Monday, December 4, 2017

TASAF KUNUFAISHA WANAFUNZI KUSOMA KWA BIDII



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa
Mpango wa kunusuru kaya masikini (TASAF) una lenga kuhakikisha wanafunzi wanufaika wa mpango huo wanapata huduma za msingi zitakazowawezesha kusoma kwa bidii.

Kauli hiyo ilitolewa na Katibu Tawala Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu alipokuwa akiongea na wanafunzi wanufaika wa mpango wa TASAF kupitia elimu katika shule ya msingi Kibwabwa iliyopo Kata ya Kitwiru Manispaa ya Iringa hivi karibuni.

Ayubu alisema kuwa serikali kupitia TASAF imelenga kumuwezesha mtoto wa kitanzania kufikia malengo yake kupitia fursa ya elimu. Alisema kuwa kutokana na umuhimu wa elimu kwa wananchi, serikali ya awamu ya tano chini ya uongozi wa Rais Dr. John Magufuli iliamua kutoa elimu bila malipo ili watoto wote wa kitanzania wapate fursa hiyo. 

Kupitia mpango wa TASAF, serikali inatoa fedha ili wanafunzi wanaotoka katika kaya zisizo na uwezo waweze kugharamia mahitaji ya muhimu kwa mwanafunzi. Mahitaji hayo ni sare, viatu, madaftari, kalamu na masweta ili kujikinga na baridi” alisema Ayubu.

Wakati huohuo, Katibu Tawala Mkoa aliwashukuru kamati ya usimamizi ngazi ya jamii (CMC) kwa kazi nzuri kuwasimamia wanufaika katika kufikia malengo ya mpango wa TASAF. “Tuendelee kusimamia vizuri ili kuleta mafanikio yaliyokusudiwa. Lazima kuwakumbusha wanufaika kuwa pesa za TASAF si za burebure, serikali inaona wananchi wake wanakosa baadhi ya mahitaji ya msingi, hivyo fedha hiyo ni kwa ajili ya kusaidia kufikia mahitaji hayo” alisema Ayubu.

Katibu Tawala Mkoa wa Iringa alifanya ziara maalum ya ufuatiliaji kwa wanafunzi wanufaika wa mpango wa TASAF kupitia elimu katika Manispaa ya Iringa kujifunza changamoto zinazowakabili. Katika ziara hiyo aliambatana na mratibu wa TASAF Mkoa, afisa mipango, mhasibu, mkaguzi wa ndani na afisa habari.

No comments:

Post a Comment