Monday, December 4, 2017

UMEME WAKWMISHA UJENZI WA VIWANDA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Upungufu wa upatikanaji wa umeme umekuwa kikwazo katika juhudi za uanzishaji wa miradi ya kiuchumi na ujenzi wa viwanda mkoani Iringa.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipokuwa akiwasilisha taarifa fupi ya Mkoa wa Iringa kwa waziri wa Nishati ofisini kwake jana.

Masenza alisema “mheshimiwa waziri, pamoja na utekelezaji huu wa kusukuma maendeleo ya wananchi, kumekuwa na changamoto kadhaa zinazochelewesha juhudi hizi. Baada ya wananchi kuitikia wito wa uanzishaji miradi ya kiuchumi ikiwemo ujenzi wa viwanda, pamekuwa na upungufu katika kupatikana kwa umeme wa uhakika. Maeneo yanayokumbwa na tatizo hili ni pamoja na Iringa mjini na wilaya ya Mufindi”. 

Changamoto nyingine ni miradi mikubwa ya kufua umeme inahitaji uwekezaji mkubwa na fedha nyingi, hivyo kuwa kikwazo kwa wananchi wazalendo na kushauri serikali kuwa na udhamini kwa miradi hiyo. 

Mkuu wa Mkoa alisema kuwa Mkoa utaendelea kukabiliana na changamoto hizo kwa kushirikiana na wadau kwa kuwa na ramani itakayoonesha maeneo ya viwanda. “Ramani hii ikikamilika itawasilishwa kwenye mamlaka zinazosimamia miundombinu kama umeme, maji, barabara ili kuhakikisha Mkoa unakuwa na mazingira bora na wezeshi kwa ujenzi na uendelezaji wa viwanda” alisema mkuu wa Mkoa.

Waziri wa Nishati alifanya ziara ya siku moja kukagua viwanda vinavyozalisha nguzo mkoani Iringa ili kujiridhisha na uwezo wa viwanda hivyo kuzalisha nguzo nchini.
=30=

No comments:

Post a Comment