Wednesday, September 13, 2017

IRUWASA YAPONGEZWA KUTENGA SIKU YA KUSIKILIZA KERO ZA WANANCHI



Na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, IRINGA
Mamlaka ya majisafi na usafi wa mazingira Iringa mjini (IRUWASA) imepongezwa kwa utekelezaji wa agizo la mkuu wa mkoa wa Iringa la kutenga siku ya kusikiliza na kutafuta ufumbuzi wa kero na malalamiko ya wananchi.

Pongezi hizo zimetolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, mheshimiwa Amina Masenza alipotembelea Iruwasa kukagua utekelezaji wa agizo lake mkoani Iringa.
Afisa Uhusiano IRUWASA Restituta Sakila (kushoto) akimuonesha jambo Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza alipotembelea taasisi hiyo kukagua wanavyopokea na kusikiliza Malalamiko ya wananchi

Nianze kwa kuwapongeza IRUWASA kwa kazi nzuri mnayofanya kupokea na kusikiliza kero na malalamiko ya wananchi. Mheshimiwa Rais Dr John Magufuli amekuwa akipokea barua nyingi za malalamiko ya wananchi. Malalamiko mengine ni madogo madogo ambayo sisi wasaidizi wake tunaweza kuyatatua. Ni matarajio ya mheshimiwa Rais kuona kero na malalamiko yote ya wananchi yanapatiwa ufumbuzi. Hili mnalotekeleza IRUWASA ni sehemu ya utekelezaji wa dhamira ya mheshimiwa Rais” alisema mheshimiwa Masenza.

Akiongelea changamoto ya upotevu wa maji inayowakabili wananchi wengi wanaohudumiwa na IRIWASA, mkuu wa mkoa aliwataka kuweka utaratibu maalum wa kupitia miundombinu ya mtandao wa mabomba ili kujiridhisha na uimara wake. Aidha, aliwataka IRUWASA kutafuta ufumbuzi wa mita za maji za malipo kabla ya huduma ya maji ambazo wateja wengi wametokea kuzipenda.

Katika taarifa ya mkurugenzi mtendaji wa IRUWASA, Gilbert Kayange kwa mkuu wa mkoa wa Iringa kuhusu usikilizaji na utatuzi wa kero na malalamiko ya wananchi alisema kuwa, jumla ya wananchi 79 waliwasilisha kero na mlalamikoa yao. 

Kati ya kero na malalamiko 79 yaliyowasilishwa, 71 yalipatiwa ufumbuzi na wananchi kuridhika. Kero nane tunaendelea kuzishughulikia ambazo ni wananchi kuhitaji huduma ya kuunganishwa na mtandao wa maji” alisema Kayange.

Kayange alisema kuwa IRUWASA imefanikiwa kufikisha huduma ya maji kwa 96% ya wakazi wa Manispaa ya Iringa. Aliongeza kuwa mamlaka yake inaendelea kushughulikia tatizo la kufikisha huduma ya maji katika maeneo ya Kitwiru, Igumbilo na Isakalilo.

Mkurugenzi mtendaji wa IRIWASA, alisema kuwa 90% ya malalamiko ya wananchi yanatokana na ukubwa wa bili za maji na mivujo ya maji. Aliongeza kuwa awali wananchi walikuwa wakifanyiwa tathmini ya vifaa na wananchi kununua vifaa wenyewe jambo lililosababisha ununuzi wa vifaa vilivyo chini ya kiwango na kuchangia katika uvujaji wa maji. 

Alitaja changamoto ya mita za huduma ya malipo kabla kuwa zinapendwa na wateja wengi zaidi na mamlaka haina uwezo wa kuwafungia wateja wote na kusababisha mita hizo kufungwa kimkakati.

Mkuu wa mkoa wa Iringa, yupo katika ziara ya kukagua utekelezaji wa agizo lake kwa taasisi za umma kutenga siku maalum ya akusikiliza kero na malalamiko ya wananchi na kuyatafutia ufumbuzi. Katika siku yake ya kwanza alitembelea taasisi za IRUWASA, TANESCO, TRA na Ofisi ya mkuu wa wilaya ya Iringa.
=30=

No comments:

Post a Comment