozalishwa katika kanda husika ili kuongeza chachu na kuinua kilimo ili kiwanufaishe wananchi wengi zaidi.
Akiongelea sekta ya elimu amesema ataendelea kushirikiana na serikali katika kuboresha utoaji wa elimu nchini. Aidha, ameishauri Serikali huongeza kasi katika kuifanya hospitali teule ya Ilembula kuwa hospitali ya rufaa ikiwa ni pamoja na kuisaidia gari la kubebea wagonjwa ili kuwasaidia wananchi wengi.
Katika salamu za Mkoa wa Iringa, zilizotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma, amempongeza Askofu mteule Mengele kwa uteuzi wake. Aidha, amewaomba viongozi wa dini na wananchi kwa ujumla wao kukaa chini na kutafakari juu ya nchi na kuiombea ili iendelee kuwa na amani, upendo na utulivu.
Vilevile, Dk. Ishengoma imelishukuru kanisa la kiinjili la kilutheri Tanzania kwa michango na ushiriki wake katika kuiletea maendeleo jamii. Ameitaja michango hiyo kuwa ni pamoja na kuijenga jamii katika maadili na kuwafanya wananchi wake kuwa raia wema, mingine ni elimu na afya. 
Nae Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, George Mkuchika aliyemuwakilisha Waziri Mkuu aliyepo safarini nchini Brazili amewataka viongozi wa dini kukemea maovu, na kuwataka waumini kufuata mfundisho ya dini na kujitolea kulijenga kanisa lao na nchi yao.

RASILIMALI ZA NCHI ZIWANUFAISHE WANANCHI

Serikali imeshauriwa kuhakikisha kuwa rasilimali za nchi zinatumika kwa maslahi ya nchi na kuwanufaisha wananchi wenyewe walio wengi.
Ushauri huo umetolewa na Askofu mteule wa Dayosisi ya Kusini- Njombe, Askofu. Isaya Japhet Mengele katika ibada ya kumsimika na kumuingiza kazini msaidizi wa Askofu, Mch. Dk. George Mark Fihavango iliyoongozwa na Mkuu wa KKKT nchini Askofu. Dk. Alex Malasusa iliyofanyika katika kanisa kuu, Dayosisi ya Kusini Njombe.
Askofu. Mengele amesema kuwa rasilimali za nchi zinapogawanywa kwa maslahi ya nchi na wanufaikaji wakawa ni wananchi, nchi hutawaliwa kwa amani na utulivu. Aidha, ameshauri pia migodi itakayoanzishwa katika ukanda wa kusini mwa nchi, uanzishwaji, uratibu na usimamizi wake lazima uwe mzuri ili kuepusha migogoro inayoshuhudiwa katika ukanda wa kaskazini mwa nchi.
Akiongelea uhifadhi wa mazingira, amesema kuwa ni muhimu kwa Serikali na wadau wengine wote wa maendeleo na wenye mapenzi mema na nchi hii kutilia mkazo dhana ya uhifadhi wa mazingira ili kuinusuru nchi na uharibifu unaotokana na uharibifu wa mazingira ili nchi iwe mahali salama kwa ustawi wa binadamu wake.
Askofu mteule Mengele ameipongeza Serikali katika jitihada zake za kuwaletea wananchi maendeleo na kusifu Serikali kutojiingiza katika masuala la kidini hali inayochangia ukuaji na ustawi wa uhuru wa kuabudu unaoendana na misingi ya kidemokrasia nchini.
Akimsimika rasmi, Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania, Askofu. Dk. Alex Malasusa amewataka viongozi wa dini kutokutumia nafasi zao kwa maslahi ya kisiasa.
Katika salamu za Mkoa wa Iringa, zilizotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk. Christine Ishengoma, amempongeza Askofu mteule Mengele kwa uteuzi wake. Aidha, amewaomba viongozi wa dini na wananchi kwa ujumla wao kukaa chini na kutafakari juu ya nchi na kuiombea ili iendelee kuwa na amani, upendo na utulivu.
Vilevile, Dk. Ishengoma imelishukuru kanisa la kiinjili la kilutheri Tanzania kwa michango na ushiriki wake katika kuiletea maendeleo jamii. Ameitaja michango hiyo kuwa ni pamoja na kuijenga jamii katika maadili na kuwafanya wananchi wake kuwa raia wema, mingine ni elimu na afya.