Monday, December 4, 2017

MUFINDI YABAINI WATEJA 31 WALIOJIUNGANISHIA UMEME KINYUME NA TARATIBU



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Wilaya ya Mufindi imefanikiwa kuwabaini wateja 31 waliojiunganishia umeme kinyume na taratibu na kuchukuliwa hatua za kisheria katika jitihada za kudhibiti upotevu wa umeme na mapato ya serikali.

Kauli hiyo ilitolewa na Katibu Tawala Wilaya ya Mufindi, Allan Benard alipokuwa akisoma taarifa fupi ya Wilaya ya Mufindi kwa waziri wa Nishati aliyefanya ziara ya kukagua viwanda vya kuzalisha nguzo wilayani Mufindi hivi karibuni.

Benard alisema kuwa jumla ya wateja 9,382 walihakikiwa na kukaguliwa na kati yao, wateja 31 walibainika kuwa wamejiunganishia umeme kinyume na taratibu. Alisema kuwa wateja hao wamechukuliwa hatua za kisheria kwa kulisababishia shirika la ugavi wa umeme kukosa mapato. 

Alisema kuwa Wilaya ya Mufindi imefanikiwa kubadilisha mita zote za kawaida za umeme (convection) na kufunga mita la Luku ambazo zimesaidia kuongeza wigo wa ukusanyaji mapato.

Akiongelea viwanda wilayani Mufindi, Benard alisema kuwa Wilaya hiyo ina fursa mbalimbali za uwezeshaji wananchi kiuchumi. Alivitaja viwanda vilivyopo kwa mchanganuo kuwa, viwanda vikubwa 14, viwanda vya kati 27 na viwanda vidogo 43. Alisema kuwa viwanda hivyo vimetoa ajira kwa watu 9,171. Aliongeza kuwa kati ya hivyo, viwanda vitano vinazalisha nguzo. Alivitaja kuwa ni Sao Hill Industries, Qwihaya General Enterprises, Sheda General Supply, Leshea na Mufindi Wood Poles and Timber.

Wilaya ya Mufindi ina ukubwa wa eneo la kimometa za mraba 7,123, halmashauri mbili na majimbo matatu ya uchaguzi.    
=30=

No comments:

Post a Comment