Wednesday, September 13, 2017

OFISI ZA UMMA ZATAKIWA KUTENGA SIKU YA KUSIKILIZA MALALAMIKO YA WANANCHI



Na. Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, IRINGA
Ofisi za serikali mkoani Iringa zimetakiwa kutenga siku maalum kwa ajili ya kusikiliza kero na malalamiko ya wananchi na kutafuta ufumbuzi wake.

Agizo hilo lilitolewa na mkuu wa mkoa wa Iringa, Mheshimiwa Amina Masenza baada ya kutembelea ofisi za TANESCO, IRUWASA, TRA na Ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Iringa kujiridhisha na utekelezaji wa agizo lake la kutenga siku moja kwa wiki kusikiliza kero na malalamiko ya wananchi.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza

Mheshimiwa Masenza alisema kuwa wananchi wanakero na malalamiko mengi yanayokwamisha mustakabari wao wa kila siku. Kero na malalamiko hayo yamekuwa yakiwakwamisha kutekeleza majukumu yao ya kila siku na wakati mwingine kuishia kuilalamikia serikali iliyo madarakani. 

Kwa kuwa nchi yetu inafuata misingi ya utawala bora na utawala wa sheria, uliojikita katika kutoa huduma bora kwa wananchi, niliziagiza ofisi za umma mkoani Iringa kutenga siku maalum ya kusikiliza kero na malalamiko ya wananchi na kuitangaza siku hiyo ili wananchi waifahamu” alisema mheshimiwa Masenza. 

Katika kufanikisha agizo hilo, Mkuu wa Mkoa amezitaka ofisi za umma kuunda kamati kwa ajili ya kupokea na kusikiliza kero na malalamiko ya wananchi na kuyatafutia ufumbuzi wa kudumu na kutoa mrejesho kwa wananchi walalamikaji. 

Upokeaji na usikilizaji wa kero na malalamiko ya wananchi uende sambamba na kuorodhesha kero na malalamiko hayo katika daftari la kudumu likionesha jina la mlalamikaji, aina ya lalamiko, afisa aliyepokea lalamiko husika, tarehe ya kupokea na kulitatua, mrejesho na maoni” alisisitiza mheshimiwa Masenza.

Ofisi ya mkuu wa mkoa wa Iringa imetenga siku ya jumatatu ya kila wiki ya kazi kwa ajili ya kupokea, kusikiliza na kutatua ufumbuzi wa kero na malalamiko ya wananchi.
=30=

No comments:

Post a Comment