Saturday, December 16, 2017

MKOA WA IRINGA UMEONGEZA KIWANGO CHA UFAULU KWA 0.27%



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Iringa
Mkoa wa Iringa umefanikiwa kuongeza kiwango cha ufaulu kwa watahiniwa wa mtihani wa kumaliza elimu ya msingi mwaka 2017 kwa asilimia 0.27 na kushika nafasi ya nne kitaifa.

Kauli hiyo ilitolewa na mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi wa wanafunzi wanaotarajia kujiunga na kidato cha kwanza mwaka 2018 mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu katika hotuba yake ya ufunguzi kwenye ukumbi wa Siasa ni Kilimo mjini Iringa.
 
Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu
Ayubu alisema “watahiniwa 20,606 (wavulana 9,513 na wasichana 11,093) sawa na asilimia 83.14 wamefaulu mtihani huo. Hali kadhalika walioshindwa kufaulu mtihani huo ni 4,178 ikiwa wavulana 1,908 na wasichana 2,270 sawa na asilimia 16.86.
Kiwango hiki cha ufaulu kimeongezeka kwa asilimia 0.27 ikilinganishwa na matokeo ya mwaka jana ambapo ufaulu ulikuwa ni 82.87% ninapenda kuchukua nafasi hii kuwapongeza wadau wote wa elimu katika Mkoa wetu ambao mchango wao ni mkubwa kwa ongezeko hili la ufaulu na kuufanya Mkoa wetu kuwa wa Nne kitaifa kati ya mikoa 26 ya Tanzania bara”.

Ayubu ambaye pia ni Katibu Tawala Mkoa wa Iringa alisema kuwa ongezeko hilo la ufaulu ni jambo jema na kutahadharisha kuwa linaibua changamoto ya uhitaji mkubwa wa vyumba vya madarasa katika shule za sekondari. “Ongezeko la ufaulu ni jambo jema kwetu lakini linaibua changamoto ya uhitaji mkubwa wa vyumba vya madarasa katika shule zetu za sekondari au ujenzi wa shule mpya za Sekondari ili kuweza kuwachukua wanafunzi wote waliofaulu kujiunga na kidato cha kwanza” alisema Ayubu.

Aidha, aliwataka wajumbe kuangalia jinsi ya kuongeza vyumba vya madarasa au kujenga shule za sekondari maeneo ambayo yamekuwa na wanafunzi wengi wanaofaulu hasa mijini. Aliongeza kuwa ongezeko la ujenzi wa vyumba vya madarasa liambatane na uongezaji wa meza na viti ili kuhakikisha wanafunzi wote wanapata meza na viti.

Mkoa wa Iringa ulikuwa na watahiniwa 24,905 waliosajiliwa kufanya mtihani wa kumaliza elimu ya msingi mwaka 2017, kati yao wavulana 11,490 na wasichana 13,415 katika shule 481.
=30=

No comments:

Post a Comment