Friday, May 25, 2012



WAANDISHI HABARI HAMASISHENI SENSA

Mkuu wa Mkao wa Iringa amewataka waandishi wa habari, viongozi wa dini na wazee mashuhuri Mkoani Iringa kuhamasisha wananchi juu ya uelewa wa Sensa ya watu na Makazi ili waweze kujitokeza na kuhesabiwa hapo Agosti 26, 2012.

Wito huo ameuto Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dkt. Christine Ishengoma katika taarifa yake aliyoitoa kwa waandishi wa habari, viongozi wa dini, wazee mashuhuri na vyombo vya ulinzi na usalama kuhusu uhamasishaji wa wananchi kushiriki katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi leo alipokutana nao katika ukumbi wa mikutano wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa.

Dkt. Christine amesema kuwa kutokana na umuhimu wa Sensa ya Watu na Makazi nchini, nafasi za makundi mbalimbali ni muhimu sana katika kusaidia kutoa elimu na hamasa, amesema “hamna budi kufahamu kuwa takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ndizo zitakazoiwezesha Serikali kutambua hali halisi na mahitaji halisi ya huduma zilipo katika maeneo yenu hivyo kuingizwa katika mipango ya maendeleo ya taifa”.

Amesema kutokana na msingi huo makundi hayo aliyokutana nayo yanapaswa kuhamasisha wananchi ili waweze kuhesabiwa na kusisitiza kuwa kuhesabiwa huko iwe ni mara moja tu kuwezesha takwimu zitakazokusanywa ziwe sahihi na za uhakika. Amesema kuwa iwapo takwimu zote zitakazokusanywa zitakuwa sahihi, huo ndio utakuwa utimilifu wa takwimu za Sensa kitaifa.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa amesema kuwa mambo muhimu ya kuzingatia wakati ya kuhamasisha wananchi ni pamoja na tarehe ya Sensa, umuhimu wa Sensa na yatakayojiti wakati wa zoezi la kuhesabu watu.
Akiwatoa hofu wananchi kuhusu mawazo potofu dhidi ya zoezi la Sensa, Mratibu wa Sensa Mkoa wa Iringa, Fabian Fundi amesema kuwa zoezi la Sensa ya Watu na Makazi halihusiani kabisa na hofu walizonazo wananchi. Amesema “ni muhimu sana kuwatoa hofu wananchi kwa kuwaelimisha kuwa zoezi la Sensa halihusiani kabisa na hofu au imani walizonazo”.

Fundi, amesisitiza kuwa wananchi wawe huru kutoa taarifa watakazoulizwa katika dodoso na kuwahakiihsia kuwa taarifa hizo zitatumika kwa mambo ya kitakwimu pekee na kwa usiri mkubwa.

Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Gertrude Mpaka amesema amewataka wananchi kuwatoa watoto wote na watu wenye ulemavu ili waweze kuhesabiwa na kuiwezesha Serikali kuangalia njia bora ya kuwahudumia vizuri zaidi. Aidha, amekemea tabia ya baadhi ya wanajamii kuwaficha watoto wenye ulemavu katika shughuli mbalimbali kutokana na ulemavu walionao.
=30=

No comments:

Post a Comment