Monday, December 4, 2017

MAAFISA MAENDELEO WATAKIWA KUHAMASISHA UJENZI WA VYOO IRINGA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa-Iringa
Maafisa maendeleo ya jamii wa halmashauri watakiwa kushiriki katika kuhamasisha kampeni ya ujenzi wa vyoo ili kuwa na jamii yenye vyoo bora na isiyokuwa na magonjwa ya mlipuko.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, Amina Masenza wakati akifanya majumuisho ya ziara yake ya kukagua hali ya ujenzi wa vyoo katika halmashauri ya wilaya ya Iringa jana.

Masenza alisema “kasi ya ujenzi wa vyoo bora si ya kuridhisha. Kuna haja ya kufanya tathimini ya kampeni ya ujenzi wa vyoo katika mkoa wa Iringa ili tuone jinsi ya kujipanga zaidi na kubadilisha mkakati. Lazima ufike wakati tusema katika Mkoa wa Iringa kutokuwa na choo bora mwisho”. 

Aliongeza kuwa maafisa maendeleo ya jamii hawajatumika ipasavyo katika kampeni ya ujenzi wa vyoo. Aliziagiza mamlaka za serikali za mitaa kuwatumia maafisa hao ili wasaidie uhamasishaji jamii katika ujenzi wa vyoo bora kwa wananchi. Aidha, aliwataka watendaji wa Kata na Vijiji kutekeleza wajibu wao katika kusimamia ujenzi wa vyoo katika maeneo yao ili zoezi hilo likamilike mapema.

Wakati huohuo, kaimu afisa mazingira katika ofisi ya mkuu wa Mkoa wa Iringa, Hawa Mwechaga alisema kuwa baadhi ya vyoo vinavyojengwa ni vidogo kiasi cha kutosha kuwahifadhi watu wembamba pekee. Alishauri kuwa wananchi waelimishwe na kusimamiwa ili wajenge vyoo vyenye nafasi ya kutosha kuweza kuwahifadhi hata watu wanene. Alisema kuwa choo ni muhimu kiwe na nafasi kwa sababu kinamsitiri na kumuhifadhi mtumiaji wake.

Mkuu wa mkoa wa Iringa alifanya ziara ya kukagua hali ya usafi wa mazingira na ujenzi wa vyoo katika kata za Isakalilo, Mseke na Mgama katika halmashauri ya wilaya ya Iringa
=30=

No comments:

Post a Comment