Monday, December 4, 2017

VIWANDA 209 KUCHANGIA PATO LA MKOA IRINGA



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Mkoa wa Iringa una viwanda 209 vinavyotoa ajira kwa zaidi ya wakazi 7,000 na kuchangia katika pato la Mkoa na Taifa.

Kauli hiyo ilitolewa na mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza ofisini kwake alipokuwa akiwasilisha taarifa fupi ya Mkoa wa Iringa kwa waziri wa Nishati, Dr Medard Kalemani wakati wa ziara yake mkoani Iringa jana.

Masenza alisema “Mkoa wa Iringa una viwanda 209 vinavyotoa ajira ya watu 7,470. Mchanganuo unaonesha viwanda 184 vilianzishwa kabla ya serikali ya awamu ya tano kuingia madarakani na viwanda 25 vilianzishwa baada yake”. 

Akiongelea viwanda hivyo kisekta, alisema kuwa Mkoa una viwanda 12 vinavyojishughulisha na uongezaji thamani katika sekta ya Nishati. Aliongeza kuwa viwanda hivyo vinazalisha umeme, nguzo za umeme, kutumia vumbi la mbao kuzalisha mkaa unaotumika viwandani na majumbani.

Mkuu wa Mkoa alisema kuwa kutokana na kuongezeka matumizi ya mazao ya miti, Mkoa kwa kushirikiana na wadau umeanzisha chuo kinachotoa mafunzo yanayohusu stadi za kilimo bora cha miti. Mafunzo yanayotolewa katika kiwanda hicho aliyataja kuwa ni jinsi ya kuchakata na kupunguza upotevu mwingi wa mazao ya miti wakati wa kuchakata, jinsi ya kupanda na kutunza miti. Mafunzo mengine aliyataja kuwa ni uandaaji wa vitalu vya miche ya miti kitaalam na kuandaa shamba la miti.

Waziri wa Nishati alifanya ziara ya siku moja kukagua viwanda vinavyozalisha nguzo mkoani Iringa ili kujiridhisha na uwezo wa viwanda hivyo kuzalisha nguzo nchini.
=30=

No comments:

Post a Comment